Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIMULIZI LA MAISHA

Nilimpoteza Baba—Nikapata Baba

Nilimpoteza Baba—Nikapata Baba

BABA yangu alizaliwa huko Graz, Austria, mwaka wa 1899. Hivyo, alikuwa kijana wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Aliandikishwa katika jeshi la Ujerumani muda mfupi baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kuanza mwaka wa 1939. Aliuawa vitani nchini Urusi mwaka wa 1943. Inasikitisha kwamba hivyo ndivyo nilivyompoteza baba yangu nikiwa na umri wa miaka miwili hivi. Sikumjua vizuri, na nilitamani sana kuwa na baba, hasa nilipogundua kwamba karibu wavulana wote shuleni walikuwa na baba zao. Baadaye, nikiwa tineja, nilipata faraja nilipojifunza kumhusu Baba yetu wa mbinguni, Baba bora zaidi asiyeweza kufa.—Hab. 1:12.

MAISHA YANGU NIKIWA SKAUTI

Alipokuwa mvulana mdogo

Nilipokuwa na umri wa miaka saba, nilijiunga na kikundi cha Maskauti. Hilo ni shirika la ulimwenguni pote lililoanzishwa nchini Uingereza mwaka wa 1908 na Robert Stephenson Smyth Baden-Powell, aliyekuwa luteni mkuu katika jeshi la Uingereza. Katika mwaka wa 1916, alianzisha shirika la maskauti wenye umri mdogo lililoitwa Wolf Cubs au Cub Scouts.

Wakati wa mwisho-juma, nilifurahia kupiga kambi mashambani na Maskauti wenzangu, hasa kulala katika mahema, kuvaa sare, na kupiga gwaride. Nilipenda kuwa na Maskauti wenzangu na kuimba pamoja nao huku tukiota moto wakati wa jioni na kucheza msituni. Tulijifunza pia mambo mengi kuhusu vitu vya asili, jambo lililofanya nithamini kazi za Muumba wetu.

Maskauti hutiwa moyo kutenda jambo jema kila siku. Huo ndio wito wao. Tulisalimiana hivi: “Niko Tayari Daima.” Wito huo ulinivutia sana. Kikundi chetu kilikuwa na wavulana zaidi ya mia moja, karibu nusu yao walikuwa Wakatoliki, wengine Waprotestanti, na Mbudha mmoja.

Tangu mwaka wa 1920, Maskauti hufanya mikutano au sherehe za kimataifa baada ya kila miaka michache. Mnamo Agosti 1951, nilihudhuria Sherehe ya saba ya Maskauti Ulimwenguni huko Bad Ischl, Austria, na pia Sherehe ya tisa ya Maskauti Ulimwenguni katika Bustani ya Sutton, karibu na Birmingham, Uingereza, mnamo Agosti 1957. Maskauti 33,000 hivi kutoka nchi na maeneo 85 walihudhuria Sherehe hiyo ya tisa. Sherehe hiyo ilikuwa na wageni 750,000 hivi, kutia ndani Malkia Elizabeth wa Uingereza. Huo ulikuwa kama undugu wa ulimwenguni pote kwangu. Sikujua kwamba baada ya muda mfupi ningepata undugu bora zaidi, yaani, undugu wa kiroho.

NAKUTANA NA SHAHIDI WA YEHOVA KWA MARA YA KWANZA

Rudi Tschiggerl, mwokaji wa keki, ndiye aliyenihubiria kwanza

Kati ya mwezi wa Machi na Aprili, mwaka wa 1958, nilikuwa karibu kuhitimu nikiwa mhudumu wa hoteli katika Grand Hotel Wiesler huko Graz, Austria. Nikiwa huko, Rudolf Tschiggerl,  mfanyakazi mwenzangu aliyekuwa mwokaji wa keki, alinihubiria isivyo rasmi. Sikuwa nimesikia kamwe kuhusu kweli ya Biblia. Mwanzoni alizungumzia Utatu na kusema kwamba hilo si fundisho la Biblia. Nilitetea Utatu na nilitaka kumthibitishia kwamba alisema uwongo. Nilimpenda Rudolf na nilitaka kumshawishi arudi kwenye Kanisa Katoliki.

Rudolf, ambaye tulimwita Rudi, aliniletea Biblia. Nilisisitiza aniletee Biblia ya Kikatoliki. Nilianza kuisoma na ndani yake nilipata trakti iliyochapishwa na Watchtower Society. Rudi ndiye aliyeiweka humo. Sikutaka kuisoma kwa sababu nilihisi kwamba machapisho kama hayo huenda yana habari za uwongo zinazoonekana kuwa za kweli. Hata hivyo, nilikubali kuwa na mazungumzo ya Biblia pamoja naye. Kwa busara, Rudi aliamua kutonipa machapisho mengine. Kwa miezi mitatu hivi, tulizungumza mara kwa mara kuhusu Biblia hadi usiku.

