Hamia kwenye habari

Kutoka juu kushoto: Mwonekano wa jukwaa, wahudhuriaji, na kikundi cha mfumo wa sauti. Ndugu Mark Sanderson akizungumza na ndugu na dada walionusurika katika shambulizi hilo pamoja na familia zao baada ya programu. Trakti ya programu ya tukio hilo. Kadi na barua za pole. Mashahidi wa Yehova waliocheza muziki kwenye jukwaa. Akina dada vijana wakifarijiana baada ya programu. Wawakilishi wa idara ya polisi na ya wazimamoto wakisubiri programu ianze

APRILI 10, 2023
UJERUMANI

Maelefu ya Watu Wahudhuria Mazishi ya Wale Waliouawa Hamburg

Maelefu ya Watu Wahudhuria Mazishi ya Wale Waliouawa Hamburg

Mashahidi wa Yehova pamoja na watu wengine wengi duniani pote walihuzunishwa sana na mauaji yaliyotokea Hamburg, Ujerumani, Machi 9, 2023 katika Jumba la Ufalme. Ndugu Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova; Ndugu Gajus Glockentin, msaidizi wa Halmashauri ya Utangazaji; na washiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Ulaya ya Kati walisafiri hadi Hamburg ili kuwafariji ndugu na dada zetu na kuwafanyia ziara za uchungaji. Mazishi yao yalifanywa Machi 25 katika ukumbi wa michezo ulio jijini humo. Wale waliotazama programu hiyo inayogusa moyo walihisi wameona nguvu za Biblia za kufariji na kutegemeza wale wanaoomboleza. Watu wengi walihisi kama ndugu mmoja aliyekuwepo katika tukio hilo alivyosema: “Tulihisi kana kwamba Yehova amekuwa akitukumbatia siku ya leo.”

Zaidi ya watu 3,300 walihudhuria programu hiyo ukumbini. Pia, programu hiyo ilirushwa hewani na zaidi ya vifaa 90,000 vilikuwa vimeunganishwa na programu hiyo.

Watu waliohudhuria si ndugu na dada zetu tu, bali pia maofisa wa serikali, wa polisi, wa afya na wazimamoto. Meya wa Kwanza na Meya wa Pili wa Hamburg, Rais wa Bunge la Jiji la Hamburg, Balozi wa Marekani aliye Hamburg, Seneta wa Mambo ya Ndani na Michezo, Mkuu wa Maseneta, Mkuu wa Polisi wa Hamburg, na Makamo wa Rais wa Polisi.

Wahudhuriaji na wanamuziki wakiimba pamoja wimbo wenye kichwa “Kazi za Mungu za Uumbaji”

Programu hiyo ilianza kwa wimbo wa Ufalme, na wimbo huo uliambatana na ala za muziki zilizochezwa na ndugu na dada zetu. Ndugu Joachim Szewczyk, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Ulaya ya Kati, alikuwa mwenyekiti. Naye alimkaribisha Ndugu Dirk Ciupek, ambaye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi pia. Ndugu Dirk alitoa hotuba ya mazishi. Baadaye, Ndugu Ciupek alimkaribisha Ndugu Sanderson, ambaye alitoa hotuba fupi inayotegemea Biblia. Kisha Ndugu Ciupek alirudi kumalizia hotuba ya mazishi. Baada ya hapo waliimba wimbo mwingine wa Ufalme na Ndugu Glockentin alitoa sala ya mwisho.

Katika hotuba ya Ndugu Sanderson, aliwasaidia watu kuelewa kwamba Mungu hasababishi ukatili. Ukweli ni kwamba hayo ni “matukio yasiyotarajiwa” yaliyozungumziwa katika kitabu cha Mhubiri. (Mhubiri 9:11) Ndugu Sanderson alisema: “Matukio haya ya kikatili si mipango ya Mungu, kwa hiyo, hatuhitaji kujiuliza kwa nini Mungu amesababisha jambo hilo . . . Tumaini letu, imani yetu, upendo wetu unaweza kustahimili ukatili. Mambo hayo matatu yanaweza kutusaidia kuvumilia chuki na ukatili wowote.” Hata aliwashukuru maofisa wa polisi, watumishi wa idara ya kushughulikia dharura, na wahudumu wa afya waliowasaidia ndugu na dada zetu.

Ndugu Dirk Ciupek

Ndugu Ciupek aligusa mioyo ya watu katika hotuba yake ya mazishi, alisema hivi: “Shambulizi lililotokea Machi 9, halikuathiri wale waliokuwepo tu bali limetuathiri sisi sote. Sote tupo hapa leo ili kujibu mashtaka ya chuki na ukatili. Tunajibu kwa kuonyesha upendo, huruma, na hisia-mwenzi, na pia tumaini na imani. Maandiko yanasema ‘usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.’ Sisi sote tunataka kufanya hivyo na ndio sababu tupo hapa leo.”​—Waroma 12:21.

