Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA

Mageuzi

Mageuzi

Baadhi ya watu husema uhai umetokana na mageuzi. Wengine wanadai kwamba Mungu alianzisha uumbaji na kisha hatua zilizofuata zikaendelezwa na mageuzi. Biblia inasema nini?

Je, simulizi la Biblia la uumbaji linaonyesha kwamba ulimwengu ulitokea kwa sababu ya mlipuko mkubwa wa ghafla?

Biblia inaeleza hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Haielezi jinsi hasa Mungu alivyoumba kila kitu. Kwa hiyo, hata ikiwa kulitokea mlipuko mkubwa sana wa ghafla uliotokeza ulimwengu wetu, hilo lisingepingana na jambo ambalo limeelezwa kwenye Biblia. Badala yake, Mwanzo 1:1 ingeonyesha aliyetokeza mlipuko huo mkubwa.

Wanasayansi wengi wanaamini kuwa mlipuko huo mkubwa ulitokea ghafla na kusababisha chembe ndogo sana zijipange na kutokeza nyota na sayari. Biblia haikubaliani na maoni hayo badala yake inasema kwamba ulimwengu ulitokezwa na Mungu, iwe alitumia mlipuko mkubwa au njia nyingine ya uumbaji.

“Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.”Mwanzo 1:1.

Je, Biblia inakubali kwamba viumbe hai hubadilika kadiri muda unavyopita?

Ndio. Biblia inasema kwamba Mungu aliumba viumbe hai ‘kulingana na aina zao.’ (Mwanzo 1:11, 12, 21, 24, 25) Je, inawezekana mabadiliko yakatokea ndani ya jamii fulani ya viumbe? Ndio. Hata hivyo, je, mabadiliko yanayotokea ndani ya jamii fulani ya viumbe yanathibitisha kwamba hatimaye jamii mpya za viumbe zinaweza kutokea? Hapana.

Fikiria kisa hiki: Mwaka wa 1970, watafiti walichunguza ndege aina ya shorewanda katika Kisiwa cha Galápagos. Waligundua kwamba mabadiliko ya hali ya hewa yalisababisha shorewanda wenye midomo mikubwa kidogo waishi muda mrefu zaidi. Jambo hilo limefanya wengine waone hilo kuwa uthibitisho wa mageuzi. Je, jambo hilo lilikuwa uthibitisho wa mageuzi, au yalikuwa mabadiliko ya viumbe yaliyotokana na mazingira? Miaka kadhaa baadaye, shorewanda wenye midomo midogo walikuwa wengi zaidi. Jambo hilo lilifanya profesa wa anthropolojia, Jeffrey H. Schwartz, kufikia mkataa wa kwamba mabadiliko hayo yanasaidia jamii ya viumbe iendelee kuishi kwa muda mrefu hali zinapobadilika lakini “hayatokezi jambo lolote jipya.”

Je, inawezekana kupatanisha Biblia na dhana ya mageuzi?

Biblia inasema kwamba ‘Mungu aliumba vitu vyote.’ (Ufunuo 4:11) ‘Hakupumzika’ mpaka kazi zake zilipokamilika. (Mwanzo 2:2) Maandiko hayo yanaonyesha wazi jambo hili: Mungu hakuumba kiumbe cha aina moja na kisha akapumzika, au akasubiri tu, kiumbe hicho kilipokuwa kikigeuka kwa mamilioni ya miaka kuwa samaki, sokwe, na binadamu. * Dhana hiyo, inayoitwa mageuzi makubwa, inapinga jukumu la Muumba, ambaye Biblia husema “aliumba mbingu na vitu vilivyo ndani yake na dunia na vitu vilivyo ndani yake na bahari na vitu vilivyo ndani yake.”—Kutoka 20:11; Ufunuo 10:6.

“Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote.”Ufunuo 4:11.

Jifunze zaidi: Biblia inasema kwamba “sifa [za Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa.” (Waroma 1:20) Kujifunza kuhusu Mungu kunaweza kukusaidia uwe na maisha yenye maana, kwa sababu ana kusudi zuri ambalo linawahusisha wale wote wanaomtafuta. (Mhubiri 12:13; Waebrania 11:6) Kwa habari zaidi, tembelea www.ps8318.com/sw au wasiliana na Mashahidi wa Yehova. Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > MAJIBU YA MASWALI YA BIBLIA.

^ fu. 12 Tofauti na maoni ya watu, Biblia haiungi mkono dhana ya kwamba Mungu aliumba dunia kwa siku sita zenye urefu wa saa 24. Kwa habari zaidi, ona ukurasa wa 24-27 wa broshua UhaiUlitokana na Muumba? Broshua hiyo imechapishwa na Mashahidi wa Yehova na unaweza kuipakua bila malipo kwenye Tovuti ya www.ps8318.com/sw.