Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuteseka kwa Wanadamu​—Je, Ni Adhabu Kutoka kwa Mungu?

Kuteseka kwa Wanadamu​—Je, Ni Adhabu Kutoka kwa Mungu?

LUZIA ANA ULEMAVU KWENYE MGUU WAKE WA KUSHOTO. Alipokuwa mdogo, aliugua polio, ugonjwa unaoambukizwa kwa urahisi sana ambao hushambulia mfumo wa neva mwilini. Alipokuwa na umri wa miaka 16, mwajiri wake alimwambia hivi: “Mungu alikupa ulemavu kwa sababu hukuwa mtiifu na ulimsumbua mama yako.” Miaka mingi imepita, lakini Luzia bado anakumbuka jinsi maneno hayo yalivyomuumiza.

DAMARIS ALIPOGUNDUA KWAMBA ANA SARATANI YA UBONGO, baba yake alimuuliza: “Kwa nini umepatwa na hali hii? Umefanya kosa gani? Lazima uwe umefanya jambo baya sana. Ndiyo sababu Mungu anakuadhibu.” Maneno hayo yalimchoma sana Damaris.

Wazo la kwamba magonjwa ni adhabu kutoka kwa Mungu limekuwepo kwa muda mrefu. Kitabu kimoja (Manners and Customs of Bible Lands) kinasema kuwa katika siku za Kristo, watu wengi waliamini kwamba “ugonjwa ulikuwa adhabu ya dhambi fulani ya yule aliyekuwa akiugua au ya watu wa familia yake.” Kitabu kingine (Medieval Medicine and the Plague) kinasema kwamba karne nyingi baada ya siku za Kristo, “baadhi ya watu waliamini kwamba Mungu alileta magonjwa ili kuwaadhibu kwa sababu ya dhambi zao.” Kwa hiyo mamilioni ya watu walipokufa barani Ulaya kutokana na ugonjwa ulioenea katika karne ya 14, je, ni Mungu aliyekuwa akiwaadhibu kwa sababu ya uovu wao? Au je, tatizo hilo lilisababishwa tu na bakteria, kama ambavyo watafiti wa tiba waligundua? Huenda baadhi yetu tukajiuliza, je, kweli Mungu anatumia magonjwa kuwaadhibu wanadamu kwa sababu ya dhambi zao? *

FIKIRIA HILI: Ikiwa magonjwa na hali ngumu tunazokabili ni adhabu kutoka kwa Mungu, kwa nini Yesu aliwaponya wagonjwa? Je, kitendo hicho hakingekuwa sawa na kupinga haki na uadilifu wa Mungu? (Mathayo 4:23, 24) Yesu hawezi kamwe kutenda kinyume na mapenzi ya Mungu. Alisema hivi: “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza” na, “ninafanya kama vile Baba alivyoniamuru.”—Yohana 8:29; 14:31.

Biblia inasema wazi kwamba Yehova Mungu “kamwe hana ukosefu wa haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Kwa mfano, Mungu hawezi kusababisha ndege ianguke na kuua mamia ya watu wasio na hatia ili tu amwadhibu mtu fulani ndani ya ndege hiyo! Akizingatia uadilifu wa Mungu, Abrahamu, mtumishi mwaminifu wa Mungu, alisema kwamba Mungu hawezi kamwe ‘kumfagilia mbali mwadilifu pamoja na mwovu.’ Alimwambia, hilo “ni jambo usiloweza kuwazia.” (Mwanzo 18:23, 25) Biblia pia inasema kwamba “Mungu hatendi uovu”; hawezi “kutenda kosa.”—Ayubu 34:10-12.

BIBLIA INASEMA NINI KUHUSU MATESO TUNAYOKABILI?

Mateso tunayokabili si adhabu ya Mungu kwa dhambi fulani tuliyofanya. Yesu aliweka jambo hilo wazi yeye na wanafunzi wake walipomwona mwanamume fulani aliyezaliwa kipofu. “Wanafunzi wake wakamuuliza: ‘Rabi, ni nani aliyetenda dhambi, ni mtu huyu au ni wazazi wake, hivi kwamba akazaliwa kipofu?’ Yesu akajibu: ‘Mtu huyu hakutenda dhambi wala wazazi wake.’”—Yohana 9:1-3.

Tunapofikiria maoni ya uwongo yaliyokuwa yameenea, inaelekea wanafunzi wa Yesu walishangaa sana alipowaambia kwamba ulemavu wa mwanamume huyo haukutokana na dhambi aliyofanya au ya wazazi wake. Yesu alimponya mwanamume huyo kipofu, na kwa kufanya hivyo, alirekebisha maoni ya uwongo kwamba mateso ni adhabu kutoka kwa Mungu. (Yohana 9:6, 7) Leo, wale walio na matatizo makubwa ya afya wanaweza kupata faraja kwa kujua kwamba Mungu hasababishi magumu wanayokabili.

Ikiwa Mungu alikuwa akiwaadhibu wagonjwa kwa sababu ya makosa yao, kwa nini Yesu aliwaponya?

Maandiko yanatuhakikishia kwamba . . .

  • “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (YAKOBO 1:13) Kwa kweli, “mambo maovu” ambayo yamewataabisha wanadamu kwa karne nyingi, kama vile magonjwa, maumivu, na kifo yatakomeshwa hivi karibuni.

  • Yesu Kristo ‘aliwaponya wote waliokuwa wakiteseka.’ (MATHAYO 8:16) Kwa kuwaponya wale wote waliokuja kwake, Mwana wa Mungu alionyesha mambo ambayo Ufalme wa Mungu utatimiza katika dunia yote.

  • “Naye [Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”​—UFUNUO 21:3-5.

NANI WA KULAUMIWA?

Hivyo basi, kwa nini wanadamu wamekuwa wakiteseka sana na kupata maumivu mengi? Swali hilo limewasumbua wanadamu kwa karne nyingi sana. Ikiwa si Mungu anayesababisha hali hizi, ni nani wa kulaumiwa? Majibu ya maswali hayo yanapatikana katika makala inayofuata.

^ fu. 4 Ingawa zamani Mungu aliwaadhibu watu fulani kwa sababu ya dhambi hususa walizofanya, Biblia haisemi popote kwamba leo Yehova anatumia magonjwa au majanga kuwaadhibu watu kwa sababu ya dhambi zao.