Hamia kwenye habari

Ndugu Mark Sanderson akionyesha Biblia zilizotolewa katika lugha ya Kwangali, Sepulana, na Setswana

MACHI 10, 2021
AFRIKA KUSINI

Biblia Tatu Zatolewa Nchini Afrika Kusini

Biblia Tatu Zatolewa Nchini Afrika Kusini

Machi 7, 2021, wahubiri wanaozungumza lugha za Kwangali, Sepulana, na Setswana nchini Afrika Kusini walipokea zawadi ya pekee. Katika hotuba iliyorekodiwa mapema, Ndugu Mark Sanderson wa Baraza Linaloongoza alitoa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Kwangali na Sepulana na pia akatoa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa katika lugha ya Setswana. Wahubiri walitazama programu hiyo ya pekee kupitia video iliyounganishwa kwenye mtandao, na Biblia hizo zilipatikana kwa njia ya kidijitali.

Kwangali

Kikundi cha watafsiri watatu kilikamilisha kazi ya kutafsiri katika miaka miwili. Wahubiri zaidi ya 240 katika eneo hilo sasa wana tafsiri inayoweza kueleweka kwa urahisi na itakayoboresha funzo lao la kibinafsi na huduma yao.

Sepulana

Watafsiri sita walishughulikia mradi huo, ambao ulichukua mwaka mmoja na nusu hivi kukamilika. Kuna wahubiri 374 wanaozungumza lugha ya Sepulana nchini Afrika Kusini.

Mtafsiri mmoja alisema hivi: “Tunaposhiriki katika kazi ya kuhubiri, mara nyingi tulitumia tafsiri ya lugha ya Sepedi. Hata hivyo, kabla ya kuelezea Andiko, tulihitaji kwanza kumfafanulia mwenye nyumba au kumtafsiria neno moja au zaidi katika mstari huo. Lakini sasa tukiwa na tafsiri hii, tunahitaji kusoma tu mara moja na kila mtu ataelewa mara moja.”

Setswana

Mradi huu wa kurekebisha tafsiri hii ulichukua miaka minne kukamilika. Watafsiri sita walishughulikia mradi huo. Zaidi ya wahubiri 5,600 wanatumikia katika eneo la lugha ya Setswana.

Mtafsiri mmoja alisema hivi kuhusu Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kitswana: “Tafsiri hii itawasaidia wahubiri kukazia fikira kuboresha ustadi wao katika huduma badala ya kufafanua maneno magumu. Pia kitakuwa kifaa kizuri kwa ajili ya kujifunzia. Wahubiri wataweza kuwazia masimulizi ya Biblia wanapotumia chati, ramani, picha, na kamusi.”

Biblia hizo mpya zitawasaidia ndugu na dada zetu na wote tunaowahubiria kutosheleza uhitaji wao wa kiroho. Tunathamini sana chakula kingi cha kiroho tunachopata leo.—Isaya 65:13.