Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Alijifunza Kutokana na Makosa Yake

Alijifunza Kutokana na Makosa Yake

Igeni Imani Yao

Alijifunza Kutokana na Makosa Yake

YONA alitamani kuziba masikio yake asisikie sauti hizo mbaya. Hazikuwa tu sauti za pepo kali zilizokuwa zikiipiga meli; wala hazikuwa sauti za mawimbi makubwa yaliyokuwa yakiipiga na kufanya mbao zake zipige kelele kana kwamba zitavunjika. Sauti zilizomhuzunisha Yona ni kelele za kapteni na wafanyakazi wake walipojitahidi kufanya meli iendelee kuelea. Yona alikuwa na hakika kwamba watu hao walikuwa karibu kufa, na yeye ndiye angelaumiwa!

Yona alijipata jinsi gani katika hali hiyo ya kuhuzunisha? Alikuwa amemkosea sana Mungu wake, Yehova. Alikuwa amefanya nini? Je, angeweza kurekebisha hali hiyo? Majibu ya maswali hayo yanaweza kutufundisha mambo mengi. Kwa mfano, kisa cha Yona kinaweza kutusaidia kuona kwamba hata wale walio na imani ya kweli wanaweza kukosea na jinsi wanavyoweza kufanya marekebisho.

Nabii Kutoka Galilaya

Watu wanapofikiri kumhusu Yona, mara nyingi wao wanakazia fikira tu kuhusu sifa zake mbaya kama vile kutokutii au kichwa chake kigumu. Lakini kuna mambo mengi zaidi tunayoweza kujifunza kutoka kwake. Kumbuka kwamba Yona alikuwa amechaguliwa kutumika akiwa nabii wa Yehova Mungu. Yehova hangempa pendeleo hilo kubwa ikiwa hakuwa mwaminifu au mwadilifu.

Katika andiko la 2 Wafalme 14:25, tunajifunza mambo fulani kuhusu malezi ya Yona. Alitoka Gath-heferi, uliokuwa kilomita nne tu kutoka Nazareti, mji ambako Yesu angelelewa miaka 800 hivi baadaye. * Yona alitumika akiwa nabii wakati wa utawala wa Mfalme Yeroboamu wa Pili wa ufalme wa Israeli wa makabila kumi. Siku za Eliya zilikuwa zimepita; nabii aliyemfuata, Elisha, alikufa wakati wa utawala wa baba ya Yeroboamu. Ingawa Yehova alikuwa amewatumia manabii hao kuondoa ibada ya Baali, kwa mara nyingine tena Israeli ilikuwa imeanza kuasi. Nchi ilikuwa chini ya mfalme ambaye ‘aliendelea kutenda yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova.’ (2 Wafalme 14:24) Hivyo, kazi ya Yona haingekuwa rahisi au yenye kufurahisha. Hata hivyo, aliifanya kwa uaminifu.

Siku moja maisha ya Yona yalibadilika ghafula. Alipata mgawo kutoka kwa Yehova ambao aliuona kuwa mgumu sana. Yehova alikuwa akimwomba afanye nini?

“Ondoka, Uende Ninawi”

Yehova alimwambia Yona: “Ondoka, uende Ninawi lile jiji kubwa, ukalitangazie kwamba ubaya wao umefika mbele zangu.” (Yona 1:2) Si vigumu kuona ni kwa nini mgawo huo ulionekana kuwa mgumu. Ninawi lilikuwa kilomita 800 hivi upande wa mashariki, safari ambayo ingechukua muda wa mwezi mmoja kwa kutembea. Hata hivyo, safari hiyo ngumu ilikuwa rahisi ikilinganishwa na kazi ambayo angefanya. Huko Ninawi, Yona alipaswa kutoa ujumbe wa hukumu ya Yehova kwa Waashuru ambao walikuwa wajeuri na wakatili sana. Ikiwa ni watu wachache sana kati ya watu wa Mungu waliomsikiliza Yona, je, kulikuwa na tumaini lolote kwamba angesikilizwa na wapagani hao? Mtumishi mmoja wa Yehova angefaulu jinsi gani katika jiji hilo kubwa la Ninawi, ambalo lingekuja kuitwa “jiji la umwagaji wa damu”?—Nahumu 3:1, 7.

