Hamia kwenye habari

Je, Wakristo Wanapaswa Kushika Sabato?

Je, Wakristo Wanapaswa Kushika Sabato?

Jibu la Biblia

 Si takwa kwa Wakristo kushika sabato ya kila juma. Wakristo wako chini ya “sheria ya Kristo,” ambayo haitii ndani kushika Sabato. (Wagalatia 6:2; Wakolosai 2:16, 17) Kwa nini tunasema hivyo kwa uhakika? Kwanza, fikiria chanzo cha Sabato.

Sabato ni nini?

 Neno “sabato” linatokana na neno la Kiebrania linalomaanisha “kupumzika; kukoma.” Neno hilo linaonekana kwa mara kwanza kwenye Biblia katika amri ambazo taifa la kale la Israeli lilipewa. (Kutoka 16:23) Kwa mfano, amri ya nne kati ya zile Amri Kumi inasema hivi: “Kwa kuikumbuka siku ya sabato ili kuiona kuwa takatifu, utafanya utumishi nawe uifanye kazi yako yote kwa siku sita. Lakini siku ya saba ni sabato kwa Yehova Mungu wako. Usifanye kazi yoyote.” (Kutoka 20:8-10) Siku ya Sabato ilianza Ijumaa jua lilipotua hadi Jumamosi baada ya jua kutua. Katika muda huo, Waisraeli hawangeweza kuondoka katika eneo lao, kuwasha moto, kukusanya kuni, au kubeba mzigo. (Kutoka 16:29; 35:3; Hesabu 15:32-36; Yeremia 17:21) Mtu aliyevunja Sabato alihukumiwa kifo.—Kutoka 31:15.

 Siku nyingine pia katika kalenda ya Kiyahudi ziliitwa sabato, kutia ndani mwaka wa 7 na wa 50. Katika miaka hiyo ya Sabato, nchi haikupaswa kulimwa na Waisraeli hawakupaswa kulazimishwa kulipa madeni.—Mambo ya Walawi 16:29-31; 23:6, 7, 32; 25:4, 11-14; Kumbukumbu la Torati 15:1-3.

Dhabihu ya Yesu ilibatilisha sheria ya Sabato

Kwa nini sheria kuhusu Sabato haiwahusu Wakristo?

 Sheria ya Sabato iliwahusu tu watu waliokuwa chini ya Sheria waliyopewa kupitia Musa. (Kumbukumbu la Torati 5:2, 3; Ezekieli 20:10-12) Mungu hakuamuru watu wengine washike sabato. Isitoshe, kwa msingi wa dhabihu ya Yesu Kristo, hata Wayahudi ‘walifunguliwa kutoka katika Sheria’ ya Musa, kutia ndani zile Amri Kumi. (Waroma 7:6, 7; 10:4; Wagalatia 3:24, 25; Waefeso 2:15) Badala ya kushika Sheria ya Musa, Wakristo wanafuata ile sheria kuu ya upendo.—Waroma 13:9, 10; Waebrania 8:13.

Maoni yasiyo sahihi kuhusu Sabato

 Maoni yasiyo sahihi: Mungu aliweka sheria ya Sabato alipopumzika siku ya saba.

 Ukweli: Biblia inasema hivi: “Mungu akaibariki siku ya saba na kuifanya takatifu, kwa kuwa katika siku hiyo amekuwa akipumzika kutokana na kazi yake yote ya kuumba ambayo Mungu alikusudia kuifanya.” (Mwanzo 2:3) Mstari huo haukuwawekea wanadamu sheria, bali ulieleza kile ambacho Mungu alifanya wakati wa siku ya saba ya uumbaji. Kabla ya siku za Musa, Biblia haimtaji mtu yeyote ambaye alishika sabato.

 Maoni yasiyo sahihi: Waisraeli walikuwa chini ya sheria ya Sabato kabla ya kupokea Sheria ya Musa.