Baada ya kumaliza mazoezi yangu katika hoteli ya mji wa nyumbani wa Graz, mama yangu alinipeleka kwenye chuo cha usimamizi wa hoteli ili niendelee na masomo. Kwa hiyo nilihamia Bad Hofgastein, mji ulio katika bonde la Milima ya Alps, ambako shule hiyo ilikuwa. Wasimamizi wa shule hiyo walishirikiana na wamiliki wa Grand Hotel huko Bad Hofgastein, na nyakati nyingine nilifanya kazi katika hoteli hiyo ili kupata uzoefu.

DADA WAWILI WAMISHONARI WANITEMBELEA

Ilse Unterdörfer na Elfriede Löhr walianza kunifundisha Biblia mwaka wa 1958

Rudi aliijulisha ofisi ya tawi ya Vienna anwani yangu mpya, na dada wawili wamishonari walipewa anwani hiyo, Ilse Unterdörfer na Elfriede Löhr. * Siku moja, mpokea-wageni katika hoteli hiyo alinipigia simu na kunijulisha kwamba wanawake wawili walikuwa wakiningojea kwenye gari na walitaka kuongea nami. Nilishangaa kwa sababu sikuwafahamu kamwe. Hata hivyo, nilienda kuwaona. Nilijua baadaye kwamba walikuwa Mashahidi waliosafirisha machapisho nchini Ujerumani siku za Wanazi wakati kazi ya Mashahidi ilipokuwa imepigwa marufuku kabla ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Hata kabla ya vita hivyo kuanza, walikuwa wamekamatwa na askari wa siri wa Ujerumani (Gestapo) na kupelekwa kwenye kambi ya mateso ya Lichtenburg. Kisha wakati wa vita, walipelekwa kwenye kambi nyingine huko Ravensbrück, karibu na Berlin.

Dada hao walikuwa wa rika la mama yangu, kwa hiyo niliwaheshimu. Ndiyo sababu sikutaka kupoteza muda wao kwa kuzungumza nao na kisha kukatiza mazungumzo hayo baada ya majuma au miezi kadhaa. Hivyo, niliwauliza ikiwa wangeweza kuniletea tu orodha ya maandiko kuhusu fundisho la Kikatoliki la urithi wa upapa. Niliwaambia kwamba nitazungumzia jambo hilo na kasisi wa eneo hilo. Nilifikiri hiyo ndiyo njia ya kujua ukweli.

NAJIFUNZA KUMHUSU BABA MTAKATIFU WA KWELI ALIYE MBINGUNI

Fundisho la Kanisa Katoliki kuhusu urithi wa upapa linadai kwamba kumekuwako na msururu usiokatizwa wa kupokezana upapa tangu wakati  wa mtume Petro. (Kanisa hilo linafafanua kimakosa maneno ya Yesu katika Mathayo 16:18, 19.) Wakatoliki wanadai pia kwamba papa hakosei anapofundisha mambo ya kidini akiwa katika mamlaka yake rasmi, yaani, ex cathedra. Niliamini jambo hilo na nilifikiri kwamba ikiwa papa, ambaye Wakatoliki wanamwita Baba Mtakatifu, hakosei anapofundisha mambo ya kidini na ikiwa amesema fundisho la Utatu ni la kweli, basi lazima liwe la kweli. Lakini ikiwa anakosea, huenda fundisho hilo ni la uwongo. Haishangazi kwamba fundisho la urithi wa upapa ndilo fundisho muhimu zaidi kwa Wakatoliki wengi, kwa kuwa huo ndio msingi wa kuamua ikiwa mafundisho ya Kikatoliki ni sahihi au si sahihi.

Nilipomtembelea kasisi, alishindwa kujibu maswali yangu, lakini alinipa kitabu cha mafundisho ya Wakatoliki kilichozungumzia fundisho la urithi wa upapa. Nilienda nacho nyumbani, nikakisoma, na niliporudi nilikuwa na maswali mengi zaidi. Mwishowe, kasisi huyo aliposhindwa kujibu maswali yangu aliniambia hivi: “Siwezi kukushawishi, wala wewe huwezi kunishawishi. . . . Nakutakia mema!” Hakutaka kuongea nami tena.

