Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waisraeli wa Kale Walipigana Vita—Kwa Nini Sisi Hatupigani?

Waisraeli wa Kale Walipigana Vita—Kwa Nini Sisi Hatupigani?

“IKIWA yeyote kati yenu atakataa kupigana dhidi ya Ufaransa au Uingereza, nyote lazima mfe!” Hivyo ndivyo afisa mmoja wa nazi alivyofokea kikundi cha Mashahidi wa Yehova wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Hata ingawa wanajeshi wa SS waliokuwa na silaha kamili walikuwa hapo karibu, hakuna hata mmoja wa ndugu zetu aliyekubali. Huo ulikuwa ujasiri wa kweli! Msimamo wao unaonyesha vizuri maoni yetu tukiwa Mashahidi wa Yehova. Tunakataa kupigana vita katika ulimwengu huu. Hata tunapotishwa kuuawa, tunakataa kuunga mkono mizozo ya ulimwengu huu.

Hata hivyo, si wote wanaodai kuwa Wakristo wanakubali msimamo huo. Wengi wanaamini kwamba Mkristo anaweza na anapaswa kupigania nchi yake. Huenda wakasema hivi: ‘Waisraeli wa kale walikuwa watu wa Mungu na walipigana vita; kwa nini Wakristo wasipigane leo?” Ungejibuje? Huenda ukawafafanulia kwamba hali ya Waisraeli wa kale ilikuwa tofauti kabisa na hali ya watu wa Mungu leo. Fikiria tofauti tano.

1. WATU WOTE WA MUNGU WALIKUWA KATIKA TAIFA MOJA

Zamani, Yehova aliwakusanya watu wake katika taifa moja, yaani, Israeli. Aliwaita Waisraeli ‘mali yake ya pekee kati ya mataifa yote.’ (Kut. 19:5) Pia, Mungu aliwapa nchi hususa. Basi Mungu alipowaamuru Waisraeli waende vitani dhidi ya mataifa mengine, hawakuwa wakipigana au kuwaua waabudu wenzao. *

Leo, waabudu wa kweli wametoka katika “mataifa yote na makabila na jamii na lugha.” (Ufu. 7:9) Ikiwa watu wa Mungu wangeshiriki katika vita, wangepigana dhidi ya waabudu wenzao na hata kuwaua.

2. YEHOVA ALIWAAMURU WAISRAELI WAENDE VITANI

Zamani, Yehova aliamua wakati na sababu ambazo ziliwafanya Waisraeli waende vitani. Kwa mfano, Mungu aliwaagiza Waisraeli watekeleze hukumu yake dhidi ya Wakanaani, ambao walijulikana kwa kushiriki katika ibada ya roho waovu, kufanya uasherati kwa kiwango kikubwa sana, na kuwatoa watoto dhabihu. Yehova aliwaamuru Waisraeli waondoe mambo hayo maovu katika nchi ambayo alikuwa ameahidi kuwapa. (Law. 18:24, 25) Baada ya Waisraeli kuimiliki Nchi ya Ahadi, nyakati nyingine Mungu aliwaagiza waende vitani ili kulinda taifa la Israeli dhidi ya maadui waliowakandamiza. (2 Sam. 5:17-25) Hata hivyo, hakuna wakati wowote ambapo Yehova aliwaruhusu Waisraeli wajiamulie wenyewe wakati wa kwenda vitani. Ikiwa wangeenda, mara nyingi walipatwa na matokeo mabaya sana.​—Hes. 14:41-45; 2 Nya. 35:20-24.

Leo, Yehova hawaamuru wanadamu waende vitani. Mataifa hupigana ili kuendeleza masilahi ya wanadamu, bali si masilahi ya Mungu. Huenda wakaenda vitani ili kulinda eneo la nchi yao au kwa sababu za kiuchumi, kisiasa, au itikadi fulani. Lakini namna gani wale ambao wanadai kwamba wanapigana katika jina la Mungu ili kulinda ibada yao au kuwaua maadui wa Mungu? Yehova atawalinda waabudu wake wa kweli na kuwaangamiza maadui wake katika vita vya wakati ujao, yaani, vita vya Har–Magedoni. (Ufu. 16:14, 16) Katika vita hivyo, jeshi la Mungu litafanyizwa na majeshi yake ya mbinguni, si waabudu wake wa kibinadamu.​—Ufu. 19:11-15.

3. WAISRAELI HAWAKUUA WALE WALIOONYESHA IMANI

Je, leo Yehova analipigania taifa lolote kama alivyowapigania Waisraeli huko Yeriko?

Zamani, jeshi la Waisraeli mara nyingi liliwaonyesha rehema wale walioonyesha imani katika Mungu na kuwauwa tu wale ambao Yehova alikuwa amewahukumu kwamba wanastahili kuangamizwa. Fikiria mifano miwili. Ingawa Yehova aliagiza jiji la Yeriko liangamizwe, Waisraeli hawakumuua Rahabu na familia yake kwa sababu alionyesha imani. (Yos. 2:9-16; 6:16, 17) Baadaye, hawakuliangamiza jiji la Gibeoni kwa sababu Wagibeoni walionyesha kwamba wanamwogopa Mungu.​—Yos. 9:3-9, 17-19.

