Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani Ni Nini?

Imani Ni Nini?

Imani Ni Nini?

UNGEFAFANUA imani jinsi gani? Watu fulani wanasema kwamba imani ni kuamini tu jambo bila kuwa na msingi. Wakati mmoja mwandishi mashuhuri kutoka Marekani, H. L. Mencken, alisema kwamba imani ni “kuamini bila msingi jambo lisiloweza kutukia.”

Tofauti na hilo, Biblia haisemi kwamba tunapaswa kuamini tu jambo bila kuwa na msingi. Neno la Mungu linasema: “Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.”—Waebrania 11:1.

Kwa sababu watu wana maoni mbalimbali kuhusu imani, hebu tuchunguze majibu ya maswali yafuatayo:

Ufafanuzi wa Biblia unatofautiana jinsi gani na maoni ya watu wengi kuhusu imani?

kwa nini ni muhimu kusitawisha imani ambayo Biblia inazungumzia?

Unaweza kuimarisha imani yako jinsi gani?

Hati ya Kumiliki na Uthibitisho Imara

Wakati kitabu cha Biblia cha Waebrania kilipoandikwa, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “tarajio lililohakikishwa” lilikuwa likitumiwa sana. Mara nyingi neno hilo lilitumiwa kwenye hati za kibiashara kumhakikishia mtu kwamba atamiliki kitu fulani wakati ujao. Kwa hiyo, kitabu kimoja kinasema kwamba andiko la Waebrania 11:1 linaweza kutafsiriwa hivi: “Imani ni hati ya kumiliki ya mambo yanayotumainiwa.”

Ikiwa umewahi kununua kitu fulani katika kampuni yenye kutegemeka kisha ukangoja uletewe kitu hicho, basi umeonyesha imani kama hiyo. Risiti uliyopewa uliponunua kitu hicho ilikupa sababu ya kuwa na imani katika kampuni hiyo. Kwa njia fulani, risiti hiyo ilikuwa hati yako ya kumiliki, uhakikisho kwamba utapata kitu ulichonunua. Ikiwa ungekuwa umeipoteza risiti yako ama kuitupa, ungekuwa umepoteza uthibitisho wa kwamba umenunua kitu hicho. Vivyo hivyo, watu walio na imani kwamba Mungu atatimiza ahadi zake wanahakikishiwa kuwa ahadi hizo zitatimizwa. Kwa upande mwingine, wale wasio na imani, au wanaoipoteza, hawatastahili kupokea mambo ambayo Mungu ameahidi.—Yakobo 1:5-8.

Katika Waebrania 11:1, neno linalotafsiriwa “uthibitisho ulio wazi,” linamaanisha kuthibitisha mambo, kinyume na jinsi yanavyoonekana. Kwa mfano, jua linaonekana kuizunguka dunia—linachomoza upande wa mashariki, linapita juu angani, kisha linatua upande wa magharibi. Hata hivyo, wataalamu wa nyota na wanahisabati wamethibitisha kwamba jua halizunguki dunia lakini dunia yenyewe ndiyo inayozunguka. Baada ya kuona uthibitisho huo na kuukubali, unaamini jambo hilo ijapokuwa inaonekana tofauti kwa macho. Kwa hiyo, imani haimaanishi kuamini jambo bila msingi, bali inakusaidia kuona jinsi mambo yalivyo kikweli.

Imani Imara Ni Muhimu

Biblia inatutia moyo tuwe na imani imara inayojengwa juu ya uthibitisho thabiti, hata ikiwa itabidi tubadili maoni yetu. Imani kama hiyo ni muhimu sana. Mtume Paulo aliandika: “Pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”—Waebrania 11:6, Union Version.

Kuna mambo mengi yanayoweza kukuzuia usisitawishe imani imara. Lakini ukifanya mambo manne yanayozungumziwa katika kurasa zinazofuata, unaweza kufaulu.