Sasa, nilikuwa tayari kujifunza Biblia pamoja na Ilse na Elfriede. Walinifunza mambo mengi kumhusu Baba Mtakatifu wa kweli aliye mbinguni, Yehova Mungu. (Yoh. 17:11) Wakati huo, hakukuwa na kutaniko katika eneo hilo, kwa hiyo dada hao wawili waliongoza mikutano katika nyumba ya familia fulani iliyopendezwa na kweli. Ni watu wachache tu waliohudhuria. Kwa kawaida dada hao wawili walifanya mikutano kwa njia ya mazungumzo kati yao kwa sababu hakukuwa na ndugu aliyebatizwa ambaye angeongoza. Mara kwa mara, ndugu kutoka eneo lingine alikuja kutoa hotuba katika chumba walichokodi.

NAANZA HUDUMA

Nilianza kujifunza Biblia na Ilse na Elfriede mnamo Oktoba 1958, nikabatizwa baada ya miezi mitatu mnamo Januari 1959. Kabla sijabatizwa, niliwauliza ikiwa ningeweza kuandamana nao nyumba kwa nyumba ili nione jinsi kazi ya kuhubiri ilivyofanywa. (Mdo. 20:20) Baada ya kuandamana nao kwa mara ya kwanza, niliwaomba eneo langu la kuhubiri. Walinipa kijiji fulani, na nilienda kuhubiri peke yangu nyumba kwa nyumba na kuwarudia waliopendezwa. Ndugu wa kwanza niliyehubiri naye nyumba kwa nyumba ni mwangalizi wa mzunguko aliyetutembelea.

Mwaka wa 1960, baada ya kumaliza masomo yangu ya kazi ya hoteli, nilirudi kwenye mji wa nyumbani ili nijaribu kuwasaidia watu wangu wa ukoo kujifunza kweli za Biblia. Hadi leo, hakuna hata mmoja aliyeikubali kweli lakini baadhi yao wanapendezwa kwa kiasi fulani.

MAISHA YA UTUMISHI WA WAKATI WOTE

Nilipokuwa na miaka 20 hivi, na nikiwa mvulana mdogo

Mwaka wa 1961, makutaniko yalisomewa barua kutoka kwenye ofisi ya tawi iliyowatia moyo wahubiri kuwa mapainia. Nilikuwa mseja mwenye afya nzuri, kwa hiyo sikuwa na sababu ya kutokuwa painia. Nilimuuliza mwangalizi wa mzunguko aliyeitwa Kurt Kuhn, ikiwa ingefaa nifanye kazi ya kimwili kwa miezi kadhaa ili ninunue gari ambalo lingenisaidia nikiwa painia. Aliniuliza hivi: “Je, Yesu na mitume walihitaji gari ili kuwa watumishi wa wakati wote?” Jibu hilo lilitosha! Nilipanga kuanza upainia haraka iwezekanavyo. Lakini kwa kuwa nilifanya kazi saa 72 kila juma hotelini, nilihitaji kufanya mabadiliko fulani kwanza.

Nilimwomba mwajiri wangu aniruhusu nifanye kazi saa 60. Alikubali ombi langu na kunilipa mshahara uleule. Muda mfupi baadaye,  nilimwomba aniruhusu kufanya kazi kwa saa 48 tu kila juma. Alikubali ombi hilo pia na kunilipa mshahara uleule. Kisha nikamwomba aniruhusu kufanya kazi saa 36 tu kila juma, yaani, saa 6 kwa siku 6, na alikubali ombi hilo pia. Inashangaza kwamba niliendelea kupokea mshahara uleule! Ilionekana kwamba mwajiri wangu hakutaka niache kazi. Ratiba hiyo iliniwezesha kuanza upainia wa kawaida. Mapainia walihitaji kuhubiri saa 100 kila mwezi wakati huo.

Miezi minne baadaye, niliwekwa rasmi kuwa painia wa pekee na mtumishi wa kutaniko dogo katika jimbo la Carinthia, mji wa Spittal an der Drau. Wakati huo, painia wa pekee alipaswa kuhubiri saa 150 kila mwezi. Sikutumwa pamoja na painia mwingine, lakini nilithamini sana msaada wa dada aitwaye Gertrude Lobner, aliyetumika akiwa msaidizi wa mtumishi wa kutaniko. *

NAPOKEA MIGAWO ZAIDI MIPYA

Mwaka wa 1963, nilipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko. Nyakati nyingine nilisafiri kwa garimoshi kutoka kutaniko moja hadi lingine, nikiwa nimebeba mizigo mizito. Ndugu wengi hawakuwa na gari, kwa hiyo hakuna mtu aliyekuja kunipokea katika kituo cha garimoshi. Ili isionekane kwamba “ninajionyesha,” niliamua kutokodi teksi, kwa hiyo nilitembea hadi mahali pa kulala.

