Hamia kwenye habari

Juu: Ndugu na dada huko Vlorë, Albania, mwaka wa 1930. Juu kulia: Broshua zinazoonyesha historia ya kitheokrasi nchini Albania. Chini kulia: David Splane wa Baraza Linaloongoza akitoa Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Utii wa Kimungu” la 2005

JANUARI 7, 2022
ALBANIA

Kuhubiri Habari Njema kwa Miaka 100 Nchini Albania Licha ya Kupigwa Marufuku kwa Miaka Mingi

Kuhubiri Habari Njema kwa Miaka 100 Nchini Albania Licha ya Kupigwa Marufuku kwa Miaka Mingi

Mwaka wa 2022, Mashahidi wa Yehova wanatimiza miaka 100 nchini Albania.

Nasho Idrizi alikuwa mmoja kati ya Waalbania wa kwanza kukubali kweli. Alipokuwa akiishi nchini Marekani katika miaka ya mapema ya 1920, alijifunza Biblia na International Bible Students, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo.

Nasho alirudi Albania mwaka wa 1922. Hatimaye, Waalbania wengine ambao walikuwa Wanafunzi wa Biblia walipokuwa wakiishi nchini Marekani walirudi nyumbani na kuwafundisha watu mambo waliyokuwa wamejifunza.

Thanas Duli

Thanas Duli alikuwa mmoja kati ya Wanafunzi wa Biblia wa mapema nchini Albania. Anasema hivi: “Mwaka wa 1925, kulikuwa na makutaniko matatu yaliyopangwa nchini Albania kutia ndani Wanafunzi wa Biblia na watu wanaopendezwa waliokuwa wakiishi maeneo mbali nchini kote.”

Katika miaka hiyo ya mapema, machapisho kadhaa yalitafsiriwa katika Kialbania, kama vile The Harp of God na A Desirable Government. Toleo la Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1925 lilisema kwamba “watu waligawiwa kiasi kikubwa [cha machapisho ya Kialbania], na Waalbania wengi wanajifunza kweli kwa shangwe.”

Argjiro na Nasho Dori

Watu wakaanza kuwaita Mashahidi ungjillorë, jina linalomaanisha “waeneza-injili,” kwa sababu ya bidii yao ya kuhubiri. Nasho Dori, aliyebatizwa mwaka wa 1930, anakumbuka hivi: “Katika mwaka wa 1935, kikundi fulani kati yetu tulikodi basi ili tukahubiri katika mji wa Këlcyrë. Baada ya hapo, tulipanga safari kubwa zaidi ya Albania, tukitembelea miji ya Përmet, Leskovik, Ersekë, Korçë, Pogradec, na Elbasan. Tulimalizia safari hiyo katika mji wa Tirana kabla tu ya kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo.”

Katika mwaka wa 1939, serikali ya Kifashisti ya Italia ilidhibiti Albania na kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova. Suala la kutounga mkono upande wowote likawa jambo kubwa kwa sababu akina ndugu walikataa kubeba silaha wakati wa Vita vya Ugiriki na Italia. a Katika miaka hiyo, ndugu 15 walifungwa gerezani. Ndugu Nikodhim Shyti alipelekwa katika kambi ya mateso na hakuonekana tena.

Kufikia mwisho wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Chama cha Komunisti kilianza kutawala Albania mwaka wa 1944. Mateso yaliendelea. Wengi kati ya ndugu zetu walifungwa na kuteswa. Wengine walipelekwa katika kambi za kazi ngumu mbali na familia zao. Katika miaka hiyo, Albania ilitengwa na ulimwengu. Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova​—1959 kiliripoti hivi: “Ingawa watawala wa nchi wanaweza kuwatenga ndugu zetu nchini Albania na Sosaiti ya Ulimwengu Mpya, hawawezi kuzuia roho takatifu ya Mungu isitende juu yao.” Mwaka wa 1967, Albania ilijitangaza kuwa taifa la kwanza kuamini kwamba hakuna Mungu. Kikundi kidogo cha Mashahidi waliokuwa huko waliendelea kuabudu kwa busara.

Baada ya kuanguka kwa Ukomunisti, Mashahidi wa Yehova walitambuliwa kisheria Mei 22, 1992, baada ya kuwa chini ya marufuku kwa miaka 50.

Sasa kuna Mashahidi 5,550 nchini Albania, wanaotumikia katika makutaniko 89. Tunashangilia pamoja na ndugu zetu kwamba “kwa njia yenye nguvu, neno la Yehova likazidi kukua na kusitawi” licha ya mateso makali.​—Matendo 19:20.

a Vita vya Ugiriki na Italia vilipiganwa kati ya Oktoba 28, 1940 na Aprili 23, 1941. Vita hivyo vilikuwa mwanzo wa shambulizi dhidi ya eneo la Balkan wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu.