Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Vibaya Kubadili Uamuzi Wako?

Je, Ni Vibaya Kubadili Uamuzi Wako?

VIJANA fulani Wakristo wameamua kwenda kutazama sinema. Walisikia kwamba wanafunzi wenzao walifurahia sana sinema hiyo. Wanapofika kwenye ukumbi wa sinema, wanaona mabango yenye picha za silaha hatari na wanawake waliovalia nusu uchi. Wafanye nini sasa? Je, waingie ukumbini na kutazama sinema hiyo?

Mfano huo unaonyesha kwamba tunakabili maamuzi ambayo yanaweza ama kuharibu au kuboresha hali yetu ya kiroho na uhusiano wetu na Yehova. Nyakati nyingine, huenda ukataka kufanya jambo fulani lakini baada ya kuchanganua tena hali, unabadili uamuzi wako. Je, kufanya hivyo kunaonyesha kwamba huna msimamo, au huenda umefanya uamuzi unaofaa?

Wakati Ambapo Haifai Kubadili Uamuzi Wako

Upendo wetu kwa Yehova ulituchochea kujiweka wakfu kwake na kubatizwa. Tumeazimia kutoka moyoni kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu. Hata hivyo, adui yetu Shetani Ibilisi ameazimia kuvunja utimilifu wetu. (Ufu. 12:17) Tumeamua kumtumikia Yehova na kushika amri zake. Ingesikitisha kama nini ikiwa tungebadili uamuzi tuliofanya wa kujiweka wakfu kwa Yehova! Hilo linaweza kufanya tupoteze uhai wetu.

Zaidi ya karne 26 zilizopita, Mfalme Nebukadneza wa Babiloni alisimamisha sanamu kubwa ya dhahabu na kuwaamuru watu wote waiinamie na kuiabudu. Mtu yeyote ambaye angekataa kuiabudu angetupwa katika tanuru ya moto. Waabudu watatu wa Yehova—Shadraki, Meshaki, na Abednego—walikataa kuiinamia sanamu hiyo. Kwa sababu hiyo walitupwa katika tanuru ya moto. Waliokolewa kimuujiza na Yehova, lakini walikuwa tayari kufa badala ya kulegeza uamuzi wao wa kumtumikia Mungu.—Dan. 3:1-27.

 Baadaye, nabii Danieli alidumu katika sala, licha ya kutishwa kutupwa katika tundu la simba. Aliendelea na zoea lake la kusali kwa Yehova mara tatu kwa siku. Danieli hakubadili uamuzi wake wa kumwabudu Mungu wa kweli. Kwa sababu hiyo, nabii huyo aliokolewa “kutoka katika makucha ya simba.”—Dan. 6:1-27.

Watumishi wa Mungu leo huishi pia kupatana na wakfu wao kwake. Katika shule moja barani Afrika, kikundi cha wanafunzi ambao ni Mashahidi wa Yehova kilikataa kushiriki katika sherehe ya kuabudu bendera ya taifa. Walitishwa kufukuzwa shuleni ikiwa wangekataa kushiriki katika sherehe hiyo pamoja na wanafunzi wengine. Muda mfupi baadaye, waziri wa elimu alitembelea mji huo na kuzungumza na baadhi ya wanafunzi hao Mashahidi. Kwa heshima na ujasiri, vijana hao Mashahidi walimweleza msimamo wao. Tangu wakati huo, suala hilo halijatokea tena. Sasa ndugu na dada zetu vijana hawashinikizwi walegeze msimamo wao wa kumtumikia Yehova.

Fikiria pia kisa cha Joseph, ambaye mke wake alikufa ghafla baada ya kuugua kansa. Familia ya Joseph ilielewa na kuheshimu msimamo wake kuhusu desturi za mazishi. Hata hivyo, familia ya mke wake si Mashahidi na walitaka desturi fulani za mazishi zifanywe, kutia ndani desturi ambazo hazimpendezi Mungu. Joseph anasema hivi: “Nilipokataa kulegeza msimamo wangu, walijaribu kuwashawishi watoto wangu, lakini walibaki imara. Watu hao wa ukoo walijaribu pia kupanga kukesha nyumbani kwangu kama ilivyo desturi, lakini niliwaambia kwamba wakisisitiza kukesha, basi hawatafanya hivyo nyumbani kwangu. Walijua kwamba desturi ya kukesha haipatani na imani yangu wala imani aliyokuwa nayo mke wangu, basi baada ya mazungumzo marefu walienda kukesha kwingineko.

“Katika kipindi hicho kigumu cha kuomboleza, nilimsihi Yehova anisaidie ili familia yetu isivunje sheria zake. Alisikiliza sala zangu na kutusaidia kubaki imara licha ya kushinikizwa.” Joseph na watoto wake walikuwa wameazimia kutobadili kamwe msimamo wao kuhusu ibada.

Wakati Ambapo Huenda Ikafaa Kubadili Uamuzi Wako

Muda mfupi tu baada ya Pasaka ya 32 W.K., mwanamke wa taifa la Sirofoinike alimwendea Yesu Kristo katika eneo la Sidoni. Alimwomba tena na tena amfukuze roho mwovu kutoka katika binti yake. Mwanzoni, Yesu hakumjibu neno lolote. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Sikutumwa kwa wowote ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” Alipoendelea kumsihi, Yesu alisema hivi: “Si sawa kuuchukua mkate wa watoto na kuwatupia mbwa wadogo.” Akionyesha kwamba ana imani kubwa, mwanamke huyo alijibu: “Ndiyo, Bwana; lakini kwa kweli hao mbwa wadogo hula sehemu ya makombo yanayoanguka kutoka kwenye meza ya mabwana zao.” Yesu alikubali ombi lake na kumponya binti yake.—Mt. 15:21-28.