Mwaka wa 1965, nikiwa bado mseja, nilialikwa kuhudhuria darasa la 41 la Shule ya Gileadi. Wengi wa wanadarasa wenzangu walikuwa waseja pia. Wakati wa kuhitimu, nilishangaa sana nilipopewa mgawo wa kurudi nyumbani Austria ili niendelee na kazi ya mzunguko. Hata hivyo, kabla sijaondoka Marekani, niliombwa niandamane na mwangalizi mwingine wa mzunguko kwa majuma manne. Nilithamini sana kufanya kazi pamoja na Anthony Conte, ndugu mpendwa ambaye pia alipenda utumishi wa shambani na alikuwa stadi sana. Tulitumika pamoja kaskazini mwa New York katika eneo la Cornwall.

Siku yetu ya harusi

Niliporudi Austria, nilipewa mgawo wa kuzungukia eneo fulani ambako nilikutana na Tove Merete, dada mseja mrembo. Alilelewa katika kweli tangu akiwa na umri wa miaka mitano. Ndugu wanapotuuliza jinsi tulivyokutana, sisi huwaambia hivi kwa utani: “Ofisi ya tawi ndiyo iliyofanya mipango hiyo.” Tulioana mwaka mmoja baadaye, mnamo Aprili 1967, na tuliruhusiwa kuendelea na kazi ya mzunguko pamoja.

Mwaka uliofuata, nilitambua kwamba kwa fadhili zake zisizostahiliwa, Yehova alinifanya kuwa mwana wake wa roho. Hivyo ndivyo ulivyoanza uhusiano wa pekee kati yangu na Baba yangu wa mbinguni, na pamoja na wale wote, ambao kulingana na andiko la Waroma 8:15, ‘wanapaaza sauti: “Abba, Baba!”’

Mimi na Merete tuliendelea kutumika pamoja katika kazi ya mzunguko na ya wilaya hadi mwaka wa 1976. Nyakati nyingine katika majira ya baridi kali, tulilazimika kulala katika vyumba vyenye baridi kali kupindukia visivyo na vipasha-joto. Siku moja tulipoamka, blanketi tulilojifunika lilikuwa jeupe na lilikuwa limeganda kwa sababu ya baridi kali! Hatimaye tuliamua kusafiri na  kipasha-joto kidogo cha umeme ili tuweze kuhimili baridi kali usiku. Katika maeneo mengine, tulitembea kwenye theluji kwenda msalani wakati wa usiku, kwa kawaida kilikuwa kibanda kibovu tu. Pia, hatukuwa na nyumba yetu, kwa hiyo siku ya Jumatatu tulibaki kwenye nyumba tuliyotumia katika juma la ziara. Kisha, Jumanne asubuhi tulienda katika kutaniko lililofuata.

Ninafurahi kusema kwamba mke wangu mpendwa amenitegemeza sana kwa miaka mingi. Anapenda sana utumishi wa shambani, na sihitaji kamwe kumhimiza kwenda kuhubiri. Anawapenda ndugu na dada na anawajali sana. Hilo limenisaidia sana.

Mwaka wa 1976, tulialikwa kwenda kutumikia kwenye ofisi ya tawi ya Austria iliyoko Vienna, na niliwekwa rasmi kuwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi. Wakati huo, ofisi ya tawi ya Austria ilisimamia kazi katika nchi nyingi za Ulaya Mashariki na ilifanya mipango ya kupeleka kwa siri machapisho katika nchi hizo. Ndugu Jürgen Rundel ndiye aliyesimamia mipango hiyo, na alitimiza mgawo wake vizuri. Nilipata pendeleo la kufanya kazi naye na baadaye niliombwa nisimamie kazi ya kutafsiri machapisho yetu katika lugha kumi za Ulaya Mashariki. Jürgen na mke wake, Gertrude, bado wanatumika kwa uaminifu wakiwa mapainia wa pekee nchini Ujerumani. Kuanzia mwaka wa 1978, ofisi ya tawi ya Austria ilianza kuchapisha magazeti katika lugha sita kwa kutumia mashine ndogo. Tulituma pia maandikisho ya magazeti katika nchi mbalimbali. Otto Kuglitsch, ambaye sasa anatumika pamoja na mke wake, Ingrid, kwenye ofisi ya tawi nchini Ujerumani, ndiye aliyesimamia kazi hiyo.