Huenda Yona alifikiria mambo kama hayo lakini hatuwezi kujua. Tunachojua ni kwamba alikimbia mgawo wake. Yehova alimwelekeza aende upande wa mashariki; Yona alielekea upande wa magharibi, na alijaribu kwenda mbali kadiri ambavyo angeweza. Alienda pwani, kwenye jiji la bandarini la Yopa, ambako alipata meli iliyokuwa ikielekea Tarshishi. Wasomi fulani wanasema kwamba Tarshishi ilikuwa huko Hispania. Ikiwa ndivyo, basi Yona alikuwa akielekea kilomita 3,500 hivi kutoka Ninawi. Safari kama hiyo ya kwenda mwisho wa Bahari Kuu, kama Bahari ya Mediterania ilivyoitwa nyakati hizo, ingechukua mwaka mmoja hivi! Yona alikuwa ameazimia kutoroka mgawo ambao Yehova alikuwa amempa!

Je, hilo linamaanisha kwamba Yona alikuwa mwoga? Hatupaswi kumhukumu haraka. Kama tutakavyoona, alikuwa na ujasiri mkubwa. Lakini, kama sisi sote, Yona hakuwa mkamilifu na alikosea mara nyingi. (Zaburi 51:5) Ni nani kati yetu ambaye hajawahi kuwa na woga?

Huenda ikaonekana kwamba nyakati nyingine Mungu anatuomba tufanye jambo tunaloona kuwa gumu, au hata lisilowezekana. Huenda hata tukaona kuwa ni vigumu kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, kama Wakristo wanavyoamriwa wafanye. (Mathayo 24:14) Ni rahisi sana kusahau ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Mambo yote yanawezekana kwa Mungu.” (Marko 10:27) Huenda tukaelewa ugumu ambao Yona alikabili ikiwa nyakati nyingine sisi tunasahau ukweli huo. Hata hivyo, Yona alipatwa na nini alipokuwa akitoroka?

Yehova Amtia Nidhamu Nabii Wake Mwasi

Tunaweza kumwazia Yona akitafuta mahali pa kuketi katika meli hiyo ambayo huenda ilikuwa meli ya mizigo ya Wafoinike. Alimwona kapteni pamoja na wafanyakazi wa meli hiyo wakiwa na shughuli nyingi za kuiondoa meli bandarini. Kadiri walivyosonga mbali kutoka pwani, huenda ikawa Yona alidhani anahepa hatari aliyoiogopa sana. Lakini ghafula hali ya hewa ikabadilika.

Pepo zenye nguvu ziliichafua sana bahari kwani mawimbi yaliyokuwa yakipiga yangeweza kuifunika meli ya kisasa. Ilichukua muda gani kwa meli hiyo iliyotengenezwa kwa mbao kuonekana kuwa ndogo na dhaifu, ikiwa imepotea katika mawimbi makubwa sana? Je, wakati huo Yona alijua kile alichoandika baadaye kwamba “Yehova mwenyewe akavumisha upepo mkubwa baharini”? Ni vigumu kusema. Hata hivyo, aliona kwamba mabaharia walianza kuililia miungu yao mbalimbali, na alijua kwamba hawangepata msaada wowote. Simulizi lake linasema: “Nayo meli ikawa karibu kuvunjika.” (Yona 1:4; Mambo ya Walawi 19:4) Naye Yona angesali namna gani kwa Mungu aliyekuwa akimtoroka?

Huku akihisi kuwa hana uwezo wa kusaidia, Yona alienda chini kwenye sehemu za ndani kabisa za meli hiyo na kupata mahali pa kulala. Akalala fofofo. * Kapteni alimpata Yona, akamwamsha, na kumsihi amwombe mungu wake, kama kila mtu alivyokuwa akifanya. Wakiwa na hakika kwamba hiyo haikuwa dhoruba ya kawaida, mabaharia walipiga kura ili kuona ni nani aliyekuwa amewaingiza taabani. Haikosi Yona alizidi kuwa na wasiwasi kadiri mtu mmoja baada ya mwingine alivyoondolewa kupitia kura. Baada ya muda ukweli ukaonekana. Yehova alikuwa akielekeza dhoruba, kutia ndani kura yenyewe, imwangukie mtu mmoja—Yona!—Yona 1:5-7.

Yona aliwafunulia mabaharia kila kitu. Alikuwa mtumishi wa Mungu Mweza-Yote, Yehova. Huyu ndiye Mungu aliyekuwa akimtoroka na alikuwa amemkosea, na hivyo akawaingiza wote hatarini. Mabaharia hao walishtuka sana na Yona angeweza kuona kwamba walijawa na hofu. Walimwuliza wamfanye nini ili kuokoa meli hiyo na uhai wao. Alisema nini? Huenda ikawa Yona alijawa na hofu alipofikiria jinsi ambavyo angezama katika bahari hiyo baridi na iliyochafuka. Lakini angeweza namna gani kuwaacha wanaume hao wote wafe huku akijua angeweza kuwaokoa? Kwa hiyo akasema: “Mninyanyue na kunitupa baharini, nayo bahari itatulia kwa ajili yenu; kwa maana najua kwamba ni kwa sababu yangu tufani hii kubwa imewajia.”—Yona 1:12.