Leo, mataifa yanayopigana huwaua hata wale wanaonyesha imani. Na nyakati nyingine, raia wasio na hatia huuawa mataifa yanapopigana.

4. WAISRAELI WALIPASWA KUFUATA SHERIA ZA MUNGU KUHUSU VITA

Zamani, Yehova aliwaagiza wanajeshi Waisraeli wapigane vita kulingana na mwongozo wake. Kwa mfano, nyakati nyingine aliwaambia watangaze “masharti ya amani” kwa majiji yaliyowapinga. (Kum. 20:10) Pia, Yehova alitarajia kwamba wanajeshi Waisraeli wadumishe usafi wa kimwili na kimaadili, wao wenyewe na katika kambi zao. (Kum. 23:9-14) Ingawa mara nyingi majeshi ya mataifa jirani yaliwabaka wanawake katika maeneo waliyoteka, Yehova aliwaagiza Waisraeli wasifanye hivyo. Hata hawakuruhusiwa kumwoa mwanamke aliyetekwa mpaka baada ya mwezi mmoja kupita tangu jiji lilipotekwa.​—Kum. 21:10-13.

Leo, nchi nyingi zimetia saini makubaliano ya kimataifa ambayo yanaongoza jinsi vita vinavyopiganwa. Ingawa sheria hizo zinakusudiwa kuwalinda raia, inasikitisha kwamba mara nyingi zinavunjwa.

5. MUNGU ALIPIGANA KWA AJILI YA TAIFA LAKE

Katika vita vya siku hizi, je, wanajeshi wanaepuka kuwaua watu waaminifu kama vile Rahabu na familia yake walivyookolewa katika vita vya Yehova dhidi ya Yeriko?

Zamani, Yehova aliwapigania Waisraeli, na mara nyingi akawapa ushindi kimuujiza. Kwa mfano, Yehova aliwasaidiaje Waisraeli washinde jiji la Yeriko? Kwa mwongozo wa Yehova, Waisraeli ‘walipopiga kelele kubwa za vita, ukuta ukaanguka chini,’ na kufanya iwe rahisi kwao kuliteka jiji hilo. (Yos. 6:20) Na walishindaje vita dhidi ya Waamori? “Yehova [alinyesha] mvua ya mawe makubwa kutoka angani . . . Kwa kweli, wale waliouawa na mvua ya mawe walikuwa wengi kuliko wale waliouawa na Waisraeli kwa upanga.”​—Yos. 10:6-11.

Leo, Yehova hapiganii taifa lolote duniani. Ufalme wake chini ya Mfalme Yesu, “si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yoh. 18:36) Kinyume chake, Shetani ndiye aliye na mamlaka juu ya serikali zote za wanadamu. Vita vya kikatili katika ulimwengu wake vinaonyesha uovu wake.​—Luka 4:5, 6; 1 Yoh. 5:19.

WAKRISTO WA KWELI NI WAFANYA-AMANI

Kama tulivyoona, leo hali yetu ni tofauti kabisa na taifa la kale la Israeli. Hata hivyo, tofauti hizo si sababu pekee zinazofanya tusiende vitani. Kuna sababu nyingine. Kwa mfano, Mungu alitabiri kwamba katika siku za mwisho, wale ambao wangefundishwa naye, ‘hawangejifunza vita tena kamwe,’ basi ni wazi kwamba hawangeshiriki katika vita. (Isa. 2:2-4) Isitoshe, Kristo alisema kwamba wanafunzi wake hawangekuwa “sehemu ya ulimwengu”; basi hawangeunga mkono mizozo ya ulimwengu.​—Yoh. 15:19.

Kristo hata aliwahimiza wafuasi wake wafanye jambo la ziada. Aliwaagiza waepuke mitazamo inayosababisha kinyongo, hasira, na vita. (Mt. 5:21, 22) Pia, aliwaagiza wafuasi wake wawe ‘wafanya amani’ na kuwapenda maadui wao.​—Mt. 5:9, 44.

Namna gani sisi binafsi? Inawezekana kwamba hatutamani kupigana katika vita, lakini je, tunaweza kuwa na mielekeo ya chuki moyoni ambayo inaweza kusababisha mizozano au migawanyiko katika kutaniko? Acheni tuendelee kujitahidi kuondoa hisia zozote kama hizo ndani yetu.​—Yak. 4:1, 11.

Badala ya kuunga mkono mizozano kati ya mataifa, tunaendeleza amani na umoja kati yetu. (Yoh. 13:34, 35) Acheni tuazimie kuendelea kutounga mkono upande wowote tunapotarajia siku ambayo Yehova ataondoa kabisa vita milele.​—Zab. 46:9.

^ Nyakati nyingine, makabila ya Israeli yalipigana kati yao, lakini vita hivyo havikumfurahisha Yehova. (1 Fal. 12:24) Ingawa hivyo, pindi fulani alikubaliana na vita hivyo kwa sababu makabila fulani yalikuwa yamemwasi au kufanya dhambi nyingine nzito.​—Amu. 20:3-35; 2 Nya. 13:3-18; 25:14-22; 28:1-8.