Nikiwa Austria, nilihubiri kwa njia mbalimbali, kama vile barabarani

Ndugu wa Ulaya Mashariki pia walichapisha vitabu na magazeti katika nchi zao wenyewe kwa kutumia mashine au mabamba ya kunakili. Hata hivyo, bado walihitaji machapisho zaidi kutoka nchi nyingine. Yehova alilinda kazi hiyo, na katika ofisi ya tawi, tuliwapenda akina ndugu waliofanya kazi hiyo kwa miaka mingi chini ya hali ngumu na marufuku.

ZIARA YA PEKEE HUKO ROMANIA

Mwaka wa 1989, nilipata pendeleo la kwenda Romania na Ndugu Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Kusudi la ziara hiyo lilikuwa kusaidia kikundi kikubwa cha ndugu kurudi katika tengenezo. Kuanzia mwaka wa 1949,  walijitenga na tengenezo kwa sababu mbalimbali na kuanzisha makutaniko yao wenyewe. Hata hivyo, waliendelea kuhubiri na kuwabatiza wapya. Walifungwa pia gerezani kwa sababu ya msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote, sawa tu na ndugu wengine waliokuwa katika tengenezo lililotambuliwa na makao makuu ya ulimwenguni pote. Bado kulikuwa na marufuku nchini Romania, kwa hiyo tulikutana nao kisiri katika nyumba ya Ndugu Pamfil Albu, pamoja na wazee wanne waliowaongoza na wawakilishi wa Halmashauri ya Nchi ya Romania. Tuliandamana pia na mkalimani kutoka Austria, Rolf Kellner.

Usiku wa pili wa mazungumzo yetu, Ndugu Albu aliwashawishi wazee wenzake wanne wakubali kuungana nasi aliposema hivi: “Tusipoungana sasa, huenda tusipate fursa nyingine ya kufanya hivyo.” Kwa hiyo, ndugu 5,000 hivi wakarudi katika tengenezo. Huo ulikuwa ushindi ulioje kwa Yehova na pigo kwa Shetani!

Mwishoni mwa mwaka wa 1989, kabla ya kuanguka kwa Ukomunisti huko Ulaya Mashariki, Baraza Linaloongoza lilinialika mimi na mke wangu kuhamia makao makuu ya ulimwenguni pote huko New York. Hatukutarajia jambo hilo kamwe. Tulianza kutumika katika Betheli ya Brooklyn mnamo Julai 1990. Mwaka wa 1992, niliwekwa rasmi kuwa msaidizi wa Halmashauri ya Utumishi ya Baraza Linaloongoza, na tangu Julai 1994, nimekuwa na pendeleo la kutumika katika Baraza Linaloongoza.

KUFIKIRIA WAKATI ULIOPITA NA KUKAZIA FIKIRA WAKATI UJAO

Nikiwa Brooklyn, New York, pamoja na mke wangu

Miaka mingi sana imepita tangu nilipokuwa mhudumu wa hoteli. Sasa ninafurahia pendeleo la kushiriki kutayarisha na kuandaa chakula cha kiroho kwa undugu wetu wa ulimwenguni pote. (Mt. 24:45-47) Nikifikiria miaka zaidi ya 50 ambayo nimetumika katika utumishi wa pekee wa wakati wote, ninafurahi na kuthamini sana baraka za Yehova juu ya undugu wetu wa ulimwenguni pote. Ninapenda kuhudhuria makusanyiko ya kimataifa, ambayo yanatuhimiza kujifunza kumhusu Baba yetu wa mbinguni, Yehova, na kweli ya Biblia.

Ninasali ili mamilioni zaidi wajifunze Biblia, waikubali kweli, na kumtumikia Yehova kwa umoja pamoja na undugu wetu wa Kikristo wa ulimwenguni pote. (1 Pet. 2:17) Pia, ninatazamia kwa hamu kuona nikiwa mbinguni wanadamu wakifufuliwa duniani, ili nimpate baba yangu mzazi. Ninatumaini kwamba baba, mama, pamoja na watu wangu wa ukoo wapendwa watakubali wote kumwabudu Yehova katika Paradiso.

Ninatazamia kwa hamu kuona nikiwa mbinguni wanadamu wakifufuliwa duniani, ili nimpate baba yangu mzazi

^ fu. 15 Tazama simulizi la maisha yao katika Mnara wa Mlinzi, Novemba 1, 1979, la Kiingereza.

^ fu. 27 Siku hizi, hakuna mtumishi wa kutaniko na msaidizi wake, badala yake kila baraza la wazee lina mratibu na mwandishi.