Hayo si maneno ya mtu mwoga, sivyo? Lazima moyo wa Yehova uwe ulijawa na furaha kuona ujasiri wa Yona na roho yake ya kujidhabihu katika pindi hiyo ngumu. Kisa hicho kinatuonyesha imani yenye nguvu ya Yona. Leo tunaweza kumwiga kwa kutanguliza mahitaji ya wengine. (Yohana 13:34, 35) Tunapomwona mtu mwenye uhitaji, iwe ni kimwili, kihisia, au kiroho, je, tunajitolea kumsaidia? Tunampendeza Yehova kama nini tunapofanya hivyo!

Huenda mabaharia waliguswa sana na tendo hilo kwa kuwa mwanzoni walikataa kufanya kama Yona alivyowaambia! Badala yake, walifanya juu chini ili wapenye dhoruba hiyo, lakini hawakufua dafu. Tufani hiyo ilizidi kuwa mbaya. Mwishowe, waliona kwamba hawakuwa na la kufanya. Huku wakimwomba, Yehova, Mungu wa Yona, awaonyeshe rehema, walimnyanyua Yona na kumtupa baharini.—Yona 1:13-15.

Yona Aonyeshwa Rehema na Kuokolewa

Yona alitumbukia katika mawimbi yaliyokuwa yakivuma. Labda aling’ang’ana kuelea, na kati ya mawimbi hayo makubwa aliiona meli ikiondoka kasi. Lakini mawimbi hayo makubwa yalimsukuma chini ya maji. Alizidi kuzama akihisi hana tumaini kabisa.

Baadaye Yona alieleza jinsi alivyohisi wakati huo. Mawazo mengi yalimjia akilini. Huku akiwa na huzuni aliwaza kwamba hangeliona tena hekalu maridadi la Yehova huko Yerusalemu. Alijihisi akizama kwenye vilindi vya bahari, karibu na sehemu za chini kabisa za milima, ambako magugu yalimnasa. Hilo lilionekana kuwa shimo lake, au kaburi lake.—Yona 2:2-6.

Lakini ngoja kidogo! Aliona kitu kikisonga karibu naye, kitu kikubwa, cheusi, kilicho hai. Kilizidi kumkaribia. Mdomo mkubwa ulifunguka na kummeza!

Huu ndio mwisho. Hata hivyo, Yona alishangazwa na jambo moja. Bado alikuwa hai! Hakuwa amevunjwa-vunjwa, wala kumeng’enywa, wala kusongwa pumzi. Ingawa ni kana kwamba alikuwa katika kaburi lake, bado alikuwa hai. Pole kwa pole, Yona alijawa na woga wenye heshima. Bila shaka, ni Mungu wake, Yehova, ‘aliyemweka samaki mkubwa ammeze Yona.’ *Yona 1:17.

Dakika zilizidi kupita. Akiwa humo, katika giza kubwa zaidi ambalo amewahi kuona, Yona alipata nafasi ya kutafakari na kusali kwa Yehova Mungu. Sala yake, ambayo yote imerekodiwa katika sura ya pili ya Yona, inafunua mambo mengi. Inaonyesha kwamba Yona alikuwa na ujuzi mwingi wa Maandiko, kwa sababu inarejelea Zaburi mara nyingi. Pia, inaonyesha sifa fulani nzuri ya Yona: alikuwa mwenye shukrani. Yona alimalizia sala yake hivi: “Lakini mimi, kwa sauti ya kutoa shukrani nitakutolea dhabihu. Nilichoweka nadhiri, nitakitimiza. Wokovu ni wa Yehova.”—Yona 2:9.

Yona alijifunza kwamba Yehova anaweza kumwokoa mtu yeyote, mahali popote, wakati wowote. Hata humo, “ndani ya tumbo la samaki huyo,” Yehova alimpata na kumwokoa mtumishi wake aliyekuwa taabani. (Yona 1:17) Ni Yehova peke yake ambaye angeweza kumhifadhi mtu hai kwa siku tatu mchana na usiku ndani ya tumbo la samaki mkubwa. Leo, tunafaa kukumbuka kwamba ‘pumzi yetu imo mkononi mwa’ Yehova Mungu. (Danieli 5:23) Tuko hai kwa sababu ya mapenzi yake. Je, tunaonyesha kwamba tunashukuru? Basi, je, hatupaswi kumtii Yehova?

