Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unahitaji Kujifunza Kiebrania na Kigiriki?

Je, Unahitaji Kujifunza Kiebrania na Kigiriki?

Je, Unahitaji Kujifunza Kiebrania na Kigiriki?

SEHEMU kubwa ya Biblia iliandikwa katika lugha mbili tu hapo mwanzoni, Kiebrania na Kigiriki. * Waandishi ambao walitumia lugha hizo walifanya hivyo wakiongozwa na roho takatifu ya Mungu. (2 Samweli 23:2) Kwa hiyo, tunaweza kusema kwamba ujumbe ambao waliandika ‘uliongozwa na roho ya Mungu.’—2 Timotheo 3:16, 17.

Hata hivyo, idadi kubwa ya watu ambao wanasoma Biblia leo hawaelewi Kiebrania au Kigiriki. Badala yake, wanahitaji kutumia Biblia iliyotafsiriwa katika lugha yao wenyewe. Labda unahitaji kufanya vivyo hivyo. Kwa kuwa tafsiri hizo hazidai kwamba ziliongozwa na roho ya Mungu, huenda umewahi kujiuliza hivi: ‘Je, ninaweza kuelewa kikamili ujumbe wa Biblia ikiwa ninatumia Biblia iliyotafsiriwa, au je, ninapaswa kujaribu kujifunza Kiebrania na Kigiriki?’

Mambo Unayopaswa Kukumbuka

Kabla ya kujibu swali hilo, unahitaji kukumbuka mambo fulani. Kwanza, kujua tu lugha ya Kiebrania au Kigiriki hakumfanyi mtu aelewe kimuujiza ujumbe wa Biblia. Alipokuwa akizungumza na Wayahudi wa siku zake, Yesu alisema hivi: “Ninyi mnayachunguza Maandiko, kwa sababu mnafikiri kwamba kwa njia yake mtakuwa na uzima wa milele; na hayo yenyewe ndiyo yanayotoa ushahidi juu yangu. Na bado hamtaki kuja kwangu ili mpate kuwa na uzima.” (Yohana 5:39, 40) Walikuwa na tatizo gani? Je, hawakuelewa Kiebrania? Hapana, walijua lugha hiyo vizuri. Hata hivyo, Yesu aliendelea kusema hivi: “Ninajua vizuri kwamba ninyi hammpendi Mungu ndani yenu.”—Yohana 5:42.

Vivyo hivyo, mtume Paulo aliwaambia hivi Wakristo waliozungumza Kigiriki katika jiji la kale la Korintho: “Wayahudi wanaomba ishara na Wagiriki wanatafuta hekima; lakini sisi tunamhubiri Kristo aliyetundikwa mtini, kwa Wayahudi ni sababu ya kujikwaa lakini kwa mataifa ni upumbavu.” (1 Wakorintho 1:22, 23) Basi, ni wazi kwamba kuzungumza tu Kiebrania au Kigiriki si ufunguo wa kukubali ujumbe wa Neno la Mungu.

Jambo la pili ni kwamba ingawa watu fulani leo wanazungumza Kiebrania au Kigiriki cha kisasa, lugha hizo ni tofauti kabisa na Kiebrania na Kigiriki kilichotumiwa kuandika Biblia. Leo, watu wengi wanaozungumza Kigiriki wanaona kwamba ni vigumu kuelewa kwa usahihi Kigiriki cha Biblia. Sababu ni kwamba maneno mapya yameongezwa katika lugha hiyo, na kuchukua mahali pa maneno ya zamani, na maneno mengi ambayo bado yanatumiwa leo yana maana tofauti. Kwa mfano, neno linalotafsiriwa “sura nzuri” kwenye andiko la Matendo 7:20 au “mwenye kupendeza” kwenye Waebrania 11:23 linamaanisha “mwenye kuchekesha” katika Kigiriki cha leo. Kwa kuongezea, mpangilio wa maneno na sheria za lugha hiyo zimebadilika sana.

Hata ikiwa utajifunza Kiebrania au Kigiriki cha leo, haimaanishi kwamba utaweza kuielewa kwa usahihi zaidi Biblia iliyoandikwa katika lugha za zamani. Bado utahitaji kutegemea kamusi na vitabu vya lugha ili ujue jinsi lugha hizo zilivyotumiwa wakati vitabu vya Biblia vilipoandikwa hapo mwanzoni.

