Hamia kwenye habari

Ndugu Taurai Mazarura akionyesha kitabu cha Mathayo kwenye tablet katika Lugha ya Ishara ya Zimbabwe wakati wa programu iliyorekodiwa mapema

JANUARI 26, 2021
ZIMBABWE

Mashahidi wa Yehova Watoa Kitabu cha Mathayo Katika Lugha ya Ishara ya Zimbabwe

Mashahidi wa Yehova Watoa Kitabu cha Mathayo Katika Lugha ya Ishara ya Zimbabwe

Januari 24, 2021, Biblia—Injili ya Mathayo ilitolewa katika Lugha ya Ishara ya Zimbabwe (ZSL). Ndugu Taurai Mazarura, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Zimbabwe, alitoa Biblia hiyo kupitia programu iliyorekodiwa mapema.

Wahubiri 401 wanaotumikia katika makutaniko ya Lugha ya Ishara ya Zimbabwe, walifurahi sana kupokea toleo hilo la karibuni. Wanatazamia kwa hamu kutumia kitabu cha Mathayo wanapofanya funzo la kibinafsi na katika huduma.

Kikundi cha watafsiri wa Lugha ya Ishara ya Zimbabwe wakirekodi

Ugonjwa wa virusi vya corona unaoendelea ulitokeza changamoto zaidi kwa kikundi cha watafsiri wa lugha hiyo. Kwa kawaida, watafsiri hushirikiana kwa ukaribu na watu wanaozungumza lugha yao ili kufahamu na kutumia ishara zinazotumiwa kwa ukawaida wanapotafsiri. Hata hivyo, vizuizi vilivyowekwa kwa sababu ya COVID-19, vimefanya iwe vigumu kuwatembelea viziwi katika maeneo mbalimbali. Watafsiri walifaulu kukabiliana na changamoto hiyo kwa kuwasiliana kwa ukawaida na viziwi kupitia video mtandaoni. Kufanya hivyo kuliwasaidia watafsiri kutokeza tafsiri inayoeleweka kwa urahisi na idadi kubwa ya viziwi nchini Zimbabwe.

Ndugu John Hunguka, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Zimbabwe alisema hivi: “Kutoa kitabu cha Mathayo katika ZSL ni mwanzo wa mradi wa Mashahidi wa Yehova wa kutafsiri Biblia nzima katika lugha hiyo. Mradi huu unatarajiwa kukamilika baada ya miaka kumi hivi.”

Mradi huu unaonyesha upendo wa Yehova kwa watu wote. Tunathamini sana baraka zake, tunapojitahidi kuhubiri “habari njema ya milele . . . kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.”—Ufunuo 14:6, maelezo ya chini.