Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Ni Mvumilivu Kadiri Gani?

Mungu Ni Mvumilivu Kadiri Gani?

Maoni ya Biblia

Mungu Ni Mvumilivu Kadiri Gani?

“MUNGU, INGAWA ANAYO NIA YA KUONYESHA HASIRA YA KISASI YAKE NA KUJULISHA NGUVU YAKE, ALIVUMILIA KWA USTAHIMILIVU MWINGI VYOMBO VYA HASIRA YA KISASI VILIVYOFANYWA KUFAA KWA AJILI YA UHARIBIFU.”—WAROMA 9:22.

SIKUZOTE, Mungu amevumilia mabaya mengi na uovu unaoonekana waziwazi. Zaidi ya miaka 3,000 iliyopita, Yobu aliomboleza hivi: “Mbona waovu wanaishi, na kuwa wazee, naam, na kuongezeka kuwa na nguvu? Kizazi chao kinathibitika nao machoni pao, na wazao wao mbele ya macho yao. Nyumba zao zi salama pasina hofu, wala fimbo ya Mungu haiwapigi.” (Ayubu 21:7-9) Watu wengine wanaopenda haki, kama vile nabii Yeremia, wamehangaishwa pia na namna ambavyo Mungu huonekana kuwa anavumilia watu wabaya.—Yeremia 12:1, 2.

Wewe waonaje? Je, unatatanishwa na jinsi Mungu anavyoruhusu uovu? Je, nyakati nyingine wewe huhisi kwamba Mungu apaswa kuharakisha kuwaharibu waovu wote mara moja? Fikiria yale ambayo Biblia husema kuhusu mipaka ya uvumilivu wa Mungu na kwa nini yeye ni mvumilivu.

Kwa Nini Mungu Ni Mvumilivu?

Kwanza kabisa, lazima tuulize hivi: Kwa nini Mungu huvumilia ubaya na yeye ndiye mwenye viwango vya juu kabisa vya uadilifu? (Kumbukumbu la Torati 32:4; Habakuki 1:13) Je, hiyo yamaanisha kwamba yeye hukubali uovu? La hasha! Fikiria mfano ufuatao: Hebu wazia kuna daktari-mpasuaji asiyezingatia usafi hata kidogo ambaye huwaumiza sana wagonjwa. Ikiwa yeye hufanya kazi hospitalini, si angefutwa kazi mara moja? Lakini uvumilivu wa kipekee ungehitajika katika hali fulani. Katika hali ya dharura, kama vile katika sehemu zenye vita, je, haingefaa kuwavumilia madaktari-wapasuaji wanaofanya kazi katika mazingira ya kishamba na yaliyo hatari, labda hata wakitumia vifaa duni vya upasuaji?

Vivyo hivyo, leo Mungu anavumilia kwa subira mambo mengi anayochukia kabisa. Ijapo anachukia uovu, yeye huuruhusu uendelee kwa muda. Kuna sababu nzuri za kufanya hivyo. Sababu moja ni kwamba kufanya hivyo huruhusu wakati ili yale masuala mazito yaliyozushwa na uasi wa Shetani kwenye shamba la Edeni yasuluhishwe kabisa. Masuala hayo yanahusiana na kama njia ya Mungu ya kutawala inafaa na ni ya haki. Pia, kuvumilia kwake ubaya kwa subira huwapa watu wabaya wakati na fursa ya kubadilika.

Mungu Mwenye Rehema na Subira

Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walijiunga na Shetani kumwasi Mungu. Kwa haki, Mungu angewaharibu papo hapo. Badala yake, alithibitika kuwa mwenye rehema na subira, akiwaruhusu kwa upendo wapate watoto. Lakini watoto hao, na wanadamu wote waliotokana nao, walizaliwa wakiwa na dhambi.—Waroma 5:12; 8:20-22.

Mungu alikusudia kuwaokoa wanadamu kutoka kwenye hali yao ya kusikitisha. (Mwanzo 3:15) Hata hivyo, kwa kuwa yeye huelewa jinsi hali ya kutokamilika ambayo tulirithi kutoka kwa Adamu inavyotuathiri, kwa sasa yeye huonyesha subira na rehema nyingi sana. (Zaburi 51:5; 103:13) Yeye ni “mwingi wa fadhili [“fadhili-upendo,” NW]” na yu tayari na anataka ‘kusamehe kabisa.’—Zaburi 86:5, 15; Isaya 55:6, 7.

Mipaka ya Uvumilivu wa Mungu

Hata hivyo, halingekuwa jambo la upendo na la akili ikiwa Mungu angeruhusu ubaya uendelee milele. Hakuna baba mwenye upendo ambaye angevumilia kumwona mtoto wake mmoja akiendelea daima kuwaumiza sana washiriki wengine wa familia kimakusudi. Kwa hiyo, kwa habari ya kuvumilia dhambi, sikuzote subira ya Mungu itasawazishwa kwa sifa nyingine kama upendo, hekima, na haki. (Kutoka 34:6, 7) Mara tu kusudi lake la kustahimili limalizikapo, ataacha kuvumilia uovu.—Waroma 9:22.

Mtume Paulo alionyesha jambo hilo waziwazi. Yeye alisema hivi wakati fulani: “Katika vizazi vilivyopita [Mungu] aliruhusu mataifa yote yaendelee katika njia zayo.” (Matendo 14:16) Kwenye pindi nyingine Paulo alizungumzia jinsi “Mungu ameachilia nyakati za kutokuwa na ujuzi kwa namna hiyo” kwa habari ya watu walioasi sheria na kanuni zake. Paulo aliendelea hivi: “Sasa [Mungu] anaambia wanadamu kwamba wapaswa wote kila mahali kutubu.” Kwa nini? “Kwa sababu ameweka siku ambayo katika hiyo akusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa.”—Matendo 17:30, 31.

Faidika Sasa Kutokana na Uvumilivu wa Mungu

Hivyo basi, hakuna mtu anayepaswa kufikiri kwamba anaweza kupuuza sheria za Mungu na kisha amwombe Mungu msamaha kimchezo ili aepuke matokeo ya matendo yake. (Yoshua 24:19) Watu wengi katika taifa la Israeli la kale walifikiri wangefanya hivyo. Hawakutaka kubadilika. Walikosa kusudi la uvumilivu na subira ya Mungu. Mungu hakuendelea kuvumilia ubaya wao daima.—Isaya 1:16-20.

Biblia huonyesha kwamba ili kuepuka hukumu ya mwisho ya Mungu, mtu apaswa ‘kutubu’—yaani, akubali hali yake ya kutokamilika ya dhambi mbele ya Mungu kwa kujuta sana, kisha aache ubaya kabisa. (Matendo 3:19-21) Kisha, kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Kristo, Yehova Mungu atamsamehe. (Matendo 2:38; Waefeso 1:6, 7) Kwa wakati wake unaofaa, Mungu ataondoa madhara yote yenye kuhuzunisha ya dhambi ya Adamu. Kutakuwapo na “mbingu mpya na dunia mpya” ambapo hatavumilia tena “kuwapo . . . kwa vitu vinavyopaaza kilio ili viharibiwe.” (Ufunuo 21:1-5; Waroma 9:22, Phillips) Hilo ni tokeo zuri kama nini la uvumilivu wa Mungu wa ajabu, ulio na mipaka!

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mungu aliwaruhusu Adamu na Hawa wapate watoto