Jambo la tatu ni kwamba kujifunza lugha mpya kunaweza kuwa kazi gumu sana. Ingawa mwanzoni inaweza kuwa rahisi kidogo kujifunza maneno machache ya lugha nyingine, huenda ukahitaji kuendelea kujitahidi sana kwa miaka mingi ili uweze kuelewa tofauti ndogo-ndogo katika maana ya maneno ya lugha hiyo. Kwa sasa, msemo huu wa zamani ni wa kweli, Ujuzi mdogo unaweza kuwa hatari. Jinsi gani?

Neno Hilo Linamaanisha Nini?

Je, umewahi kuulizwa na mtu fulani anayejifunza lugha yako maana ya neno fulani? Ikiwa ndivyo, unajua kwamba sikuzote si rahisi kujibu swali hilo. Kwa nini? Kwa sababu neno linaweza kuwa na maana mbalimbali. Huenda ulijikuta ukimuuliza mtu huyo akupe mfano wa sentensi iliyo na neno hilo. Usipojua jinsi neno hilo linavyotumiwa katika sentensi hiyo, inaweza kuwa vigumu kujua maana sahihi ya neno hilo. Kwa mfano, huenda ukaulizwa maana ya neno “chuma” katika Kiswahili. Neno hilo linaweza kuwa na maana tofauti katika hali mbalimbali. Linaweza kumaanisha aina fulani ya mawe magumu, mtu mwenye nguvu, au silaha, hasa bastola au bunduki. Katika hali tofauti, neno hilo linaweza kumaanisha kitu au jambo gumu, au hata virutubishi fulani vya kujenga mwili vinavyopatikana katika chakula. Pia, neno hilo linaweza kumaanisha tendo la kuchukua matunda au maua kutoka kwenye mti, au kupata faida ya pesa nyingi hasa katika biashara. Linapotumiwa katika msemo “moyo wa chuma” linakuwa na maana tofauti kabisa, yaani, mtu asiye na huruma au mgumu. Ni maana gani iliyo sahihi?

Kamusi inaweza kukusaidia kupata maana mbalimbali za neno fulani. Kamusi fulani hata zinaonyesha maana ya neno kulingana na jinsi linavyotumiwa kwa ukawaida. Lakini unaweza kujua maana fulani hususa ikitegemea linatumiwa katika hali gani. Kwa mfano: Tuseme kwamba una ujuzi mdogo sana kuhusu matibabu na unataka kujua ni nini kinachosababisha dalili fulani ulizonazo. Unaweza kuchunguza kamusi ya matibabu. Huenda ikasema kwamba katika asilimia 90 ya watu, dalili hizo zinasababishwa na tatizo fulani lakini katika asilimia 10 ya watu ni dalili za tatizo lingine tofauti kabisa. Huenda ukahitaji ujuzi zaidi kabla ya kuelewa kwa usahihi tatizo lako. Vivyo hivyo, kujua kwamba neno fulani linamaanisha jambo fulani katika asilimia 90 ya visa hakuwezi kukusaidia ikiwa unasoma habari ambayo haihusu maana ya msingi ya neno hilo. Unahitaji kujua habari kamili kabla ya kuelewa maana ya neno hilo.

Inapohusu kujifunza maneno yaliyo katika Biblia, unahitaji pia kujua neno hilo linatumiwa katika hali gani. Kwa mfano, maneno ya awali ambayo kwa kawaida yanatafsiriwa “roho” yanaweza kuwa na maana mbalimbali, ikitegemea habari inayozungumziwa. Nyakati nyingine, yanaweza kutafsiriwa kwa usahihi kuwa “upepo.” (Kutoka 10:13; Yohana 3:8) Katika habari nyingine yanamaanisha nguvu ya uhai ambayo iko ndani ya viumbe wote walio hai, wanadamu na wanyama. (Mwanzo 7:22; Zaburi 104:29; Yakobo 2:26) Viumbe wa mbinguni ambao hawaonekani wanaitwa pia roho. (1 Wafalme 22:21, 22; Mathayo 8:16) Nguvu ya Mungu ya utendaji inaitwa roho yake takatifu. (Mwanzo 1:2; Mathayo 12:28) Neno hilohilo linatumiwa kumaanisha nguvu ambayo inamsukuma mtu kuonyesha mtazamo, mwelekeo, au hisia fulani, vilevile mwelekeo wa akili ambao unaonyeshwa kwa ujumla na kikundi fulani cha watu.—Yoshua 2:11; Wagalatia 6:18.

