Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Niliona Ukosefu wa Haki Kila Mahali

Niliona Ukosefu wa Haki Kila Mahali

NILIZALIWA mwaka wa 1965 katika familia maskini huko Ireland Kaskazini. Nililelewa Mkoa wa Derry wakati wa ile “Mizozo,” yaani, vita vyenye jeuri kati ya Wakatoliki na Waprotestanti ambavyo viliendelea kwa zaidi ya miaka 30. Wakatoliki waliokuwa wachache walihisi kwamba wamebaguliwa na serikali iliyokuwa na Waprotestanti wengi, na walilalamika kwamba kulikuwa na matendo ya ukosefu wa haki kama vile kukandamizwa na polisi, hila katika uchaguzi, kunyimwa ajira, na upendeleo katika kutoa makao.

Niliona ukosefu wa haki na ukosefu wa usawa kila mahali. Hata siwezi kukumbuka ni mara ngapi nilipigwa, niliburutwa kutoka kwenye gari na kuelekezewa bunduki, au kuhojiwa na kupekuliwa na polisi au askari-jeshi. Nilihisi kwamba ninaonewa, na nikajiambia, ‘Mambo ni mawili, ama nikubali kutendewa hivi, ama nilipize kisasi!’

Nilishiriki katika maandamano ya mwaka wa 1972 yaliyoitwa Jumapili Yenye Umwagaji wa Damu, ili kuwakumbuka watu 14 waliopigwa risasi na kuuawa na wanajeshi wa Uingereza, na pia nilishiriki katika maandamano ya kuwakumbuka wafungwa waliopinga utawala wa Uingereza huko Ireland Kaskazini ambao walisusia chakula na kufa katika mwaka wa  1981. Nilisimamisha bendera za Ireland Kaskazini zilizokuwa zimepigwa marufuku na nikaandika mahali popote ukutani maneno yenye kupinga utawala wa Uingereza. Ni kana kwamba kila mara kulikuwa na ukatili au mauaji ya Mkatoliki yaliyofanya watu waandamane. Mara nyingi maandamano hayo yaligeuka kuwa ghasia.

Nilipokuwa katika chuo kikuu, nilijiunga na kikundi cha wanafunzi walioandamana ili kutetea mazingira. Baadaye nilihamia London, na nikiwa huko nilijiunga na vikundi vya waandamanaji wa kijamii waliokuwa wakipinga sera za serikali ambazo ziliwanufaisha tu matajiri na kuwaumiza maskini. Nilishiriki katika migomo ya vyama vya wafanyakazi ili kupinga kupunguzwa kwa mishahara, na pia nilishiriki katika maandamano ya kupinga kodi ya kichwa ya mwaka wa 1990. Maandamano hayo yalisababisha uharibifu mkubwa katika uwanja wa Trafalgar Square.

Hata hivyo, mwishowe nilikatishwa tamaa. Badala ya kutimiza malengo yake, mara nyingi maandamano yalichochea chuki tu.

Licha ya kuwa na nia nzuri, wanadamu hawawezi kuleta haki na usawa

Katika kipindi hicho, rafiki yangu alinijulisha kwa Mashahidi wa Yehova. Walinionyesha katika Biblia kwamba Mungu anajali tunapoteseka na kwamba ataondoa madhara yote ambayo yamesababishwa na wanadamu. (Isaya 65:17; Ufunuo 21:3, 4) Licha ya kuwa na nia nzuri, wanadamu hawawezi kuleta haki na usawa. Tunahitaji mwongozo wa Mungu na pia uwezo wake wa kushinda roho wasioonekana ambao ndio wanaosababisha matatizo ulimwenguni.—Yeremia 10:23; Waefeso 6:12.

Sasa naona kwamba maandamano niliyoshiriki ya kupinga ukosefu wa haki yalikuwa bure tu kama vile kupanga vyombo katika nyumba inayoteketea. Nimefarijika sana kujua kwamba kuna siku hakutakuwa na ukosefu wa haki katika dunia hii, kutakuwa na usawa kila mahali.

Biblia inafundisha kwamba Yehova Mungu ni “mpenda-haki.” (Zaburi 37:28) Hiyo ni sababu moja inayotuhakikishia kwamba ataleta haki kwa njia ambayo serikali za kibinadamu zimeshindwa kufanya. (Danieli 2:44) Ikiwa ungependa kujifunza mengi, wasiliana na Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu au tembelea Tovuti yetu kwenye www.ps8318.com/sw.