Hamia kwenye habari

Yehova Ni Nani?

Yehova Ni Nani?

Jibu la Biblia

 Biblia inamtaja Yehova kuwa Mungu wa Kweli, Muumba wa kila kitu. (Ufunuo 4:​11) Manabii kama Abrahamu na Musa walimtumikia, kama alivyofanya Yesu. (Mwanzo 24:27; Kutoka 15:1, 2; Yohana 20:17) Yeye si Mungu wa watu fulani pekee, bali wa “dunia yote.”​—Zaburi 47:2.

 Kama inavyoonyeshwa katika Biblia, Yehova ni jina la pekee la Mungu. (Kutoka 3:​15; Zaburi 83:18) Linatokana na kitenzi cha Kiebrania kinachomaanisha “kuwa,” na wasomi wengi wanaona kwamba jina hilo linamaanisha “Husababisha Iwe.” Maana hii inapatana kabisa na cheo chake akiwa Muumba na Mtimizaji wa makusudi. (Isaya 55:10, 11) Biblia inatusaidia pia kuelewa utu wa Yehova, hasa sifa yake kuu ya upendo.—Kutoka 34:5-7; Luka 6:35; 1 Yohana 4:8.

 Jina Yehova limetafsiriwa kutoka kwa jina la Mungu katika lugha ya Kiebrania lenye herufi nne za Tetragramatoni יהוה (YHWH). Matamshi sahihi ya jina hilo yaliyotumiwa katika Kiebrania cha kale hayajulikani. Hata hivyo, jina “Yehova” limetumiwa kwa miaka mingi katika Kiswahili. Jina hilo lilionekana kwa mara ya kwanza katika Kiingereza kwenye tafsiri ya Biblia ya Tyndale ya 1530. a

Kwa nini matamshi sahihi ya jina la Mungu yaliyotumiwa katika Kiebrania cha kale hayajulikani?

 Kiebrania cha kale kiliandikwa kwa kutumia herufi bila irabu. Msomaji wa lugha ya Kiebrania angeweza kwa urahisi kutambua ni irabu gani zilizokusudiwa neno litamkwe. Hata hivyo, Maandiko ya Kiebrania (“Agano la kale”) yalipokamilika, baadhi ya Wayahudi walikuwa na imani potovu kwamba ni kosa kutaja jina la Mungu. Waliposoma Maandiko yaliyokuwa na jina la Mungu walilibadilisha kwa majina kama vile “Bwana” au “Mungu.” Kadiri wakati ulivyopita, imani hii ilienea na matamshi ya awali ya jina hilo yakapotea kabisa. b

 Watu fulani hufikiri kwamba jina hilo takatifu lilitamkwa “Yahweh,” na wengine husema mambo mbalimbali. Kitabu cha Kukunjwa cha Bahari ya Chumvi kilicho na sehemu ya kitabu cha Walawi katika lugha ya Kigiriki, kimetafsiri jina hilo Iao. Waandishi wa zamani wa Kigiriki wametumia matamshi kama Iae, I·a·beʹ, na I·a·ou·eʹ, lakini hakuna uthibitisho wowote kwamba matamshi hayo yalitumiwa katika Kiebrania cha kale. c

Mawazo yasiyo ya kweli kuhusu jina la Mungu katika Biblia

 Uwongo: Tafsiri zinazotumia jina “Yehova” zimeongeza jina hilo.

 Kweli: Herufi za Kiebrania za jina la Mungu zilizoandikwa katika Tetragramatoni zinapatikana karibu mara 7,000 katika Biblia. d Tafsiri nyingi za Biblia zimeondoa jina la Mungu na kulibadili na majina ya cheo kama vile “Bwana.”

 Uwongo: Mungu Mweza-Yote hahitaji jina la kibinafsi.

 Kweli: Mungu mwenyewe aliwaongoza waandikaji wa Biblia kutumia jina lake mara elfu kadhaa na aliwaamuru wale wanaomtumikia walitumie. (Isaya 42:8; Yoeli 2:​32; Malaki 3:​16; Waroma 10:13) Mungu hata aliwahukumu manabii wa uwongo waliojaribu kuwafanya watu wasahau jina lake.​—Yeremia 23:27.

 Uwongo: Kulingana na utamaduni wa Kiyahudi, jina la Mungu linapaswa kuondolewa katika Biblia.

 Kweli: Ni kweli kwamba baadhi ya waandishi wa Kiyahudi walikataa kutamka jina takatifu la Mungu. Hata hivyo, hawakuliondoa katika Biblia zao. Mungu hapendi tufuate utamaduni wowote ulio kinyume cha mapenzi yake.​—Mathayo 15:​1-3.

 Uwongo: Jina takatifu la Mungu halipaswi kuwepo katika Biblia kwa sababu hatujui matamshi sahihi ya jina hilo katika Kiebrania.

 Kweli: Kufikiri hivyo ni kana kwamba mtu anasema Mungu anatarajia watu wanaozungumza lugha tofauti watamke jina lake kwa njia moja. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba tangu zamani waabudu wa Mungu waliozungumza lugha tofauti walitamka majina kwa njia tofauti-tofauti.

 Kwa mfano, mfikirie mwamuzi wa Israeli aliyeitwa Yoshua. Wakristo walioishi katika karne ya kwanza wangetamka jina lake Yehoh·shuʹaʽ, na wale waliozumgumza Kigiriki wangemwita I·e·sousʹ. Biblia inatumia jina la Kigiriki Yoshua ambalo limetafsiriwa kutoka kwa lugha ya Kiebrania, jambo hilo linaonyesha kwamba Wakristo walitumia majina kwa njia iliyozoeleka katika lugha zao.​—Matendo 7:​45; Waebrania 4:8.

 Njia hiyo inaweza kutumiwa katika kutafsiri jina la Mungu. Mbali na kujali matamshi sahihi ya jina hilo, jambo muhimu ni kwamba jina la Mungu linawekwa mahali panapofaa katika Biblia.

a Tyndale alitumia jina “Iehouah” alipotafsiri vitabu vitano vya kwanza vya Biblia. Kadiri wakati ulivyopita, lugha ya Kiingereza ilibadilika na matamshi ya jina hilo takatifu yaliboreshwa. Kwa mfano, katika mwaka wa 1612, Henry Ainsworth alitumia jina “Iehovah” katika tafsiri yake nzima ya kitabu cha Zaburi. Alipoboresha tafsiri hiyo katika mwaka wa 1639, alitumia jina “Jehovah.” Pia, watafsiri wa Biblia ya American Standard Version iliyochapishwa mwaka 1901, walitumia jina “Jehovah” mahali ambapo jina hilo takatifu lilitumiwa katika Maandiko ya Kiebrania.

b Kitabu New Catholic Encyclopedia, Toleo la Pili, Buku la 14, ukurasa wa 883-​884, kinasema: “Kipindi kifupi baada ya Wayahudi kutoka uhamishoni, jina Yahweh lilianza kuonwa kwa njia ya pekee, na mazoea yakaanza ya kulibadili kwa majina kama vile ADONAI au ELOHIM.”

c Ili kupata habari zaidi, ona Sehemu ya 1 yenye kichwa “Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kiebrania,” katika kijitabu Mwongozo wa Kujifunza Neno la Mungu.

d Ona kitabu Theological Lexicon of the Old Testament, Buku la 2, ukurasa wa 523-​524.