Ingawa kamusi ya Kiebrania au ya Kigiriki inaweza kuonyesha maana hizo mbalimbali, ni matumizi ya neno hilo katika hali fulani ndiyo yanayoamua maana inayofaa. * Jambo hilo ni la kweli iwe unasoma Biblia katika lugha za awali au unatumia tafsiri fulani katika lugha yako.

Je, Ni Kosa Kutumia Biblia Iliyotafsiriwa?

Watu fulani wamejitahidi sana kujifunza Kiebrania au Kigiriki cha Biblia au lugha zote mbili. Hata ingawa wanajua kwamba hawaelewi mambo yote katika lugha hizo, wanafurahi kwamba wanaweza kusoma Biblia katika lugha za awali na wanahisi kuwa jitihada zao si za bure. Hata hivyo, ikiwa huwezi kufanya hivyo, je, unapaswa kuvunjika moyo na kuacha kutafuta kweli ya Biblia? Hapana! Kuna sababu za kutokata tamaa.

Kwanza, ni jambo linalofaa kutumia Biblia iliyotafsiriwa. Kwa kweli, waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, au yale ambayo wengine wanaita Agano Jipya, mara nyingi walitumia tafsiri ya Kigiriki waliponukuu Maandiko ya Kiebrania. * (Zaburi 40:6; Waebrania 10:5, 6) Ingawa walizungumza Kiebrania na wangeweza kunukuu Maandiko ya awali ya Kiebrania, ni wazi kwamba walifurahi kutumia tafsiri ya mistari hiyo ambayo watu wengi waliokuwa wakiwaandikia walikuwa nayo.—Mwanzo 12:3; Wagalatia 3:8.

Pili, hata ikiwa mtu anaweza kuelewa lugha zilizotumiwa kuandika Biblia, anaweza kusoma maneno ya Yesu kwa kutumia tu Biblia iliyotafsiriwa. Sababu ni kwamba waandikaji wa vitabu vya Injili waliandika katika lugha ya Kigiriki mambo ambayo Yesu alisema mwanzoni kwa kutumia aina fulani ya Kiebrania. * Mtu yeyote anayefikiri kwamba kuweza kusoma maneno yaliyoandikwa na watumishi waaminifu wa zamani wa Yehova katika lugha za awali kunamfanya awe na aina fulani ya hekima ya pekee anapaswa kufikiria matokeo ya jambo hilo. Uhakika wa kwamba Yehova alitumia roho yake kuhifadhi maneno ya Mtumishi wake mkuu zaidi katika tafsiri, yaani, lugha iliyoeleweka zaidi wakati huo, unaonyesha kwamba lugha tunayotumia kusoma Biblia si muhimu. Jambo la maana ni kusoma ujumbe wa Biblia ulioongozwa na roho ya Mungu katika lugha ambayo tunaweza kuelewa na kutenda kulingana na yale tunayosoma.

Tatu, “habari njema” ambayo iko katika Biblia ilipaswa kuenezwa kwa watu wanyenyekevu wa “kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufunuo 14:6; Luka 10:21; 1 Wakorintho 1:27-29) Kupatana na hilo, idadi kubwa sana ya watu leo wanaweza kujifunza kusudi la Mungu kwa kutumia Biblia ya lugha yao wenyewe bila kujifunza lugha nyingine. Katika lugha nyingi, kuna tafsiri mbalimbali ambazo zinapatikana, hivyo msomaji anaweza kuchagua tafsiri yoyote ile. *

