Hamia kwenye habari

APRILI 8, 2021
NIGERIA

Mashahidi wa Yehova Watoa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Iliyorekebishwa Katika Kiigbo

Mashahidi wa Yehova Watoa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Iliyorekebishwa Katika Kiigbo

Aprili 4, 2021, Ndugu Kenneth Cook, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa katika Kiigbo kwenye mkutano wa pekee kupitia mtandao. Wahubiri katika makutaniko 1,140 ya Kiigbo nchini Nigeria, walifurahi sana kupata Biblia hiyo iliyorekebishwa. Biblia hiyo imetolewa miaka 14 baada ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kutolewa katika Kiigbo kwa mara ya kwanza.

Toleo hilo litawanufaisha zaidi ya wahubiri 50,000 walio katika makutaniko na vikundi vya lugha ya Kiigbo. Biblia hiyo itafaa sana katika kuwahubiria watu milioni 40 hivi wanaozungumza Kiigbo.

Mshiriki mmoja wa kikundi cha watafsiri cha Kiigbo alisema hivi: “Kwa kuwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa ina maelezo mengi sana ya chini, Biblia hii inayotumia lugha ya kisasa itawavutia wasomaji wa Kiigbo. Maelezo hayo ya chini hayafafanui tu maneno ya Kiebrania na Kigiriki. Katika visa fulani, maelezo hayo yanaonyesha maneno mengine ya Kiigbo, na katika visa vingine yanaweza kutia ndani maneno yatakayowasaidia wasomaji wanaozungumza lahaja nyingine za Kiigbo kuelewa mambo wanayosoma.”

Ndugu Archibong Ebiti, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Nigeria, alisema hivi: “Iliwachukua watafsiri sita miaka minne kukamilisha kazi hiyo. Ijapokuwa kulikuwa na changamoto zisizotarajiwa kwa sababu ya janga la ugonjwa wa corona, tunamshukuru Yehova kwa kuwapa roho yake wote waliohusika katika mradi huo.”

Tuna uhakika kwamba Mashahidi wanaozungumza Kiigbo ulimwenguni pote, watafurahia kusoma maneno yenye kupendeza ya Biblia hiyo iliyorekebishwa. Pia, wataona kwamba ni rahisi kufundisha na ‘kufafanua kwa usahihi njia za Mungu’ kwa wengine.—Matendo 18:26.