Kwa kufanya hivyo, Yesu alikuwa akimwiga Yehova kwa kuwa tayari kubadili uamuzi wake hali zikiruhusu. Kwa mfano, Mungu alikusudia kuwaangamiza Waisraeli walipotengeneza ndama wa dhahabu, lakini alikubali Musa amsihi abadili uamuzi Wake.—Kut. 32:7-14.

Mtume Paulo alimwiga Yehova na Yesu. Kwa muda fulani, Paulo alihisi kwamba haingefaa kwenda na Yohana Marko katika safari zake za umishonari kwa kuwa alimwacha yeye na Barnaba wakati wa safari yao ya kwanza ya umishonari. Hata hivyo, baadaye Paulo alitambua kwamba Marko alikuwa amebadili mtazamo wake na angemfaa sana. Kwa hiyo Paulo alimwambia hivi Timotheo: “Umchukue Marko na uje  pamoja naye, kwa maana yeye ni mwenye faida kwangu kwa ajili ya huduma.”—2 Tim. 4:11.

Namna gani sisi? Ili tumwige Baba yetu wa mbinguni mwenye rehema, subira, na upendo, huenda ikafaa tubadili mtazamo wetu. Kwa mfano, huenda tukabadili maoni yetu kuhusu watu wengine. Lakini, tofauti na Yehova na Yesu, sisi si wakamilifu. Ikiwa Yehova na Yesu walikuwa tayari kubadili maoni yao, je, hatupaswi kubadili maoni yetu tunapofikiria hali za wengine?

Huenda ikafaa kubadili maoni yetu tunapofikiria miradi ya kiroho. Baadhi ya watu wanaojifunza Biblia na ambao kwa muda fulani wamekuwa wakihudhuria mikutano ya kutaniko huenda wakasita kubatizwa. Au huenda ndugu fulani wakasita kufanya upainia, hata ingawa wanaweza kupanua utumishi wao kwa njia hiyo. Na huenda ndugu wengine wakasita kujitahidi kufikia mapendeleo kutanikoni. (1 Tim. 3:1) Je, wewe ni kati ya watu wanaosita kufanya baadhi ya mambo yaliyotajwa? Kwa upendo, Yehova anakualika ufikie mapendeleo hayo. Kwa hiyo basi, mbona usibadili mtazamo wako na kupata shangwe ya kujitoa kumtumikia Mungu na watu wengine?

Unaweza kupata baraka ukibadili uamuzi wako

Ella anayetumika katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova barani Afrika anasema hivi: “Nilipokuja Betheli, sikujua ningekaa kwa muda mrefu. Nilitamani kumtumikia Yehova kwa nafsi yote, lakini pia niliipenda sana familia yetu. Mwanzoni, niliwakosa sana! Hata hivyo, dada niliyeishi naye alinitia moyo, nikaamua kuendelea kutumika Betheli. Baada ya kutumika Betheli kwa miaka kumi, ninahisi kwamba ninataka kuendelea kuwatumikia ndugu na dada zangu kwa muda mrefu iwezekanavyo.”

 Wakati Ambapo Ni Lazima Ubadili Uamuzi Wako

Je, unakumbuka kilichompata Kaini alipomwonea wivu ndugu yake na kuwaka hasira? Mungu alimwambia mwanamume huyo aliyekasirika kwamba angepata kibali chake ikiwa angegeuka na kutenda mema. Mungu alimshauri Kaini ashinde dhambi ‘iliyokuwa ikivizia katika mwingilio.’ Kaini angeweza kubadili mtazamo na uamuzi wake, lakini aliamua kupuuza shauri la Mungu. Kwa kusikitisha, Kaini alimuua ndugu yake na akawa mwanadamu wa kwanza kumuua mwenzake!—Mwa. 4:2-8.

Mambo yangekuwaje ikiwa Kaini angebadili uamuzi wake?

Fikiria pia mfano wa Mfalme Uzia. Mwanzoni, alifanya yaliyo sawa machoni pa Yehova na aliendelea kumtafuta Mungu. Hata hivyo, inasikitisha kwamba Uzia aliharibu sifa yake nzuri kwa kuwa na kiburi. Aliingia hekaluni kufukiza uvumba ingawa hakuwa kuhani. Makuhani walipomwonya asitende hivyo kwa kimbelembele, je, alibadili uamuzi wake? Hapana. Uzia “akawa na ghadhabu” na kupuuza onyo lao. Yehova alimpiga kwa ukoma.—2 Nya. 26:3-5, 16-20.

Naam, kuna pindi ambapo ni lazima tubadili uamuzi wetu. Mfano wa ndugu anayeitwa Joachim unaonyesha hilo. Alibatizwa mwaka wa 1955, lakini alitengwa na ushirika katika mwaka wa 1978. Miaka 20 baadaye, alitubu na kuwa tena Shahidi wa Yehova. Hivi karibuni, mzee mmoja alimuuliza ni kwa nini alichukua muda mrefu sana kuomba arudishwe. Joachim alijibu hivi: “Nilikuwa na hasira na kiburi. Ninajuta kwamba nilichukua muda mrefu hivyo. Ingawa nilikuwa nimetengwa na ushirika, nilijua kwamba Mashahidi wa Yehova wanafundisha kweli.” Alihitaji kubadili mtazamo wake na kutubu.

Huenda tukakabili hali ambayo itatulazimu kubadili uamuzi wetu na njia zetu. Na tuwe tayari kufanya hivyo ili tumpendeze Yehova.—Zab. 34:8.