Hamia kwenye habari

Mwongozo uliotolewa na Wizara ya Elimu ya Kenya

JUNI 7, 2022
KENYA

Serikali ya Kenya Imetoa Mwongozo Unaolinda Haki za Wanafunzi

Serikali ya Kenya Imetoa Mwongozo Unaolinda Haki za Wanafunzi

Wizara ya Elimu nchini Kenya imetoa mwongozo unaowahimiza wakuu wa shule kulinda haki za kidini za wanafunzi. Mwongozo huo ulitolewa Machi 4, 2022. Tunatumaini kwamba hilo litasaidia kulinda haki za watoto wa Mashahidi wa Yehova, ambao kwa miaka mingi wamekuwa wakibaguliwa kwa sababu ya imani yao.

Tangu mwaka wa 2015, watoto 36 ambao ni Mashahidi wa Yehova wamefukuzwa shuleni au kusimamishwa kwa muda kwa sababu ya kukataa kushiriki sherehe za kidini ambazo wanafunzi wote wanaamuriwa kushiriki. Mwaka wa 2018, wawakilishi wa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova jijini Nairobi, walifanya mkutano na maofisa wa elimu nchini Kenya ili kuzungumzia suala hilo. Oktoba 23, 2018, wawakilishi hao walikutana na Dkt. Amina Mohamed ambaye alikuwa Waziri wa Elimu wakati huo.

Mwongozo huo wa serikali unakiri hivi: ‘Wakuu wa shule nchini Kenya wanatumia sababu zisizo za msingi kuwafukuza wanafunzi shuleni.’ Pia, mwongozo huo umekazia jambo hilo kwa kusema: “kihususa, . . . baadhi ya shule zinakiuka haki za kidini za wanafunzi kwa kukataa wajiunge na shule hizo au kwa kuwafukuza shuleni kwa sababu ya imani yao.”

Mwongozo huu umejadiliwa sana nchini Kenya. Vituo vya habari vimesema kwamba mwongozo huo umekazia hili: “Kukiuka haki za kidini kunapingana na sheria za kitaifa, mikataba ya maeneo mbalimbali na ya kimataifa, . . . na kihususa inapingana na Katiba ya Kenya.” Kwa hiyo, watoto wa Mashahidi na wengine hawawezi “kulazimishwa kushiriki katika utendaji ambao ni kinyume na imani yao.” Mwongozo huo ulimalizia kwa kuwaomba wakuu wa shule kutekeleza sheria hiyo.

Kimberly Nyang’ate, ambaye ni dada mwenye umri wa miaka 17 jijini Nairobi, anasema hivi: “Wazazi wangu wameitwa zaidi ya mara tano shuleni kwa sababu nilikataa kushiriki katika sherehe za kidini. Ninafurahi kwamba tuna mwongozo huu utakaolinda uamuzi wetu unaotegemea Biblia.”

Tunashukuru kwamba wakuu hawa wenye usawaziko wametoa mwongozo huo utakaowasaidia watoto wetu wanaoenda shule nchini Kenya kuendelea kubaki imara katika imani yao.​—1 Wakorintho 15:58.