Hamia kwenye habari

Vijana nchini Timor-Mashariki na wazazi wao wakizungumzia masimulizi yanayopatikana katika sehemu ya Habari za JW

JANUARI 22, 2021
TIMOR-MASHARIKI

Makala za Habari za JW Zaimarisha Vijana wa Timor-Mashariki Kuvumilia Upinzani

Makala za Habari za JW Zaimarisha Vijana wa Timor-Mashariki Kuvumilia Upinzani

Watu wengi wanatiwa moyo kwa kusoma makala za Habari za JW kuhusu ndugu zetu nchini Urusi ambao wanadumisha ushikamanifu licha ya mateso. Hata hivyo, wahubiri wa Timor-Mashariki wana makala tatu tu zilizotafsiriwa katika Kitetun Dili. Moja ya makala hizo ni simulizi la Ndugu Andrey Suvorkov. Siku chache baada ya kutafsiriwa katika Kitetun Dili, vijana watano walikabili jaribu gumu. Wanaeleza jinsi imani yao ilivyoimarishwa kwa kutafakari kielelezo cha ndugu huyo.

Wakati wa sherehe moja iliyofanyika shuleni, vijana hao waliambiwa waisalimu bendera. Walipokataa, walipelekwa kwa mwalimu mkuu wa shule. Aliwahoji mbele ya walimu wengine. Kwa ujasiri na heshima, vijana hao walitoa sababu za Kimaandiko zilizowafanya waamue kukataa kusalimu bendera.

Walimu waliwaita polisi waliowapeleka vijana hao Mashahidi kwenye kituo cha polisi bila kuwataarifu wazazi wao. Polisi hao walipiga simu kwenye kambi ya jeshi na kuomba mwanajeshi mmoja aje na kuzungumza na vijana hao Mashahidi. Kisha, maofisa wa polisi wakiwa na mwanajeshi huyo, walijaribu kuwatisha vijana hao kwa kuwaweka jela kwa nusu saa. Ofisa mmoja hata aliweka silaha juu ya meza mbele ya vijana hao, na kuwahoji kwa zaidi ya saa mbili. Mwishowe, vijana hao Mashahidi waliruhusiwa kwenda nyumbani.

Dada Ruth Ximenes (kulia) pamoja na mama yake, Anita (kushoto)

Wazazi wa vijana hao walipojua kilichotokea, walizungumza na walimu na polisi. Upinzani bado uliendelea, hivyo waliamua kupeleka malalamiko yao kwa maofisa wa serikali katika eneo lao. Mwishowe, vijana hao walilazimika kuhamia shule nyingine.

Vijana hao Mashahidi wanathamini sana kwamba walisoma simulizi la Ndugu Andrey Suvorkov kwa kuwa liliwasaidia kukabiliana na upinzani kutoka kwa vijana wenzao, walimu, na wenye mamlaka.

Noviana Jose do Carmo anakumbuka hivi: “Tuliteswa na walimu wetu na kufukuzwa shule. Hata hivyo, simulizi la Ndugu Suvorkov lilinichochea kuwa mtulivu na mwenye furaha.” Cejiana, dada ya Noviana anasema hivi pia: “Simulizi la Ndugu Suvorkov lilinisaidia kuwa mtulivu ninapokabili majaribu.” Ruth Ximenes anasema kwamba simulizi la ndugu huyo lilimsaidia ‘asikate tamaa.’

Dada Ananda Maria Delavega (kulia) pamoja na mama yake, Juliana (kushoto)

Ananda Maria Delavega anasema kwamba “kielelezo cha Ndugu Andrey Suvorkov cha kumtegemea Yehova, kilinichochea kumtegemea Yehova kupitia sala,” hasa ninapokabili upinzani.

Roni da Cruz anasema: “Kujua kwamba Yehova anawategemeza akina ndugu ulimwenguni pote kulinipa uhakika wa kwamba Yehova alikuwa pamoja nami na sikuwa na sababu yoyote ya kuogopa.”

Wazazi wa vijana hao waaminifu walitaja pia jinsi wanavyothamini masimulizi yanayopatikana katika sehemu ya Habari za JW.

Dada Anita Ximenes, mama ya Ruth, ni mzazi asiye na mume anayelea mabinti wengine wawili. Anita alikuwa na wasiwasi aliposikia majirani wakisema: “Tuwapige wasaliti hawa!” Hata hivyo, Anita anasema hivi: “Mimi hupata ujasiri kwa kujua kwamba ndugu na dada zetu nchini Urusi wanasimama mbele za maofisa wa mahakama wakiwa watulivu. Nimetumia masimulizi yao kuwafundisha binti zangu. Tunamwona Yehova kuwa Baba ambaye sikuzote yuko pamoja nasi.”

Kuanzia kushoto hadi kulia: Roni da Cruz, Cejiana Jose do Carmo, Noviana Jose do Carmo, Ananda Maria Delavega, na Ruth Ximenes katika kusanyiko la eneo la 2019, majuma machache baada ya kupelekwa polisi kwa kukataa kusalimia bendera shuleni

Kama waabudu wenzetu vijana na wazazi wao nchini Timor-Mashariki, tunaimarishwa kwa kutafakari mifano ya ndugu na dada wenye ujasiri ambao licha ya mateso ‘wanatoka wakiwa wameshinda kabisa.’—Waroma 8:37.