Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ahadi Ambazo Zitatimia

Ahadi Ambazo Zitatimia

Habari njema ya Ufalme wa Mungu inahubiriwa ulimwenguni kote kama Yesu alivyotabiri. (Mathayo 24:14) Kitabu cha Danieli kwenye Biblia kinasema kwamba Ufalme huo ni serikali ya Mungu. Sura ya 2 ya kitabu hicho ina unabii kuhusu baadhi ya serikali kubwa za wanadamu au falme ambazo zimekuwa zikitawala, moja baada ya nyingine, tangu Babiloni ya kale hadi kufikia wakati wetu. Mstari wa 44 unasema hivi kuhusu mambo yatakayotukia hivi karibuni:

“Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa kamwe. Na ufalme huo hautakabidhiwa watu wengine wowote. Utazipondaponda na kuzikomesha falme hizi zote, nao pekee utasimama milele.”

Unabii huo na unabii mwingine wa Biblia unaonyesha kwamba Ufalme wa Mungu utachukua mahali pa serikali za wanadamu na kuleta amani na utulivu kwa wanadamu duniani. Maisha yatakuwaje Ufalme huo utakapokuwa ukitawala? Acheni tuchunguze ahadi kadhaa ambazo zitatimia hivi karibuni.

  • VITA HAVITAKUWEPO

    Zaburi 46:9: “[Mungu] anakomesha vita katika dunia yote. Anauvunja upinde na kuuvunja mkuki vipandevipande; anayateketeza magari ya vita motoni.”

    Hebu wazia jinsi ambavyo hali zingekuwa duniani iwapo ujuzi na pesa zote zinazotumiwa kutengenezea silaha zingetumiwa katika miradi inayowanufaisha wanadamu badala ya kuwaua! Ufalme wa Mungu utatimiza ahadi hiyo.

  • HAKUTAKUWA NA MAGONJWA

    Isaya 33:24: “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”

    Fikiria jinsi maisha yatakavyokuwa duniani wakati ambapo hakuna yeyote ambaye atapatwa na ugonjwa wa moyo, saratani, malaria, au magonjwa mengine. Hakutakuwa na uhitaji wa hospitali wala dawa. Wanadamu watakaoishi duniani wakati ujao watafurahia afya kamilifu.

  • HAKUTAKUWA NA UPUNGUFU WA CHAKULA

    Zaburi 72:16: “Kutakuwa na nafaka nyingi duniani; itafurika juu ya milima.”

    Kutakuwa na chakula cha kutosha duniani pote na kila mtu ataweza kukipata. Hakutakuwa tena na njaa wala utapiamlo.

  • HAKUTAKUWA NA MAUMIVU, HUZUNI, WALA KIFO

    Ufunuo 21:4: “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”

    Hilo linamaanisha kwamba wanadamu wataishi milele wakiwa wakamilifu katika dunia paradiso! Muumba wetu mwenye upendo, Yehova Mungu, ametuahidi hivyo.

“HAKIKA LITAFANIKIWA”

Je, kweli ahadi hizo zitatimia au ni hadithi tu? Ingawa watu wengi wanakubali kwamba maisha yanayotajwa na kuelezewa katika Biblia yanavutia, kwa wengi wao suala la kuishi milele haliingii akilini. Hilo halishangazi kwa sababu hakuna mwanadamu yeyote aliyewahi kuishi maisha ya aina hiyo.

Wanadamu wamekuwa watumwa wa dhambi na kifo na kutaabishwa na maumivu, mateso, na kuishi maisha magumu kwa muda mrefu sana hivi kwamba wamekubaliana na hali hizo na kuziona kuwa za kawaida. Lakini hilo ni kinyume kabisa na kile ambacho Muumba wetu, Yehova Mungu, alikusudia alipowaumba wanadamu.

Ili kutusaidia kuwa na uhakika kuelekea ahadi zake, Mungu alisema hivi kuhusiana na neno linalotoka kinywani mwake: “Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatimiza jambo lolote linalonipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 55:11.

Biblia inasema kwamba Yehova ni Mungu “asiyeweza kusema uwongo.” (Tito 1:2) Kwa kuwa ameahidi kufanya mambo yote hayo mazuri, maswali tunayoweza kujiuliza ni: Je, kweli inawezekana kupata zawadi hiyo ya uzima wa milele katika dunia Paradiso? Tunapaswa kufanya nini ili tufurahie mambo ambayo Mungu ametuahidi? Utapata majibu ya maswali hayo katika makala zinazofuata za gazeti hili.