Namna gani Yona? Je, alijifunza kumwonyesha Yehova shukrani kwa kumtii? Ndiyo. Baada ya kukaa siku tatu mchana na usiku, samaki huyo alimpeleka Yona hadi ufuoni na “akamtapika Yona kwenye nchi kavu.” (Yona 2:10) Hebu fikiria—baada ya kupitia mambo hayo yote, Yona hakuhitaji hata kuogelea! Bila shaka, alihitaji kutafuta njia ya kutoka ufuo huo ambao samaki alimwacha. Hata hivyo, baada ya muda mfupi roho yake ya kuonyesha shukrani ilijaribiwa. Yona 3:1, 2 inasema: “Ndipo neno la Yehova likamjia Yona mara ya pili, na kusema: ‘Ondoka, uende Ninawi lile jiji kubwa, ukalitangazie neno ninalokuambia.’” Yona angefanya nini?

Yona hakusitasita. Tunasoma hivi: “Basi Yona akasimama na kwenda Ninawi kulingana na neno la Yehova.” (Yona 3:3) Ndiyo, alitii. Ni wazi kwamba alijifunza kutokana na makosa aliyofanya. Sisi pia tunapaswa kumwiga Yona katika njia hiyo. Sisi sote tunafanya dhambi; sisi sote tunafanya makosa. (Waroma 3:23) Je, tunakata tamaa, au tunajifunza kutokana na makosa yetu na kuanza kutenda kwa njia inayoonyesha tunamtii Mungu kwa kumtumikia?

Je, Yehova alimthawabisha Yona kwa utii wake? Bila shaka alifanya hivyo. Inaonekana kwamba Yona aligundua baadaye kuwa wale mabaharia waliokoka. Dhoruba ilitulia mara moja baada ya Yona kujidhabihu, na mabaharia hao “wakaanza kumwogopa sana Yehova” na wakamtolea dhabihu badala ya kuitolea miungu yao ya uwongo.—Yona 1:15, 16.

Thawabu nyingine kubwa ilikuja baadaye. Yesu alifananisha kwa njia ya kinabii wakati ambao Yona alikuwa ndani ya samaki huyo mkubwa na muda ambao angekuwa kaburini, au Sheoli. (Mathayo 12:38-40) Yona atafurahi kama nini kujua kuhusu baraka hiyo atakapofufuliwa aishi duniani! (Yohana 5:28, 29) Yehova anataka kukubariki pia. Kama Yona, je, utajifunza kutokana na makosa yako na kuonyesha roho ya utii na ya kujidhabihu?

[Maelezo ya chini]

^ fu. 7 Ni muhimu kujua kwamba Yona alitoka Galilaya kwa sababu Mafarisayo walisema hivi kwa kiburi kumhusu Yesu: “Chunguza uone kwamba hakuna nabii atakayeinuliwa kutoka Galilaya.” (Yohana 7:52) Watafsiri na wachunguzi wengi wamedokeza kwamba Mafarisayo walikuwa wakizungumza kwa ujumla kwamba hakuna nabii aliyewahi au atakayewahi kutoka mji wa hali ya chini wa Galilaya. Ikiwa ndivyo, walipuuza historia na pia unabii.—Isaya 9:1, 2.

^ fu. 17 Tafsiri ya Septuajinti inakazia jinsi Yona alivyolala fofofo kwa kusema kwamba alikuwa akikoroma. Hata hivyo, badala ya kuona usingizi wa Yona kuwa ishara ya kutojali, tunapaswa kukumbuka kwamba nyakati fulani watu walioshuka moyo wanapatwa na usingizi. Yesu alipokuwa na uchungu mwingi katika bustani ya Gethsemane, Petro, Yakobo, na Yohana walikuwa “wakisinzia kwa huzuni.”—Luka 22:45.

^ fu. 25 Neno la Kiebrania “samaki,” lilitafsiriwa katika Kigiriki kuwa “mnyama mkubwa wa baharini,” au “samaki mkubwa.” Ingawa hakuna njia ya kuthibitisha ni kiumbe gani wa baharini anayetajwa, imegunduliwa kwamba katika Bahari ya Mediterania kuna papa wakubwa wanaoweza kummeza mtu mzima. Kuna papa wakubwa zaidi katika maeneo mengine. Kwa mfano, papa-nyangumi anaweza kukua kufikia urefu wa mita 15 au zaidi!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 29]

