Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tupo Hapa?

Kwa Nini Tupo Hapa?

Kwa Nini Tupo Hapa?

KULINGANA na Biblia, Mungu ambaye jina lake ni Yehova ana akili nyingi sana. Yeye ndiye Chanzo cha nguvu zote ulimwenguni na Muumba wa ulimwengu. (Zaburi 83:18; 92:5) Sura ya kwanza ya Biblia inasema hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” Baadaye, Mungu alimfanya mtu kwa “mfano” wake, yaani, akiwa na sifa kama zake—na Mungu akamwambia mwanadamu azae na kuijaza dunia.—Mwanzo 1:1, 26, 28.

Je, hilo linamaanisha kwamba Mungu aliuumba ulimwengu, kutia ndani dunia pamoja na wanyama na mimea mingi iliyomo kwa ajili tu ya wanadamu? Na je, tupo hapa ili tu tufurahie maisha kwa miaka michache, tule, tunywe, na kuzaa?

Kwa Nini Mungu Alituumba?

Yehova Mungu alimuumba mwanadamu ili kuonyesha upendo wake—alitaka kushiriki uhai na furaha yake pamoja na wanadamu. Bila shaka, Mungu alifurahia sana kutokeza uumbaji wa aina mbalimbali ili mwanadamu azungukwe na viumbe wengi maridadi. Jambo muhimu zaidi ni kwamba wanadamu waliumbwa wawe na uhusiano wa karibu na Muumba wao, wamfahamu, na kuwasiliana naye. Waliumbwa waishi milele chini ya hali kamilifu na zenye amani.—Mwanzo 3:8, 9; Zaburi 37:11, 29.

Yehova pia aliwapa wanadamu kazi muhimu na yenye kuridhisha. Mungu aliwaambia hivi wanadamu wa kwanza: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.” (Mwanzo 1:28) Naam, wanadamu wawili wa kwanza na watoto wao wangeifanya dunia yote kuwa paradiso yenye kupendeza.

Lakini mambo hayakutukia kama Yehova alivyokuwa amekusudia. * Hata hivyo, kusudi la kwanza la Mungu kwa ajili ya mwanadamu litatimia.—Isaya 46:9-11; 55:11.

Kwa sasa, jitihada za mwanadamu za kutafuta kusudi zinaonyesha kwamba anatamani na anahitaji kumfahamu Mungu na kuwa na uhusiano naye. Mwanadamu aliumbwa akiwa kiumbe mwenye akili aliye na tamaa ya kuchunguza na kuelewa mambo. Na Biblia inasema kwamba mwanadamu ataendelea kutafuta habari zenye kuridhisha kumhusu Mungu na uumbaji wake milele.

Mwandikaji mmoja wa Biblia anaeleza kusudi la mwanadamu kwa njia hii: “Nimeona shughuli ambayo Mungu amewapa wana wa binadamu wajishughulishe nayo. Amefanya kila kitu kiwe chenye kupendeza kwa wakati wake. Tena wakati usio na kipimo ameuweka ndani ya moyo wao, ili mwanadamu asiweze kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho. Nimekuja kujua kwamba hakuna jambo lingine bora kwao kuliko mtu kufurahi na kufanya mema maishani mwake; na pia kwamba kila mtu ale, naam, anywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu. Hiyo ndiyo zawadi ya Mungu.” (Mhubiri 3:10-13) Kwa hiyo, mwanadamu hatafikia mwisho wa kujifunza kumhusu Yehova na uumbaji wake.

Jifunze Kumhusu Mungu

Unaweza kujifunza kumhusu Yehova kwa kuchunguza uumbaji wake. Mwandikaji mmoja wa Biblia alisema kwamba “sifa zake [Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu.” (Waroma 1:20) Naam, uumbaji unafunua upendo, hekima, na nguvu za Yehova.

Njia nyingine muhimu ya kujifunza kumhusu Mungu ni Biblia. Kitabu hicho kilichoongozwa na roho ya Mungu kinatueleza mambo mengi zaidi kumhusu Yehova kuliko yale tunayoweza kujifunza kutokana na uumbaji wake. Kinatueleza maoni yake, sifa zake, na kusudi lake.

Biblia inasema hivi kuhusu kusudi la Mungu: “Mbingu ni mbingu za Yehova, bali dunia amewapa wana wa binadamu.” (Zaburi 115:16) Inaonekana kwamba dunia ndiyo mahali panapofaa zaidi kwa mwanadamu kuishi, nayo iliumbwa hasa kwa kusudi hilo.

Vipi kuhusu ulimwengu wetu mkubwa? Je, nyota hizo zote zinazotuzunguka ziliumbwa ili tu kudumisha usawaziko kamili katika mfumo wetu wa jua ili kuendeleza uhai duniani? Je, jua, nyota, na sayari nyingine ziliumbwa ili tu kurembesha anga letu usiku? Tunapaswa kutambua kwamba bado kuna mambo mengi sana ambayo hatujui. Lakini hilo ni jambo zuri! Kwa nini?

Hata mwanadamu aishi milele, hataweza kuelewa yote ambayo Mungu amefanya na anayokusudia kufanya. Mungu anataka wakati wetu ujao uwe wakati wa kuvumbua mambo na kuwa na shangwe isiyo na mwisho. Kuishi milele kwa furaha hapa duniani kutawapa wanadamu watiifu nafasi tele ya kuvumbua mambo mengi sana kuhusu ulimwengu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Uovu na kuteseka kunawazuia watu wengi kuamini kwamba kuna Muumba mwenye upendo. Kwa habari zaidi kuhusu jambo hilo, ona sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Mwanadamu aliumbwa akiwa kiumbe mwenye akili aliye na tamaa ya kuchunguza na kuelewa mambo

[Picha katika ukurasa wa 10]

Biblia inaonyesha kwamba dunia iliumbwa hasa ili wanadamu waifurahie