Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Kwa Nini Kusoma Ni Muhimu kwa Watoto—​Sehemu 1: Kusoma au Kutazama?

Kwa Nini Kusoma Ni Muhimu kwa Watoto—​Sehemu 1: Kusoma au Kutazama?

 Watoto wako wanapopumzika, je, wanapendelea kutazama video au kusoma? Wangechagua nini: simu ya mkononi au kitabu?

 Kwa miaka mingi, televisheni na mambo ambayo watu wanaweza kutazama na kufanya mtandaoni yamewakengeusha wasisome. Jane Healy katika kitabu chake cha mwaka wa 1990, Endangered Minds, aliandika hivi: “Kadiri muda unavyopita huenda watu wakaacha kusoma.”

 Wakati huo, ungefikiria kwamba watu hawawezi kuacha kusoma kamwe. Sasa, miaka 30 baadaye, wakufunzi fulani katika nchi ambazo teknolojia inatumika sana wanasema kwamba, kwa wastani vijana wengi hawawezi kusoma vizuri kama ilivyokuwa hapo zamani.

Katika makala hii

 Kwa nini kusoma ni muhimu kwa watoto?

  •   Unaposoma unatumia uwezo wako wa kuwazia. Kwa mfano, unaposoma hadithi, sauti za wahusika katika hadithi hiyo zinasikikaje? Wahusika wanaonekanaje? Mazingira yakoje? Mwandishi hueleza mambo fulani lakini lazima msomaji awazie mambo mengine.

     Mama mmoja anayeitwa Laura, alisema hivi: “Tunapotazama sinema au video, tunaona jinsi mtu mwingine anavyoiwazia hadithi hiyo. Sinema na video zinaweza kuwa zenye kupendeza sana lakini kuna jambo fulani la kipekee kuhusu kusoma—unawazia mambo ambayo yameandikwa na mtu mwingine.”

  •   Kusoma kunawasaidia watoto wakuze sifa nzuri. Kadiri watoto wanavyosoma, wanakuza uwezo wao wa kuchanganua mambo na kutatua matatizo. Pia, watoto wanaposoma ni lazima wakazie fikira. Wanapofanya hivyo wanakuza sifa kama vile subira, kujidhibiti na hisia-mwenzi.

     Hisia-mwenzi? Ndiyo! Watafiti fulani wanaamini kuwa watoto wanaposoma polepole kwa uangalifu, hilo linawasaidia kufikiria kuhusu hisia za watu wanaosoma kuwahusu. Hilo linaweza kuwasaidia watoto kuonyesha hisia-mwenzi kwa wale wanaowajua.

  •   Kusoma huchochea kufikiri kwa undani. Watu wanaosoma kwa makini husoma kwa mwendo wao taratibu—hata wanarudia-rudia sehemu fulani ikilazimu—ili kuelewa kile ambacho mwandishi anasema. Wanapofanya hivyo, wanaweza kukumbuka zaidi wanayosoma na kufaidika kutokana nayo.—1 Timotheo 4:15.

     Baba mmoja anayeitwa Joseph anasema hivi: “Unaposoma, unaweza kufikiria kuhusu maana ya maneno fulani, uyahusianishe na yale unayoyajua, na ufikirie kuhusu masomo unayoweza kupata kutokana na maneno hayo. Video na sinema hazitutii moyo kufikiria kwa undani kuhusu mambo.”

 Jambo kuu: Ingawa video na mambo mengine yanayotazamwa mitandaoni yana nafasi yake, watoto wako wanaweza kukosa jambo muhimu ikiwa hawatafuti wakati wa kusoma.

 Jinsi ya kuwatia moyo wasome

  •   Anza mapema. Chloe, mama mwenye wavulana wawili anasema hivi: “Tuliwasomea watoto wetu tangu walipokuwa tumboni, na tukaendelea kufanya hivyo walipozaliwa. Tunafurahi kwamba hatukuacha. Kadiri muda ulivyopita, kusoma—hata kwa kujifurahisha tu—kukawa sehemu ya maisha yao.”

     Kanuni ya Biblia: “Tangu utoto mchanga umeyajua maandishi matakatifu.”—2 Timotheo 3:15.

  •   Tengeneza mazingira mazuri ya kusoma. Mwandalie mtoto wako vitabu nyumbani ili iwe rahisi kwake kusoma. Tamara, mama mwenye watoto wanne anapendekeza hivi: “Tafuta vitabu ambavyo mtoto wako atafurahia kusoma na uviweke kando ya kitanda chake.”

     Kanuni ya Biblia: “Mzoeze mtoto njia anayopaswa kuifuata; hata atakapozeeka hataiacha.”—Methali 22:6, maelezo ya chini.

  •   Dhibiti matumizi ya mtandao wa Intaneti. Baba mmoja anayeitwa Daniel anapendekeza kuwa na jioni moja ambapo watu wote nyumbani hawatumii vifaa vya kielektroni. Anasema hivi: “Hata ikiwa tungefanya hivyo mara moja tu kwa wiki, tulikuwa na jioni tulivu ambayo hatukutazama televisheni. Tulitumia muda huo kusoma tukiwa pamoja au kila mtu akiwa peke yake.”

     Kanuni ya Biblia: “Mhakikishe mambo muhimu zaidi.”—Wafilipi 1:10.

  •   Weka mfano mzuri. Karina, mama mwenye mabinti wawili anapendekeza hivi: “Fanya hadithi zipendeze kwa njia unayowasomea watoto wako na pia kupitia shauku yako kuelekea yale unayoyasoma. Ikiwa unapenda kusoma, huenda watoto wako pia watapenda kusoma.”

     Kanuni ya Biblia: “Endelea kujitahidi kusoma mbele ya watu.”—1 Timotheo 4:13.

 Si watoto wote watakaopenda kusoma. Hata hivyo, ukiendelea kuwatia moyo kusoma huenda ukawachochea. David, baba mwenye mabinti wawili alifanya mengi zaidi. Anasema hivi: “Nilisoma vitabu ambavyo binti zangu walikuwa wakisoma, hilo lilinisaidia kujua mambo yaliyowapendeza na tukawa na mengi ya kuzungumzia. Tulianzisha kikundi chetu kidogo cha kusoma. Tulifurahia sana!”