Hamia kwenye habari

Kituo cha Wageni cha Patterson kilicho New York, nchini Marekani. Picha ndogo: Wageni wakitembelea maonyesho ya “Kijiji cha Biblia Katika Karne ya Kwanza”

JANUARI 26, 2024
HABARI ZA ULIMWENGUNI POTE

Maonyesho Mapya ya Patterson Yawapa Wageni Fursa ya Kujifunza na Kuchimba Zaidi

Maonyesho Mapya ya Patterson Yawapa Wageni Fursa ya Kujifunza na Kuchimba Zaidi

Januari 1, 2024, Kituo cha Wageni cha Patterson kilicho ndani ya Kituo cha Elimu cha Watchtower kilifunguliwa rasmi New York, nchini Marekani. Sehemu moja yenye kuvutia sana katika maonyesho hayo ni kijiji kinachofanana na siku za Biblia chenye kichwa “Kijiji cha Biblia Katika Karne ya Kwanza.” Ndugu Isaiah Miller, hufanya kazi katika Idara ya Maonyesho Betheli, naye amesema hivi: “Kijiji hicho kilijengwa kwa njia ambayo watu watakapopatembelea wataona na kujifunza jinsi watu walivyoishi katika siku za Yesu. Utafiti umeonyesha kwamba watu wa kila umri hunufaika zaidi wanapopata fursa ya kutumia uwezo wao wa kudadisi ili kujifunza.” Mgeni mmoja alipomaliza matembezi alisema hivi: “Nilipokuwa katika maonyesho nilihisi kana kwamba nilipata kufika kwenye nchi ya Israeli ya kale. Inapendeza sana!”

Sehemu hii pia inawasaidia watu kujua kuhusu wanyama, chakula, mimea, na mazoea ya kila siku ya wale walioishi katika karne ya kwanza nchini Israeli. Kwa mfano, miti ya mizeituni iliyopo inatokana na mifano iliyotengenezwa kwa mkono ya miti ya mzeituni iliyo Israeli. Wageni wanaweza kusaga nafaka kwenye jiwe la kusagia na hata kupanda mashua iliyotumiwa na wavuvi inayofanana na mashua kama zile ambazo Yesu na wanafunzi wake walitumia. Ndugu mmoja alisema hivi kwa shangwe: “Ninahisi kana kwamba nilikuwa nikiingia kwenye simulizi la Biblia mara tu Yesu alipoiambia bahari: ‘Nyamaza, utulie!’” (Marko 4:39) Wageni wanapotembelea jengo la mfano la sinagogi la kale, wanaweza kuwazia wakiwa wameketi wakisikiliza Neno la Mungu likisomwa kwa sauti kubwa.

Kushoto hadi kulia: Maonyesho ya “Kijiji cha Biblia Katika Karne ya Kwanza,” Maonyesho ya “Wana Wako Wote Watafundishwa na Yehova,” na maonyesho ya “Kutetea na Kuthibitisha Kisheria Habari Njema”

Rebecca na Marcos wakijifunza jinsi ya kutengeneza kiti cha mbao wakiwa ndani ya Kijiji cha Biblia

Fursa nyingine ya pekee ambayo wageni wanapewa ni ya kujifunza kuhusu maisha ya watu walioishi katika karne ya kwanza. Ndugu na dada ambao ni wageni wanaweza kuongea na “wanakijiji Waisraeli” ambao ni ndugu na dada zetu. Wageni wanaweza kujaribu kufanya shughuli na kazi mbalimbali zilizofanywa katika siku za Yesu. Marcos mwenye umri wa miaka kumi alisema, “Sehemu niliyofurahia zaidi ni pale nilipomsaidia seremala Mwisraeli kutengeneza kiti!” Rebecca mwenye umri wa miaka minane alisema, “Mimi pia nilifurahia sehemu hiyo zaidi, pia nilifurahia kusaga ngano ili kupata unga.”

Kuna sehemu nyingine tatu katika kituo hicho. Ya kwanza, ni maonyesho ya “Sarafu za Biblia Katika Karne ya Kwanza” iliyo na sarafu za awali zilizochimbuliwa kutia ndani, tetradrakma ambayo si rahisi kupatikana. Sehemu ya pili, “Wana Wako Wote Watafundishwa na Yehova” ni maonyesho yatakayowasaidia wageni kujua kuhusu shule mbalimbali zinazotayarishwa na tengenezo ili wajue manufaa ya kufundishwa na Yehova. Sehemu ya tatu ni “Kutetea na Kuthibitisha Kisheria Habari Njema” inayoelezea kuhusu mifano ya ndugu na dada katika nchi mbalimbali ambao waliteswa na inaonyesha jinsi tengenezo la Yehova lilivyoshikamana nao.

Kushoto hadi kulia: Maonyesho ya “Kijiji cha Biblia Katika Karne ya Kwanza,” Maonyesho ya “Wana Wako Wote Watafundishwa na Yehova,” na maonyesho ya “Kutetea na Kuthibitisha Kisheria Habari Njema”

Ndugu na dada ulimwenguni pote wanaalikwa kuja kutembelea Kituo cha Wageni cha Patterson ili kujionea wenyewe zawadi hii ya kiroho inayowangojea. Ni njia nyingine ambayo Yehova huonyesha kwamba anawapenda sana watu wake na anawathamini.​—Yakobo 1:17.