Hamia kwenye habari

Kushoto: Maelfu walimsikiliza Ndugu Joseph F. Rutherford alipotoa mwito wa kumtangaza Mfalme na Ufalme wake katika kusanyiko la kihistoria la siku tisa huko Cedar Point, Ohio, Marekani. Kulia: Ndugu Rutherford anatumia kikuza sauti ili wasikilizaji waliokuwa nje ya ukumbi waweze kumsikia

OKTOBA 6, 2022
MAREKANI

Kusanyiko la Cedar Point Lililofanywa Miaka 100 Iliyopita

Maonyesho Mapya ya Tukio Muhimu

Kusanyiko la Cedar Point Lililofanywa Miaka 100 Iliyopita

Miaka 100 iliyopita, Septemba 5-13, 1922, Mashahidi wa Yehova walifanya kusanyiko la siku tisa, huko Cedar Point, Ohio, Marekani. Kusanyiko hilo lilikuwa mojawapo ya matukio muhimu zaidi katika historia yetu ya karibuni. Wajumbe kutoka Kanada, Ulaya, na sehemu mbalimbali za Marekani walihudhuria. Kila siku kulikuwa na wastani wa wahudhuriaji 10,000, na wasemaji tofauti walitoa hotuba ileile, kwa wakati uleule, katika lugha 11.

Maonyesho mapya kuhusu mambo yaliyotokea kwenye kusanyiko hilo na jinsi lilivyosaidia kazi ya kuhubiri kusonga mbele, yamefunguliwa katika makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova. Kwa sasa, maonyesho hayo yanatembelewa na familia ya Betheli peke yake, lakini idhini ya kutembelea ofisi za tawi itakapotolewa, basi watu wengine pia watapata fursa ya kutembelea maonyesho hayo.

Septemba 8 ilikuwa siku muhimu sana ya kusanyiko la Cedar Point. Siku hiyo kulikuwa na wahudhuriaji 8,000 katika ukumbi ulio karibu na Ziwa Erie ambalo ni maridadi sana. Walikuja kusikiliza hotuba ya Ndugu Joseph F. Rutherford yenye kichwa “Ufalme.”

Baada ya kuzungumza kwa dakika 90 Ndugu Rutherford aliinua sauti na kuwauliza wasikilizaji ikiwa waliamini kwamba Kristo alikuwa akitawala. Bila kusita, umati ulijibu kwa sauti, Ndiyo! Kisha Ndugu Rutherford akasema: “Ninyi ndio mawakili wa kumtangaza. Kwa hiyo, mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni.” Wakati huohuo, kitambaa chenye maneno: “Mtangazeni Mfalme na Ufalme,” kikakunjuliwa.

Mwito huo wa kuhubiri habari njema uliwachochea sana wahudhuriaji kuongeza bidii yao. Wasikilizaji wengi tayari walikuwa wameanza kuhubiri, lakini hotuba ya Ndugu Rutherford iliwachochea kuongeza bidii yao hasa katika kipindi hicho ambapo kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ilikuwa ikifanywa kwa utaratibu zaidi. Dada Ethel Bennecoff, ambaye alikuwa anakaribia miaka 30 wakati huo, alisema kwamba baada ya kusikia hotuba hiyo, Wanafunzi wa Biblia walikuwa na “bidii na upendo mwingi moyoni kuliko wakati mwingine wowote.” Dada Odessa Tuck, aliyekuwa na miaka 18 mwaka wa 1922, alisema: “Nilitaka kuwa kama Isaya, aliyesema hivi: ‘Mimi hapa! Nitume mimi!’”

Ubatizo kwenye kusanyiko la 1922 la Cedar Point

Siku mbili baada ya hotuba ya Ndugu Rutherford, Wanafunzi wa Biblia walipitisha azimio. Kwa sehemu, azimio hilo lilisema: “Tukiwa kikundi cha Wakristo ambao wameazimia kumtii na kumfuata Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo, hatukubali kushiriki katika vita, mapinduzi, vurugu, au ukatili wa aina yoyote; tunapinga kabisa kutumia Neno la Mungu au njia nyingine yoyote kuwalaghai na kuwadanganya watu. Sisi tunataka amani.” Azimio hilo lilionyesha waziwazi kwamba Wanafunzi wa Biblia walikuwa tofauti na dini nyingine ambazo zilikuwa zimeunga mkono Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Baadaye dini hizo ziliunga mkono pia Vita vya Pili vya Ulimwengu.

Gazeti Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 1922, lilisema: “Tutafanya yote tuwezayo ili kusanyiko la mwaka wa 1922 liwe kusanyiko bora kabisa kuwahi kufanywa. . . . Ni matumaini yetu kwamba maelfu ya ndugu na dada watakaohudhuria watakumbuka kusanyiko hili kwa miaka mingi.”

Kusudi hilo lilitimia. Miaka mia moja baadaye, Yehova anaendelea kubariki kazi ya kumtangaza Mfalme na Ufalme wake.​—Mathayo 24:14.