Basi unaweza kuhakikisha namna gani kwamba unaelewa kweli iliyo katika Biblia? Mashahidi wa Yehova wamegundua kwamba kujifunza Biblia kwa kutumia vichwa mbalimbali, na kuchunguza habari yote kwa ukamili, ni njia yenye faida ya kuelewa ujumbe ulio katika Neno la Mungu. Kwa mfano, wanachukua kichwa fulani, kama vile “Ndoa,” na kuchunguza mistari inayozungumzia kichwa hicho. Kwa njia hiyo, wanaruhusu sehemu moja ya Biblia ieleze maana ya sehemu nyingine. Kwa nini usifaidike na programu ya kujifunza Biblia nyumbani bila malipo ambayo Mashahidi wa Yehova wanawatolea watu wote? Hata uwe unazungumza lugha gani, Mungu anataka “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:4; Ufunuo 7:9.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 2 Sehemu fulani za Biblia ziliandikwa katika Kiaramu, lugha ambayo inakaribiana sana na Kiebrania cha Biblia. Kwa mfano, lugha hiyo ilitumiwa kwenye Ezra 4:8 mpaka 6:18 na 7:12-26, Yeremia 10:11, na Danieli 2:4b mpaka 7:28.

^ fu. 14 Unapaswa kukumbuka kwamba kamusi na vitabu fulani vinavyofafanua maneno ya Biblia vinaonyesha tu jinsi ambavyo neno fulani limetafsiriwa katika tafsiri fulani ya Biblia, kama vile tafsiri ya King James Version, badala ya kufafanua moja kwa moja maana ya neno hilo.

^ fu. 17 Kufikia wakati wa Yesu Kristo na mitume wake, vitabu vyote vya Maandiko ya Kiebrania vingeweza kusomwa katika Kigiriki. Tafsiri hiyo iliitwa Septuagint nayo ilitumiwa sana na Wayahudi waliozungumza Kigiriki. Idadi kubwa ya mamia ya manukuu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliyonukuliwa moja kwa moja kutoka katika Maandiko ya Kiebrania yanategemea Septuagint.

^ fu. 18 Inaaminika kwamba hapo mwanzoni Injili ya Mathayo iliandikwa na mtume Mathayo katika Kiebrania. Lakini, hata kama ni kweli, tafsiri ambayo imehifadhiwa mpaka leo ni tafsiri ya awali ya Kigiriki, ambayo labda iliandikwa na Mathayo mwenyewe.

^ fu. 19 Kwa mazungumzo kuhusu aina mbalimbali za tafsiri na jinsi ya kuchagua tafsiri iliyo sahihi, ona habari yenye kichwa “Jinsi ya Kuchagua Tafsiri Nzuri ya Biblia,” katika toleo la Mei 1, 2008 la gazeti hili.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]

Tafsiri ya Septuagint

Wayahudi waliozungumza Kigiriki wakati wa Yesu na mitume wake walitumia sana tafsiri ya Septuagint ya Kigiriki. Hiyo ni tafsiri ya Maandiko ya Kiebrania katika lugha ya Kigiriki. Tafsiri hiyo ya Septuagint ni ya pekee kwa sababu ndiyo tafsiri ya kwanza ya Maandiko Matakatifu katika lugha nyingine na pia inavutia kwa sababu mradi huo ulichukua miaka mingi. Watafsiri fulani wakiwa kikundi walianza kuitafsiri Septuagint katika karne ya tatu K.W.K., na kazi hiyo ilikamilishwa na watu wengine miaka 100 baadaye.

Wakristo wa mapema walianza mara moja kuitumia kikamili tafsiri ya Septuagint ili kuthibitisha kwamba Yesu ndiye Kristo, yule Masihi aliyeahidiwa. Waliitumia kwa matokeo sana hivi kwamba watu wengine walianza kuiona Septuagint kuwa ni tafsiri ya “Wakristo.” Hilo liliwafanya Wayahudi waache kutumia tafsiri hiyo na hivyo tafsiri nyingine mpya zikatolewa katika Kigiriki. Moja ya tafsiri hizo ilitolewa na mtu aliyeitwa Akila ambaye aligeuza imani na kufuata dini ya Kiyahudi katika karne ya pili W.K. Alipokuwa akieleza kuhusu tafsiri hiyo ya Akila, msomi mmoja wa Biblia alisema kwamba ilikuwa na “kitu kisichotazamiwa kabisa.” Jina la Mungu, Yehova, likiwa limeandikwa kwa herufi za Kiebrania, linapatikana kotekote katika tafsiri ya Kigiriki ya Akila.

[Hisani]

Israel Antiquities Authority

[Picha katika ukurasa wa 23]

Ni jambo la maana kusoma ujumbe wa Biblia ulioongozwa na roho ya Mungu katika lugha ambayo tunaweza kuelewa na kutenda kulingana na yale tunayosoma