Wahudhuriaji walijawa hisia nyingi Ndugu Ciupek alipotaja jina la kila mmoja aliyeuawa aliposema: “Leo tupo hapa ili kuwaaga, na kuwakumbuka Stephan, Sebastian, James na Marie, Stephanie, Dan na mtoto wetu Romy (mtoto ambaye alikuwa hajazaliwa aliyeuawa).” Ndugu Ciupek akawaambia wale walionusurika pamoja na watu wa familia waliokuwa wamehudhuria: “Tunataka kuwa pamoja nanyi watu wao wa ukoo na kuwafariji.”

Alimalizia kwa kutaja sifa zao nzuri ambazo wapendwa wao watakosa sana. Kisha akirejelea Ufunuo 21:4, 5, alisema: “Ni kweli kwamba tunawakosa wapendwa watu waliokufa. Tunawaomboleza. Wataendelea kuwa sehemu ya familia yetu. Siku itakuja Mungu wetu atakapoondolea mbali huzuni tunayohisi sasa, kwa sababu ataikomesha. . . . Kifo hakitakuwapo tena. Huo ndio uliokuwa ujumbe wa Yesu na mitume wake. Hilo ndilo tumaini letu. Kifo kitashindwa. Kifo hakiwezi kutuamulia hatima yetu. Mungu ndiye anayeweza kuamua. . . . Kifo sio mwisho wa Stephan, Sebastian, James na Marie, Stephanie, Dan, na mtoto wetu Romy.”

Meya wa Kwanza wa Hamburg, Dakt. Peter Tschentscher

Baada ya mazishi, maofisa wa serikali walipewa nafasi ya kuzungumza. Meya wa Kwanza wa Hamburg, Dakt. Peter Tschentscher na Rais wa Bunge la Jiji la Hamburg, Bibi Carola Veit, wote wawili waliwapa pole marafiki na watu wa ukoo wa wale waliofiwa. Dakt. Tschentscher alisema kwamba wale walionusurika “wanatenda kwa ujasiri kwa sababu ya jinsi wanavyokabiliana na huzuni wanayohisi” na hilo linatokana na “imani yao ya Kikristo yenye nguvu.” Kwa kuongezea, alisoma barua iliyotayarishwa na Rais wa nchi, Bw. Frank-Walter Steinmeier.

Rais wa Bunge la Jiji la Hamburg, Bibi Carola Veit

Kulikuwa na wanahabari wengi. Mtu mmoja anayefanya kazi katika kituo cha televisheni alisema: “Watu hawa wote wana fadhili na hilo limenivutia sana.” Alisababu hivi: “Tumehudhuria matukio mengi lakini hatujawahi kujionea kitu kama hiki na hata tumeshangazwa na mambo yaliyozungumziwa.”

Mume na mke walionusurika katika shambulizi hilo walisema: “Ni vizuri sana kutafakari tumaini tulilonalo huku tukiomboleza tukiwa tumezungukwa na ndugu zetu.”

Ndugu mmoja anayehudhuria katika kutaniko lingine ambalo linakutanika katika Jumba hilo alisema: “Tumeomboleza kwa muda mrefu. Nilipokuja hapa nilikuwa ninahisi nimechoka kuona hali hiyo lakini programu hii ilikuwa yenye kuchochea. . . . Akina ndugu na wawakilishi wa serikali walizungumza kwa hisia-mwenzi.”

Programu hiyo ilikuwa wonyesho wa wazi wa upendo wa Yehova. Tunajua kwamba “Baba wa rehema nyororo na Mungu wa faraja yote” ataendelea kuwategemeza wale wote walioathiriwa na shambulizi lililotokea Hamburg.​—2 Wakorintho 1:3.

 

Mwonekano wa jukwaa na mwenyekiti, Ndugu Joachim Szewczyk, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Ulaya ya Kati. Wanamuziki stadi ambao ni Mashahidi wa Yehova wameketi nyuma yake

Ndugu Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova akitoa hotuba yenye kufariji inayotegemea Maandiko pamoja na mkalimani wa lugha ya Kijerumani

Maofisa wa serikali wakiwa wameketi kwenye viti vya mbele huku wakisikiliza hotuba

Ndugu na dada wakisalimiana na kutegemezana baada ya programu

Kadi na barua za pole zilizobandikwa kwenye mwingilio wa ukumbi huo

Katika mwingilio wa ukumbi, mtangazaji wa televisheni ya Ujerumani akimhoji mzee mmoja anayeishi Hamburg aliyejuana vizuri na baadhi ya wale waliouawa