Hamia kwenye habari

APRILI 1, 2019
URUSI

Shahidi Mwingine wa Yehova Ahukumiwa Nchini Urusi

Shahidi Mwingine wa Yehova Ahukumiwa Nchini Urusi

Aprili 1, 2019, mahakama ileile iliyomhukumu Ndugu Dennis Christensen kifungo cha miaka sita, imemhukumu Sergey Skrynnikov mwenye umri wa miaka 56 kwa kutenda kupatana na imani yake akiwa Shahidi wa Yehova. Mahakama imemtoza faini kubwa ya dola 5,348.00 (RUB 350,000; EUR 4,758.95). Hakufungwa gerezani ingawa mwendesha-mashtaka alitaka apewe kifungo cha miaka mitatu gerezani.

Ndugu Skrynnikov na mke wake, Nina, wana binti mmoja. Wanamsaidia binti yao aliyeolewa na ana watoto watano. Pia, ndugu na dada Skrynnikov ndio wanaowatunza wazazi wa Nina waliozeeka.

Akiwa mahakamani, Ndugu Skrynnikov aliitetea imani yake kwa heshima. Kwa sehemu, alisema hivi: “Ukiangalia hali iliyopo sasa kwa maoni ya mtu asiye mwamini, unaweza kukata tamaa. . . . Lakini nikiwa Shahidi wa Yehova, ninaangalia hali hii kwa macho ya imani. Mungu akiniruhusu nihukumiwe, inamaanisha ninapaswa kuangalia miaka hii mitatu si kama adhabu bali kama mgawo wa pekee wa kutumikia katika eneo jipya! Hivyo, sikati tamaa. . . . Mungu ni yuleyule iwe tuko huru au gerezani. Hivyo, hatujaachwa. Yupo nasi kila mahali mradi tu tuwe waaminifu kwake.”

Tunatiwa moyo na imani yenye nguvu ya waabudu wenzetu, kama vile Ndugu Skrynnikov. Tunapofikiria majaribu makali wanayokabili, tunahisi kama mtume Paulo aliyesema maneno haya: “Mungu anayetoa tumaini na awajaze ninyi shangwe yote na amani kwa kumtegemea, ili tumaini lenu liongezeke kwa nguvu za roho takatifu.”—Waroma 15:13.