Hamia kwenye habari

Yule Tajiri na Lazaro Walikuwa Nani?

Yule Tajiri na Lazaro Walikuwa Nani?

Jibu la Biblia

 Yule tajiri na Lazaro walikuwa watu wa kubuniwa katika mojawapo ya hotuba za Yesu. (Luka 16:19-31) Katika hadithi hiyo, watu hao waliwakilisha vikundi viwili vya watu: (1) viongozi wa dini ya Kiyahudi wa siku za Yesu na (2) watu wanyoofu wa hali ya chini ambao waliitikia ujumbe wa Yesu.

Katika makala hii

 Yesu alisema nini kumhusu yule mwanamume tajiri na Lazaro?

 Katika Luka sura ya 16, Yesu alifafanua wanaume wawili ambao walipata mabadiliko makubwa katika hali yao.

 Huu ni muhtasari wa hadithi ambayo Yesu alisimulia: Yule mwanamume tajiri aliishi maisha yenye ufanisi. Mtu fulani aliyekuwa akiombaomba aliyeitwa Lazaro alikuwa akiletwa katika lango la mwanamume huyo tajiri; Lazaro alitamani kula mabaki yaliyoanguka kutoka kwenye meza ya yule tajiri. Baada ya muda, Lazaro alikufa, na malaika wakambeba na kumpeleka kando ya Abrahamu. Yule tajiri pia akafa na kuzikwa. Katika hadithi hiyo, wanaume wote wawili wanafafanuliwa wakiwa na fahamu baada ya kufa. Yule tajiri alisimuliwa kuwa anateseka katika moto mkali, naye akamwomba Abrahamu amtume Lazaro aupoze ulimi wake kwa tone la maji ambalo angepata kwa kuchovya ncha ya kidole chake katika maji. Abrahamu alikataa ombi la mwanamume huyo tajiri na kusema kwamba hali za wanaume wote wawili zilikuwa zimegeuka kabisa na kwamba kulikuwa na shimo kubwa kati yao ambalo halingeweza kuvukwa.

 Je, hadithi hii ilikuwa halisi?

 Hapana. Ulikuwa mfano ambao Yesu alisimulia ili kufundisha somo. Wasomi wengi wanaunga mkono kwa uhakika kwamba huo ulikuwa mfano. Kwa mfano, kichwa kidogo katika toleo la 1912 la Biblia ya Luther kinasema kwamba huo ni mfano. Na Biblia ya Wakatoliki, Jerusalem Bible, ina maelezo ya chini yanayosema huo ni “mfano uliosimuliwa kupitia hadithi lakini haurejelei watu wowote halisi katika historia.”

 Je, Yesu alikuwa akifundisha masomo kuhusu uhai baada ya kifo? Je, alimaanisha kwamba baadhi ya watu wanateseka katika moto wa mateso baada ya kufa na kwamba Abrahamu na Lazaro wako mbinguni? Mambo fulani ya hakika yanaonyesha sivyo.

 Kwa mfano:

  •   Ikiwa mwanamume huyo tajiri angekuwa katika sehemu halisi ambayo alikuwa akiteseka katika moto, je, moto huo usingekausha maji yaliyokuwa kwenye ncha ya kidole cha Lazaro?

  •   Hata ikiwa maji hayo yasingekaushwa, je, tone moja lingeweza kumletea mwanamume huyo tajiri kitulizo cha kutosha ikiwa alikuwa akiteseka katika moto halisi?

  •   Abrahamu angewezaje kuwa hai mbinguni, kwa kuwa Yesu alikuwa amesema waziwazi kwamba kuufikia wakati huo, hakuna aliyekuwa ameenda mbinguni?​—Yohana 3:13.

 Je, hadithi hii inaunga mkono fundisho la moto wa mateso?

 Hapana. Ingawa hii si hadithi halisi, wengine husema kwamba inaonyesha wazo la kwamba watu wema huenda mbinguni na watu wabaya huteswa katika moto wa mateso. a

 Je, wazo hilo linapatana na akili? Hapana.

 Fundisho la moto wa mateso halipatani na kile ambacho Biblia inasema kuhusu hali ya wafu. Kwa mfano, haisemi kwamba watu wote wema wanaokufa wanafurahia maisha mbinguni au kwamba watu wote wabaya wanateswa katika moto wa mateso. Badala yake, Biblia inasema hivi waziwazi: “Walio hai wanajua kwamba watakufa, lakini waliokufa hawajui jambo lolote kamwe.”​—Mhubiri 9:5.

 Ni nini maana ya hadithi kumhusu yule mwanamume tajiri na Lazaro?

 Hadithi hiyo inaonyesha kwamba hali za vikundi viwili vya watu zingebadilika sana baada ya muda mfupi.

 Ni wazi kwamba yule mwanamume tajiri aliwakilisha viongozi wa dini ya Kiyahudi, “waliopenda pesa.” (Luka 16:14) Walisikiliza Yesu akizungumza, lakini walipinga ujumbe wake. Viongozi hao wa kidini waliwadharau watu wa kawaida.​—Yohana 7:49.

 Lazaro aliwakilisha watu wa kawaida waliokubali ujumbe wa Yesu na ambao walidharauliwa na viongozi wa dini ya Kiyahudi.

 Badiliko katika hali lingekuwa kubwa kwa vikundi vyote viwili.

  •   Viongozi wa dini ya Kiyahudi walifikiri kwamba walikuwa na kibali cha Mungu. Lakini ni kana kwamba walikufa wakati ambapo Mungu aliwakataa pamoja na ibada yao kwa sababu hawakukubali ujumbe wa Yesu. Nao waliteswa na ujumbe ambao Yesu na wafuasi wake walihubiri.​—Mathayo 23:29, 30; Matendo 5:29-33.

  •   Watu wa kawaida​—ambao kwa muda mrefu walikuwa wamepuuzwa na viongozi wao wa kidini—​sasa walikuwa na kibali. Wengi wao walikubali ujumbe wa Maandiko ambao Yesu alifundisha na wakapata manufaa. Sasa walikuwa na nafasi ya kufurahia kibali cha Mungu milele.​—Yohana 17:3.

a Baadhi ya tafsiri za Biblia hutumia moto wa mateso (hell) kufafanua mahali ambapo yule mwanamume tajiri alikuwa baada ya kufa. Hata hivyo, neno la awali la Kigiriki (Hadesi) linalotumiwa kwenye Luka 16:23 linamaanisha kaburi la kawaida la mwanadamu.