 Ukweli: Musa aliwaambia Waisraeli hivi: “Yehova Mungu wetu alifanya agano pamoja nasi katika Horebu,” eneo linalozunguka Mlima Sinai. Agano hilo lilitia ndani sheria ya Sabato. (Kumbukumbu la Torati 5:2, 12) Mambo ambayo Waisraeli walipitia yanaonyesha kwamba Sabato ilikuwa jambo jipya kwao. Mungu alisema kwamba Sabato ingewakumbusha kuhusu kukombolewa kwao kutoka Misri. Hilo lingewezekanaje ikiwa Waisraeli tayari walikuwa chini ya sheria ya Sabato walipokuwa kule Misri? (Kumbukumbu la Torati 5:15) Kwa nini walihitaji kuambiwa wasiokote mana siku ya saba? (Kutoka 16:25-30) Na kwa nini hawakujua jinsi ya kushughulikia kesi ya mtu wa kwanza aliyevunja Sabato?—Hesabu 15:32-36.

 Maoni yasiyo sahihi: Sabato ni agano la kuendelea kwa hiyo bado ni takwa kuishika.

 Ukweli: Ni kweli kwamba tafsiri fulani za Biblia zinasema kuwa Sabato ni “agano la kuendelea.” (Kutoka 31:16, King James Version) Hata hivyo, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “kuendelea” linaweza pia kumaanisha “kudumu mpaka wakati ujao usio na kipimo.” Si lazima limaanishe milele. Kwa mfano, Biblia inatumia neno hilohilo kueleza kuhusu ukuhani wa Waisraeli, ambao Mungu aliukomesha miaka 2,000 hivi iliyopita.—Kutoka 40:15; Waebrania 7:11, 12.

 Maoni yasiyo sahihi: Lazima Wakristo washike Sabato kwa kuwa Yesu aliishika.

 Ukweli: Yesu alishika Sabato kwa sababu alikuwa Myahudi, kwa hiyo tangu alipozaliwa alipaswa kuitii Sheria ya Musa. (Wagalatia 4:4) Baada ya Yesu kufa, agano hilo la Sheria—kutia ndani Sabato—liliondolewa.—Wakolosai 2:13, 14.

 Maoni yasiyo sahihi: Mtume Paulo alishika Sabato alipokuwa Mkristo.

 Ukweli: Paulo aliingia katika masinagogi siku ya Sabato, lakini si ili ajiunge na Wayahudi katika kushika Sabato. (Matendo 13:14; 17:1-3; 18:4) Badala yake, alihubiri habari njema katika masinagogi akifuata desturi ya wakati huo, kwa kuwa wasemaji wanaozuru walikaribishwa kuwahutubia wale waliokuwa wamekusanyika kwa ajili ya ibada. (Matendo 13:15, 32) Paulo alihubiri “kila siku,” si siku ya Sabato tu.—Matendo 17:17.

 Maoni yasiyo sahihi: Sabato ya Wakristo ni Jumapili.

 Ukweli: Biblia haitoi amri yoyote kwamba Wakristo watenge Jumapili kuwa siku ya kupumzika na kuabudu. Kwa Wakristo wa mapema, Jumapili ilikuwa siku ya kazi kama tu siku nyingine. Kitabu The International Standard Bible Encyclopedia kinasema hivi: “Haikuwa hadi karne ya 4 kwamba Jumapili ikaanza kuonwa kama sabato, wakati ambapo Konstantino [maliki mpagani wa Roma] aliagiza kwamba aina fulani za kazi zisifanywe Jumapili.” a

 Hata hivyo, namna gani kuhusu masimulizi ambayo huenda yanaonyesha kwamba Jumapili ilikuwa siku ya pekee? Biblia inasema kwamba katika “siku ya kwanza ya juma,” ambayo ilikuwa ni Jumapili, mtume Paulo alikula mlo pamoja na waamini wenzake, lakini hilo halishangazi kwa kuwa Paulo alikuwa akiondoka siku iliyofuata. (Matendo 20:7) Vivyo hivyo, makutaniko fulani yaliambiwa yaweke kando kiasi fulani cha pesa kwa ajili ya kazi ya kutoa msaada, katika “siku ya kwanza ya juma,” yaani Jumapili, lakini hilo lilikuwa pendekezo tu la jinsi ya kupangia pesa za kibinafsi. Watu waliweka michango hiyo nyumbani, hawakuipeleka mahali walipokutania.—1 Wakorintho 16:1, 2.

 Maoni yasiyo sahihi: Ni kosa kutenga siku moja kila juma ili iwe ya kupumzika na kuabudu.

 Ukweli: Biblia inamwachia kila Mkristo uhuru wa kufanya uamuzi huo.—Waroma 14:5.

a Ona pia kitabu New Catholic Encyclopedia, Toleo la Pili, Buku la 13, ukurasa wa 608.