Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuboresha Uhusiano wa Familia na Marafiki

Kuboresha Uhusiano wa Familia na Marafiki

Ni vigumu kwa watu wengi kudumisha uhusiano mzuri na wengine. Fikiria kanuni kadhaa za Biblia zinazoweza kukusaidia kuboresha uhusiano wako na wengine.

USIWE MBINAFSI

KANUNI YA BIBLIA: ‘Angalia, si faida zako mwenyewe, bali pia faida za wengine.’—Wafilipi 2:4.

INAMAANISHA NINI: Tutakuwa na uhusiano mzuri na wengine tukikazia fikira mambo tunayoweza kuwafanyia badala ya mambo tunayotaka watufanyie. Ikiwa utakuwa mbinafsi, utaharibu uhusiano wako na wengine. Kwa mfano, mwenzi wa ndoa ambaye ni mbinafsi anaweza kumsaliti mwenzi wake. Isitoshe, hakuna mtu anayependa kufanya urafiki na mtu ambaye sikuzote anajivuna kwa sababu ya vitu anavyomiliki au mambo anayojua. Hivyo, kama kitabu The Road to Character kinavyosema, “watu wabinafsi na ambao hawawafikirii watu wengine huwa na matatizo mengi.”

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA:

  • Wasaidie wengine. Marafiki wazuri wanaaminiana na wako tayari kusaidiana. Watafiti fulani wanasema kwamba watu wanaowasaidia wengine hujiheshimu na kupunguza uwezekano wa kupata ugonjwa wa kushuka moyo.

  • Onyesha hisia mwenzi. Kuonyesha hisia mwenzi kunamaanisha kuhisi maumivu ya mtu mwingine moyoni mwako. Ukiwa na hisia mwenzi utaepuka kutumia maneno ya kejeli, yaani, maneno makali yanayoonekana kama utani lakini yanayokusudiwa kuumiza hisia za mtu mwingine.

    Ukiwa na hisia mwenzi, utawavumilia wengine. Hivyo, hisia mwenzi inaweza kukusaidia kuepuka ubaguzi na pia itakuwezesha kuwa na marafiki wa tamaduni au malezi mbalimbali.

  • Tumia muda pamoja na wengine. Utawafahamu vizuri zaidi watu wengine ukitumia muda mwingi pamoja nao. Ikiwa unataka kupata marafiki wazuri, uwe na zoea la kuwa na mazungumzo ya kina na yenye kujenga pamoja na watu. Uwe msikilizaji mzuri. Pendezwa na mambo wanayofikiria. Utafiti wa hivi karibuni unaonyesha kwamba “mazungumzo ya kina yanaweza kufanya watu wawe na furaha.”

CHAGUA MARAFIKI KWA HEKIMA

KANUNI YA BIBLIA: “Kushirikiana na watu wabaya hupotosha maadili.”​—1 Wakorintho 15:33, maelezo ya chini.

INAMAANISHA NINI: Watu unaoshirikiana nao wana uvutano mkubwa kwako, iwe ni uvutano mzuri au mbaya. Wataalamu wa elimu ya jamii wanakubali kwamba marafiki wanaweza kuathiri maisha yako. Kwa mfano, wanasema kwamba ukishirikiana na watu wanaovuta sigara au waliotalikiwa, unaweza kuanza kuvuta sigara au kutamani kupata talaka.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA: Fanya urafiki na watu ambao wana sifa na viwango unavyoheshimu au unavyotamani kuiga. Kwa mfano, shirikiana na watu wenye busara, wenye heshima, wakarimu, na wakaribishaji wageni.

KANUNI NYINGINE ZA BIBLIA

Tazama video zinazotegemea Biblia ambazo zimekusudiwa kuwasaidia wenzi wa ndoa, vijana, na watoto kuboresha maisha ya familia

EPUKA MANENO YANAYOUMIZA.

“Maneno yanayosemwa bila kufikiri huchoma kama upanga.”​—METHALI 12:18.

UWE MKARIMU.

“Mtu mkarimu atapata ufanisi.”​—METHALI 11:25.

WATENDEE WENGINE KAMA UNAVYOTAKA KUTENDEWA.

“Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima ninyi pia mwatendee vivyo hivyo.”​—MATHAYO 7:12.