Kitabu cha Yona Kinachambuliwa

▪ Je, kweli mambo yanayosimuliwa katika kitabu cha Biblia cha Yona yalitukia? Tangu zamani, kitabu hicho kimechambuliwa sana. Katika nyakati za kisasa ambapo kuna wahakiki wa Biblia, mara nyingi kitabu hicho kimesemwa kuwa ni ngano, hekaya, au hadithi ya kubuniwa tu. Mwandishi mmoja wa karne ya 19 aliripoti jinsi kasisi fulani alivyoeleza simulizi la Yona na yule samaki mkubwa kuwa aina fulani ya sitiari: Eti Yona aliishi katika hoteli huko Yopa inayoitwa Nyangumi. Alipokosa pesa za kulipa kodi, mwenye hoteli alimfukuza. Hivyo kwa njia ya mfano Yona ‘alimezwa na’ nyangumi na baadaye “akamtapika!” Inaonekana kwamba wachambuzi wa Biblia wameazimia kummeza Yona zaidi kuliko samaki yule mkubwa!

Kwa nini kitabu hiki cha Biblia kinachambuliwa sana? Kinataja kuhusu miujiza. Inaonekana, wachambuzi wengi wameshikilia maoni yasiyofaa kwamba miujiza haiwezi kutendeka. Lakini je, mtazamo huo unapatana na akili? Jiulize hivi, ‘Je, ninaamini sentensi ya kwanza ya Biblia?’ Inasema hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wenye kukubali sababu hawapingi ukweli huo. Kwa njia fulani, sentensi hiyo peke yake inatia ndani mambo mengi zaidi kuliko miujiza yoyote inayofafanuliwa baadaye katika Biblia.

Fikiria hili: Kitabu cha Yona kina nini ambacho Yule aliyeumba mbingu na maajabu yote duniani hawezi kufanya? Je, hawezi kutokeza dhoruba? Kufanya samaki mkubwa ammeze mtu? Au kumfanya samaki huyohuyo amtapike mtu huyo? Kwa Yule aliye na nguvu zisizo na mipaka, mambo kama hayo si magumu hata kidogo.—Isaya 40:26.

Hata bila Mungu kuingilia kati, nyakati nyingine mambo ya ajabu yanatokea. Kwa mfano, inasemekana kwamba mnamo 1758, baharia mmoja alianguka ndani ya Bahari ya Mediterania kutoka melini na akamezwa na papa. Hata hivyo, papa huyo alipigwa kwa mzinga. Papa huyo alimtema baharia huyo na akaokolewa akiwa hai bila majeraha makubwa. Ikiwa kwa kweli jambo hilo lilitendeka, tunaweza kusema hilo lilikuwa jambo la ajabu, au hata la kustaajabisha, lakini si muujiza. Je, Mungu hangaliweza kutumia nguvu zake kufanya mambo makubwa hata zaidi?

Pia, wachambuzi wanasema kwamba hakuna mtu anayeweza kuendelea kuwa hai ndani ya samaki kwa siku tatu bila kusongwa pumzi. Hata hivyo, wanadamu wametumia akili sana hivi kwamba wamegundua jinsi ya kujaza hewa iliyoshindiliwa ndani ya matangi na kuitumia kupumua chini ya maji kwa muda mrefu. Je, Mungu hangaliweza kutumia nguvu na hekima yake isiyo na kifani ili kuhakikisha Yona anaendelea kuwa hai na kupumua kwa siku tatu? Kama tu malaika wa Yehova alivyomwambia Maria, mama ya Yesu, “kwa Mungu hakuna tangazo lolote lisilowezekana.”—Luka 1:37.

Ni nini kingine kinachoonyesha kwamba kitabu cha Yona ni sahihi kihistoria? Yona anatoa ufafanuzi wa wazi na ulio halisi kuhusu meli na mabaharia wake. Kwenye Yona 1:5, tunaona kwamba mabaharia walitupa vitu kutoka melini ili kupunguza uzito wake. Wanahistoria wa kale na sheria ya kirabi zinaonyesha kuwa hilo lilikuwa zoea la kawaida bahari ilipochafuka. Pia, ufafanuzi wa baadaye wa Yona kuhusu Ninawi unapatana na uthibitisho wa kihistoria na wa vitu vya kale vilivyochimbuliwa. Hata hivyo, jambo kuu zaidi ya yote ni kwamba Yesu Kristo alifananisha kwa njia ya kinabii zile siku tatu ambazo Yona alikuwa ndani ya samaki mkubwa na muda ambao Yesu angekaa kaburini. (Mathayo 12:38-40) Ushuhuda wa Yesu unathibitisha kwamba simulizi la Yona ni la kweli.

“Kwa Mungu hakuna tangazo lolote lisilowezekana.”—LUKA 1:37.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Yona alipowasihi, mabaharia walimwinua na kumtupa baharini