Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kuchoma Maiti?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kuchoma Maiti?

Jibu la Biblia

 Biblia haitoi mwongozo wowote hususa kuhusu desturi ya kuchoma maiti. Hakuna amri yoyote katika Biblia kuhusu kuzika au kuchoma maiti.

 Biblia inaripoti pindi ambazo watumishi waaminifu wa Mungu walizika maiti za wapendwa wao. Kwa mfano, Abrahamu alifanya jitihada kubwa ili kupata sehemu ya kumzika mke wake, Sara.​—Mwanzo 23:​2-​20; 49:29-​32.

 Pia, Biblia inataja watu fulani waaminifu ambao walichoma maiti. Kwa mfano, Mfalme Sauli wa Israeli na wana wake watatu walipouawa vitani, mwanzoni maiti zao zilibaki katika eneo la maadui na zilitendewa kwa njia isiyo ya heshima. Mashujaa waaminifu wa Israeli waliposikia kuhusu hilo, walienda kuichukua miili ya Sauli na wana wake, wakaiteketeza na kuzika mabaki yake. (1 Samweli 31:​8-​13) Biblia inaonyesha kwamba hiyo ilikuwa njia inayokubalika ya kushughulikia maiti za wanaume hao.​—2 Samweli 2:​4-6.

Maoni yasiyo sahihi kuhusu kuchoma maiti

 Maoni yasiyo sahihi: Kuchoma maiti hushushia heshima mwili.

 Ukweli: Biblia inasema kwamba wale wanaokufa hurudi mavumbini, na hilo ndilo jambo la asili ambalo hupata maiti inapooza. (Mwanzo 3:​19) Kuchoma maiti huharakisha jambo hilo kwa kufanya mwili uwe majivu, au vumbi.

 Maoni yasiyo sahihi: Katika nyakati za Biblia, maiti za watu ambao hawakuwa na kibali cha Mungu ndizo zilizochomwa baada ya wao kufa.

 Ukweli: Maiti za watu fulani ambao hawakuwa waaminifu, kama vile Akani na familia yake, zilichomwa. (Yoshua 7:​25) Lakini haikuwa kawaida kufanya hivyo. (Kumbukumbu la Torati 21:22, 23) Kama ilivyotajwa mapema, maiti za watu fulani waaminifu, kama vile Yonathani, mwana wa Mfalme Sauli, zilichomwa walipokufa.

 Maoni yasiyo sahihi: Kuchoma maiti kunamzuia Mungu kumfufua mtu.

 Ukweli: Kuhusu ufufuo wa wafu, si jambo kubwa kwa Mungu ikiwa mwili wa mtu ulizikwa, ulichomwa, ulipotea baharini, au uliliwa na wanyama wa mwituni. (Ufunuo 20:13) Mweza-Yote anaweza kumuumbia mtu huyo mwili mpya kwa urahisi.​—1 Wakorintho 15:35, 38.