Hamia kwenye habari

MACHI 11, 2021
MAREKANI

Kuandika Barua Kunaendelea Kuwa na Matokeo Yenye Kutia Moyo

Kuandika Barua Kunaendelea Kuwa na Matokeo Yenye Kutia Moyo

Mashahidi wengi wa Yehova wanapata shangwe kuwahubiria wengine kwa kuandika barua. Mambo yaliyoonwa yafuatayo kutoka Marekani yanaonyesha kwamba jitihada hizo zinasaidia kueneza ujumbe wa Biblia wenye kufariji.

Dada Carlee Ruggles akiwa na mama yake wakitafuta maandiko ya kuandika katika barua zao

Dada Carlee Ruggles, mwenye umri wa miaka 13, anayeishi Blue Ash, Ohio, aligundua jinsi kuandika barua kunawasaidia watu sana alipopata majibu yasiyotarajiwa.

Alasiri moja, Carlee alikuwa nje ya nyumba yake alipoona pikipiki. Dereva wa pikipiki hiyo alishuka akiwa ameshika bahasha na kuuliza kwa sauti kubwa: “Nani alinitumia barua hii?” Carlee alitambua hiyo ni barua ambayo yeye alikuwa ameandika alipokuwa akishiriki katika huduma.

Wazazi wa Carlee walipotoka nje kusimama kando yake, Carlee alisema kwa ujasiri, “Ni mimi.”

Yeye na wazazi wake walishangaa mtu huyo aliposema, “Barua yako ilinifaa kabisa!” Mwanamume huyo alisimulia jinsi barua hiyo ilivyomfariji kwa sababu alikuwa akikabiliana na upweke kutokana na hali zinazotokana na ugonjwa wa corona. Pia alieleza kwamba ndugu yake alikufa hivi karibuni na kwamba barua ya Carlee ilimfariji alipokuwa akiomboleza.

Alimalizia kwa kusema hivi: “Usiache kuwaandikia watu barua. Barua hizo zinagusa mioyo ya watu, iwe watajibu au la.”

Sasa Carlee ameazimia kuendelea kuwaandikia majirani wake barua. Anasema hivi: “Nilifurahi sana kwamba Yehova alinitumia kumtia moyo mtu. Mambo tunayoandika yanaweza kumsaidia sana mtu mwenye uhitaji.”

Dada Myrna Lopez akiwa Center, Texas

Dada Myrna Lopez, anayeishi katika eneo la Center, Texas, alikuwa ameanza kuwa na wasiwasi ikiwa barua zake zilikuwa zikiwasaidia watu. Kisha akagundua jambo fulani kuhusu mtu wa ukoo wake. Myrna aligundua kwamba mpwa wake alikuwa amefungwa gerezani. Aliamua kumwandikia barua kijana huyo ambaye alikuwa amehudhuria mikutano alipokuwa mtoto, akimhakikishia kwamba Yehova hajamsahau.

Mpwa wake alijibu barua hiyo. Alisema kwamba alijihisi akiwa na wasiwasi baada ya kukamatwa na alikosa kusudi maishani. Sasa akiwa gerezani, alikuwa akifikiria kuhusu maisha yake ya utotoni na akaanza kusoma Biblia na kusali kwa Yehova. Alisema kwamba barua ya Myrna ilikuwa jibu la sala zake na ilimthibitishia kwamba Yehova bado anamjali.

Dada Natalie Bibbs akiwa Norcross, Georgia

Dada Natalie Bibbs, anayeishi Norcross, Georgia, alipata ujumbe kutoka kwa mwanamke ambaye alipata barua yake alipokuwa akifanya mazoezi ya kukimbia. Mwanamke huyo aliona barua hiyo ikiwa imekunjwa kando ya barabara na mwanzoni akakimbia na kuiacha. Lakini kwa sababu ambazo hawezi kuelezea aliamua kurudi na kuichukua.

Mwanamke huyo alimwandikia Natalie hivi: “Nilikabiliana na changamoto nyingi sana juma hili lote na nilitamani jambo zuri litokee. Barua hiyo ilikuwa jambo zuri nililokuwa nikitafuta!”

Natalie anasema: “Kupata ujumbe huo kulinipa uhakika wa kwamba hata tukitumia njia gani ya kuhubiri, Yehova atabariki jitihada zetu.”

Dada Laura Martinez, anayeishi Athens, Texas, huwapa barua wafanyakazi wa duka ambalo yeye hununua bidhaa zake wanapomletea vyakula kwenye gari lake. Mfanyakazi mmoja alimwambia Laura kwamba barua yake ilimgusa moyo sana. Kwa hiyo, Laura akamwandikia mwanamke huyo barua nyingine mbili na sasa anajifunza naye Biblia.

Dada Laura Martinez, akiwa Athens, Texas, anawapa barua wafanyakazi wa duka ambalo yeye hununua bidhaa

Mambo hayo yaliyoonwa yanatukumbusha kwamba ingawa huenda tusijue ni wapi ambapo mbegu zetu za kweli “zitafanikiwa,” Yehova anaweza kubariki njia yoyote tunayotumia katika huduma yetu ili kuwafariji na kuwapa tumaini watu wenye mwelekeo wa kondoo.—Mhubiri 11:6.