Hamia kwenye habari

Je, Ibilisi anaweza Kuongoza Wanadamu?

Je, Ibilisi anaweza Kuongoza Wanadamu?

Jibu la Biblia

 Ibilisi na roho waovu wamekuwa na uvutano mkubwa kuelekea wanadamu hivi kwamba Biblia inasema hivi kuwahusu: “Yule Mwovu anauongoza ulimwengu mzima.” (1 Yohana 5:​19, New Century Version) Biblia inaonyesha njia anazotumia Ibilisi kushawishi watu.

  •   Uwongo. Biblia inawatia moyo Wakristo “kupigana dhidi ya mbinu zenye uovu za Ibilisi.” (Waefeso 6:​11, NCV) Mbinu moja anayotumia ni kudanganya watu waamini kwamba wawakilishi wake ni wahudumu wa Mungu.​—2 Wakorintho 11:13-​15.

  •   Kuwasiliana na Pepo. Ibilisi anawaongoza vibaya watu kupitia watu wanaowasiliana na pepo, wanaotafuta ishara za bahati, na wale wanaofanya uaguzi au unajimu. (Kumbukumbu la Torati 18:10-​12) Matumizi mabaya ya dawa za kulevya, kupumbaza akili, na mbinu fulani za kutafakari zinazotia ndani kuacha akili ikiwa bila wazo lolote, mambo yanayoweza kufanya iwe rahisi kwa mtu kuongozwa na roho waovu.​—Luka 11:24-​26.

  •   Dini ya uwongo. Dini zinazofundisha uwongo huwafanya watu wasimtii Mungu. (1 Wakorintho10:20) Biblia inaita mafundisho hayo ya uwongo kuwa “mafundisho ya roho waovu.”​—1 Timotheo 4:1.

  •   Kuongozwa na roho waovu. Biblia inataja kuhusu roho waovu walioongoza watu. Watu wenye roho waovu walipigwa upofu, kuwa bubu au kujiumiza wenyewe.​—Mathayo 12:22; Marko 5:​2-5.

Jinsi ya kujiepusha na uvutano wa Ibilisi

  Huna sababu ya kuhofu sana kwamba utaongozwa na roho waovu kwa kuwa Biblia inaonyesha jinsi unavyoweza kumpinga Ibilisi:

  •   Jifunze kutambua njia anazotumia Ibilisi ili ‘usikose kuzijua mbinu zake.’​—2 Wakorintho 2:​11.

  •   Jifunze Biblia na utumie ujuzi huo. Kutumia kanuni za Biblia kutakulinda na uvutano wa Ibilisi.​—Waefeso 6:​11-​18.

  •   Ondolea mbali kila kitu kinachohusiana na roho waovu. (Matendo 19:19) Vitu hivyo vinatia ndani muziki, vitabu, magazeti, kadi, na sinema zinazochochea kuwasiliana na pepo.