Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini andiko la Isaya 30:21, NW husema kwamba neno la Yehova linatoka “nyuma yako,” ilhali mstari unaotangulia ambao unasema “macho yako yatakuwa macho yanayomwona Mfundishaji Mkuu wako,” unaonyesha kwamba Yehova yuko mbele?

Andiko la Isaya 30:20, 21, NW husema: “Mfundishaji Mkuu wako hatajificha tena, na macho yako yatakuwa macho yanayomwona Mfundishaji Mkuu wako. Na masikio yako mwenyewe yatasikia neno nyuma yako likisema: ‘Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake,’ iwe mnapaswa kwenda upande wa kuume au iwe mnapaswa kwenda upande wa kushoto.”

Akichunguza andiko hilo kwa njia halisi, msomaji anamwona Yehova, Mfundishaji Mkuu, akiwa mbele yake lakini anasikia sauti Yake ikitoka nyuma. Hata hivyo, maneno hayo ni ya mfano, na yanapaswa kueleweka hivyo.

Usemi wa mfano ambao umetumiwa katika mstari wa 20 unafanya tuwazie mtumishi akimtumikia bwana wake, akiwa tayari daima kutekeleza maagizo ya bwana wake. Sawa na mtumishi anayetazama mkono wa bwana wake kwa makini ili afahamu mapenzi yake, watu wa Yehova leo wanaelekeza fikira zao kwa maagizo ya Biblia ambayo Yehova hutoa hatua kwa hatua kupitia tengenezo lake la kidunia. (Zaburi 123:1, 2) Naam, wanatekeleza maagizo yake, wakiwa macho kufanya lolote ambalo Yehova anasema kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mathayo 24:45-47.

Vipi neno ambalo watumishi wake husikia likitoka nyuma? Ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba sauti inayotoka nyuma ni sauti ya Mungu iliyosikika hapo kale ambayo iliandikwa katika Neno lake na kufafanuliwa na “msimamizi-nyumba mwaminifu.” (Luka 12:42) Watumishi wa Mungu wa sasa husikia sauti yake kwa kujifunza Biblia kwa bidii na kufuata kanuni zake maishani mwao kwa msaada wa vichapo vinavyotayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” “msimamizi-nyumba mwaminifu.” Kwa kutambua na kutegemea mwelekezo unaotolewa na Mfundishaji Mkuu kwa wakati unaofaa, na kwa kujifunza Neno la Mungu lililoandikwa karne nyingi zilizopita, watumishi wake humwona kwa njia ya mfano akiwa mbele yao na kusikia sauti yake kutoka nyuma.—Waroma 15:4.