Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Sifanikiwi?

Kwa Nini Sifanikiwi?

Vijana Huuliza

Kwa Nini Sifanikiwi?

“Nilikuwa nikijihisi duni nilipojilinganisha na rafiki yangu. Alipata kila kitu kwa ­urahisi​​—⁠ni kana kwamba hata hakukifanyia kazi! Hilo lilinifanya nijiulize nilikuwa na ­tatizo gani. Nilikuwa nikijivunja moyo bila ­sababu.”​​—⁠ Annette. *

JE, HISIA za kwamba hufai zinakuzuia kujaribu mambo mapya? Je, nyakati nyingine maneno yanayosemwa kwa nia nzuri na watu fulani unaoheshimu yanakufanya usijiamini? Je, umevunjika moyo kwa sababu ya makosa uliyofanya zamani na hivyo unahisi hutaki kujaribu tena? Ikiwa ndivyo, unaweza kukabiliana jinsi gani na hisia hizo—ziwe za kweli au za kuwaziwa?

Utafaidika sana kwa kupata jibu la swali hilo la mwisho kwa sababu kila mtu hufanya makosa wakati mmoja au mwingine. (Waroma 3:23) Lakini watu wanaoweza kukabiliana na hisia za kushindwa, ni wenye moyo mkuu. Hilo linamaanisha kwamba wanaweza kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu makosa yao, wafanye marekebisho, na kujaribu tena. Wanapofanya hivyo, wanakuwa na uwezekano mkubwa zaidi wa kufaulu! Sasa hebu tuone jinsi unavyoweza kukabiliana na hali tatu—uwezekano wa kutofanikiwa, kufikiri umeshindwa, na kushindwa kabisa kufanikiwa.

UWEZEKANO wa KUTOFANIKIWA → NI NINI KINACHOWEZA KUTOKEA? Unatarajia kwamba hutafanikiwa na hivyo unaamua kwamba hutajaribu kufanya jambo lolote.

Kutambua tatizo. Tia alama ya ✔ kando ya jambo unalohisi kwamba ungependa kufanya—lakini unahisi kwamba hata ukijaribu hutafaulu.

◯ Kutetea imani yako kwa wanafunzi wenzako

◯ Kutafuta kazi

◯ Kusema mbele ya umati

◯ Kushiriki katika mchezo fulani

◯ Kuimba au kujifunza kucheza ala ya muziki

◯ Mambo mengine

Chunguza kwa makini. Fikiria kuhusu jambo ambalo umechagua hapo juu, na utafakari kwa makini matokeo kwa kujibu maswali yafuatayo:

‘Ningependa kupata matokeo gani?’

․․․․․

‘Ninahofu nitapatwa na nini?’

․․․․․

Sasa andika sababu moja ambayo inakufanya uone unapaswa kujaribu kufanya jambo hilo, hata kama utashindwa.

․․․․․

Mfano wa Biblia. Musa alipoagizwa na Yehova Mungu aongoze taifa la Israeli, kwanza kabisa alifikiria matatizo ambayo yangetokea. Alimwambia Mungu hivi: “Waisraeli hawataniamini wala kunisikiliza.” Kisha akaanza kufikiria udhaifu wake. “Mimi sina ufasaha wa kuongea tangu zamani,” akasema. “Ulimi wangu ni mzito.” Hata Yehova alipoahidi kumsaidia, Musa alimwomba hivi: “Tafadhali nakusihi, umtume mtu mwingine.” (Kutoka 4:1, 10, 13, Biblia Habari Njema) Hatimaye, Musa alikubali mgawo wake, na tunajua matokeo. Chini ya uongozi wa Mungu, Musa aliwaongoza Waisraeli kwa miaka 40.

Unaweza kufanya nini? Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote.” (Mhubiri 9:10) Kwa hiyo, badala ya kuhofu kwamba utashindwa, jitahidi kadiri uwezavyo katika jambo unalofanya. Mbona usifikiri kuhusu wakati ambapo ulitimiza jambo fulani kwa njia bora kuliko ulivyotarajia? Ulijifunza nini kuhusu uwezo wako kutokana na mafanikio hayo? Matokeo hayo yanaweza kukusaidia jinsi gani kukabiliana na hofu ya kushindwa?

Dokezo: Ikiwezekana, tafuta madokezo kutoka kwa mzazi au rafiki mkomavu anayeweza kukusaidia ujiamini zaidi. *

KUFIKIRI UMESHINDWA → UNACHOFIKIRI KIMETUKIA Mtu mwingine anapofaulu katika jambo ambalo ulitaka pia kufanya, unajihisi kana kwamba umeshindwa unapojilinganisha na yeye.

Kutambua tatizo. Unajilinganisha na nani, na ni mambo gani ambayo mtu huyo tayari ametimiza yanayofanya uhisi kana kwamba umeshindwa?

․․․․․

Chunguza kwa makini. Je, mafanikio ya mtu huyo yanamaanisha kwamba kwa kweli umeshindwa? Andika hapa chini kuhusu tukio la hivi karibuni, kama vile mtihani wa shule, ambao ulifanya VIZURI lakini mtu mwingine alifanya vizuri zaidi.

