Hamia kwenye habari

APRILI 5, 2019
NIGERIA

‘Mlipuko wa Shangwe’—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Imetolewa Lugha Mbili za Nigeria

‘Mlipuko wa Shangwe’—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Imetolewa Lugha Mbili za Nigeria

Januari 12, 2019, ndugu zetu nchini Nigeria walifanya mkutano wa pekee kwenye Jumba la Kusanyiko la Benin City. Katika mkutano huo, Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova alitangaza kutolewa kwa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa katika lugha ya Isoko na Yoruba. Jumla ya watu 60,672 walisikiliza programu hiyo kwa kuunganishwa kupitia intaneti. Watu waliounganishwa na programu hiyo walikuwa katika Majumba 106 ya Ufalme na Majumba 9 ya Kusanyiko nchini Nigeria, pamoja na maeneo kadhaa katika nchi jirani ya Benin.

Ndugu Jackson akiwa pamoja na familia moja katika Jumba la Kusanyiko la Benin City nchini Nigeria

Ndugu Gad Edia anayetumikia katika ofisi ya tawi ya Nigeria alisema hivi: “Kazi ya kutafsiri Biblia katika lugha ya Isoko ilichukua miaka mitatu na miezi miwili na tafsiri ya lugha ya Yoruba ilichukua miaka mitatu na miezi mitatu.” Alimalizia kwa kusema hivi: “Nchini Nigeria, Mashahidi zaidi ya 5,000 huzungumza Isoko na wengine zaidi ya 50,000 husoma na kuandika Yoruba. Ndugu na dada walipopokea tafsiri iliyorekebishwa, mtu mmoja alisema ni kana kwamba watu ‘walilipuka kwa shangwe.’ Hivyo tunaweza kusema kwa hakika kwamba jitihada zetu hazikuwa za bure!”

Mpaka sasa, Mashahidi wa Yehova wametoa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ikiwa nzima au sehemu katika lugha 179.

Tunafurahi sana kwa kuwa ndugu zetu wanaweza kujifunza Biblia kwa urahisi zaidi sasa katika lugha hizo.—2 Timotheo 3:17.