․․․․․

Sasa andika kwa nini kulikuwa na faida kujaribu kufanya jambo hilo.

․․․․․

Mfano wa Biblia. Kaini ‘aliwaka hasira’ alipojua kwamba Yehova alimtazama kwa kibali ndugu yake Abeli. Yehova alimwonya Kaini kuhusu wivu wake, lakini pia alionyesha uhakika kwamba Kaini angeweza kufaulu, iwapo angechagua kufanya hivyo. “Ukigeuka utende mema,” Yehova akamwambia, “je, hutainuliwa?” *Mwanzo 4:6, 7.

Unaweza kufanya nini? Badala ya “kuchochea mashindano”—hata ikiwa ni akilini mwako—kubali kwamba watu wengine wamefanikiwa. (Wagalatia 5:26; Waroma 12:15) Wakati huohuo, bila kujivuna, tambua sifa zako za pekee. Biblia inasema hivi: “Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake.”Wagalatia 6:4.

KUSHINDWA KABISA KUFANIKIWA → KILE AMBACHO TAYARI KIMETUKIA Unafikiria jinsi ulivyoshindwa wakati uliopita na hivyo unakata kauli kwamba hakuna faida kujaribu tena.

Kutambua tatizo. Ni jambo gani unaloshindwa kufanya linalokufanya uvunjike moyo zaidi?

․․․․․

Chunguza kwa makini. Je, tatizo uliloandika hapo juu linamaanisha kwamba kwa kweli wewe ni duni? Kwa mfano, ikiwa umeshindwa na udhaifu fulani, je, hilo linamaanisha kwamba huna tumaini lolote? Au hilo linaonyesha kwamba unahitaji msaada? Ukianguka wakati wa michezo, utakubali kusaidiwa ili urudie mchezo huo. Mbona usiwe na mtazamo huohuo unaposhughulikia udhaifu wako? Andika jina la mtu unayeweza kuzungumza naye kuhusu tatizo lako. *

․․․․․

Mfano wa Biblia. Nyakati nyingine, mtume Paulo alivunjika moyo kwa sababu ya udhaifu wake. “Ole wangu mimi mutu wa taabu,” akaandika. (Waroma 7:24, Zaire Swahili Bible) Hata hivyo, Paulo alitambua kwamba kutokamilika kwake hakukumaanisha kwamba alikuwa duni. Aliandika hivi: “Nimepigana pigano zuri, nimekimbia mwendo mpaka mwisho, nimeishika imani.”—2 Timotheo 4:7.

Unaweza kufanya nini? Badala ya kukazia fikira udhaifu wako tu, tafakari pia kuhusu sifa zako nzuri. Yehova hufanya hivyo. Biblia inasema hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.”—Waebrania 6:10; Zaburi 110:3.

Kumbuka: Hakuna mtu mkamilifu. Kila mtu hukosa kufaulu katika jambo fulani. Ukijifunza kuwa na moyo mkuu, utakuwa umepata kitu cha thamani sana kitakachokusaidia hata utakapokuwa mtu mzima. Methali 24:16 linasema hivi: “Huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba, naye hakika atasimama.” Unaweza kuwa mtu wa aina hiyo!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Jina limebadilishwa.

^ fu. 31 Kaini alichagua kupuuza shauri la Yehova. Kushindwa kwake kunaonyesha wazi unapaswa kuzuia kabisa mwelekeo wowote wa kumwonea wivu mtu mwingine kwa sababu ya mafanikio yake.—Wafilipi 2:3.

^ fu. 36 Mkristo ambaye ametenda dhambi nzito atafaidika kwa kuzungumza na mzee wa kutaniko.—Yakobo 5:14, 16.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 27]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Unajidanganya ikiwa utafanya mambo yaleyale tu unayoweza kufanya na kufaulu bila kujaribu kufanya mambo mengine mapya ukihofu kwamba hutafaulu.”

“Unaposhindwa kufaulu unaweza kuamua ama kujifunza kutokana na tatizo ulilopata na kuchochewa kuboresha uwezo wako, ama unaweza kukazia fikira tatizo lenyewe bila kujitahidi na kuridhika tu kufanya mambo unayoweza kufanya. Wewe ndiye unayeamua utakuwa mtu wa aina gani.”

“Nikijua kwamba huenda nisifanye jambo fulani vizuri, mimi hufanya utani kulihusu. Kucheka ni bora kuliko kununa. Ikiwa umejiwekea matarajio ya juu sana, hutawahi kuwa na furaha.”

[Picha]

Andrea

Trenton

Naomi

[Sanduku katika ukurasa wa 28]

MBONA USIWAULIZE WAZAZI WAKO?

Mlipokuwa na umri wangu, mlikabili matatizo gani ya kibinafsi? Mlikabiliana nayo jinsi gani? Je, bado mnakabiliana na matatizo ya aina hiyo mara kwa mara?

․․․․․

[Picha katika ukurasa wa 28]

Baada ya kuanguka, mtu mwenye moyo mkuu husimama—naye hukubali msaada iwapo ni lazima