Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukweli Kuhusu Har–Magedoni

Ukweli Kuhusu Har–Magedoni

Ukweli Kuhusu Har–Magedoni

“Roho za pepo . . . ndio wanaokwenda kwa wafalme wa ulimwengu wote na kuwakusanya pamoja . . . mahali paitwapo kwa Kiebrania Har–Magedoni.” (Italiki ni zetu.)​—UFUNUO 16:14, 16, Biblia Habari Njema.

“HAR–MAGEDONI” ni jina la eneo fulani.

Hivyo basi, kwa nini mara nyingi linahusianishwa na tukio fulani, kama vile vita? Neno “Har–Magedoni” linamaanisha nini hasa?

Wakusanywa Mahali Panapoitwa Har–Magedoni

Kihalisi, neno la awali la Kiebrania Har–Magedon linamaanisha “Mlima wa Megido.” Ingawa hakukuwa na mlima ulioitwa hivyo, kuna eneo lililoitwa Megido. Eneo hilo lilikuwa katika sehemu muhimu ambapo barabara mbili kuu zilikutana kaskazini-magharibi mwa eneo lililomilikiwa na taifa la kale la Israeli. Vita vingi vya kukata maneno vilipiganwa karibu na eneo hilo. Kwa hiyo, jina Megido likaanza kuhusianishwa na vita. *

Hata hivyo, umuhimu wa Megido hasa, si vita vilivyopiganwa katika eneo hilo, bali kwa nini vita hivyo vilipiganwa. Megido ilikuwa sehemu ya Nchi ya Ahadi ambayo Yehova Mungu aliwapa Waisraeli. (Kutoka 33:1; Yoshua 12:7, 21) Mungu aliapa kwamba angewalinda Waisraeli wasishambuliwe na wavamizi, na alifanya hivyo. (Kumbukumbu la Torati 6:18, 19) Kwa mfano, katika eneo hilo la Megido, Yehova aliwalinda Waisraeli kimuujiza wasishindwe waliposhambuliwa na majeshi ya Mfalme Yabini wa Kanaani na mkuu wa jeshi lake Sisera.​—Waamuzi 4:14-16.

Hivyo basi, neno “Har–Magedoni,” lina maana kubwa sana ya mfano. Linahusianishwa na mapambano ambapo vikundi viwili vyenye nguvu vinapigana.

Unabii katika kitabu cha Ufunuo unataja kuhusu wakati ujao hivi karibuni ambapo Shetani na roho waovu watachochea serikali za wanadamu zikusanye majeshi yao, na kwa kufanya hivyo watakuwa wakipinga kwa ukaidi watu wa Mungu na kazi yao. Vita hivyo vitasababisha vifo vya mamilioni ya watu wakati Mungu atakapowashinda washambuliaji hao.​—Ufunuo 19:11-18.

Kwa nini Mungu, ambaye Biblia inamtaja kuwa mwenye ‘rehema, asiye mwepesi wa hasira, na mwingi wa fadhili zenye upendo,’ asababishe vifo vya wanadamu wengi hivyo? (Nehemia 9:17) Ili tuelewe kwa nini Mungu atatenda hivyo, tunahitaji kujibu maswali matatu: (1) Ni nani anayeanzisha vita hivyo? (2) Kwa nini Mungu ashiriki katika vita hivyo? (3) Vita hivyo vitakuwa na matokeo gani ya kudumu juu ya dunia na wakaaji wake?

1. NANI ANAYEANZISHA VITA HIVYO?

Vita vya Har–Magedoni si mashambulizi yanayoanzishwa na Mungu. Badala yake, Mungu atawalinda watu wazuri kutokana na wale watakaowashambulia. Washambuliaji katika vita hivi ni “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa,” yaani, watawala wa dunia. Kwa nini wawashambulie watu wa Mungu? Kwa sababu, Shetani atayachochea mashirika ya kiserikali na ya kijeshi yawashambulie vikali watu wanaomwabudu Yehova Mungu.​—Ufunuo 16:13, 14; 19:17, 18.

Kwa kuwa watu wanathamini sana uhuru wa kusema na uhuru wa kuabudu katika nchi fulani leo, huenda wazo la kwamba serikali zitajaribu kuondoa au kuzuia mashirika ya kidini likaonekana kuwa lisilowezekana. Ingawa hivyo, mashambulizi kama hayo yalitokea katika karne ya 20 na pia yanaendelea kutokea leo. * Hata hivyo, kuna angalau tofauti mbili kati ya mashambulizi hayo na lile linalohusianishwa na Har–Magedoni. Kwanza, shambulizi hilo litafanywa duniani kote. Pili, Yehova atatenda kwa kiwango kikubwa kuliko jinsi alivyotenda wakati uliopita. (Yeremia 25:32, 33) Biblia inataja mapambano hayo kuwa “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.”

2. KWA NINI MUNGU ASHIRIKI KATIKA VITA HIVYO?

Yehova anawafundisha wale wanaomwabudu wawe wenye kufanya amani na wawapende adui zao. (Mika 4:1-3; Mathayo 5:43, 44; 26:52) Hivyo, hawatatumia silaha ili kujilinda watakaposhambuliwa vikali. Ikiwa Mungu hataingilia kati ili kuwaokoa watu wake, basi wataangamizwa kabisa. Kwa hiyo, jina la Yehova Mungu, au sifa zake nzuri, zitapatwa na suto. Ikiwa washambulizi hao watafaulu kuwaangamiza watu wake, hilo litamaanisha kwamba Yehova hana upendo, uwezo, na hatendi kwa haki. Jambo hilo haliwezekani kamwe!​—Zaburi 37:28, 29.

Mungu hataki kumwangamiza mtu yeyote, hivyo anatoa onyo kuhusu mambo atakayotenda. (2 Petro 3:9) Kupita masimulizi yaliyo katika Biblia, anawakumbusha wote kwamba hapo zamani aliwatetea watu wake waliposhambuliwa. (2 Wafalme 19:35) Pia, Biblia inaonya kwamba wakati ujao Shetani na wanadamu anaowaongoza watakapowashambulia watu wake, Yehova ataingilia kati tena na kuwapigania. Isitoshe, Neno la Mungu lilikuwa limetabiri zamani kwamba Mungu atawaharibu waovu. (Methali 2:21, 22; 2 Wathesalonike 1:6-9) Bila shaka, kufikia wakati huo, washambuliaji hao watafahamu kwamba wanapigana na Mungu Mweza-Yote.​—Ezekieli 38:21-23.

3. VITA HIVYO VITAKUWA NA MATOKEO GANI YA KUDUMU?

Baada ya vita vya Har–Magedoni mamilioni ya watu wataokolewa. Huo utakuwa mwanzo wa kipindi cha amani duniani.​—Ufunuo 21:3, 4.

Kitabu cha Ufunuo kinataja “umati mkubwa” wa watu wasio na hesabu ambao wataokoka vita hivyo. (Ufunuo 7:9, 14) Chini ya utawala wa Mungu, watu hao watajitahidi kufanya dunia iwe Paradiso tena kama Mungu alivyokusudia mwanzoni.

Je, tunajua wakati ambapo watu wa Mungu watashambuliwa?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ni jambo la kawaida kuhusianisha eneo fulani na vita. Kwa mfano, jiji la Hiroshima nchini Japani, ambalo liliharibiwa na bomu la atomu, sasa huhusianishwa na tisho la vita vya nyuklia.

^ fu. 13 Maangamizi makubwa yaliyofanywa na Wanazi ni mfano unaoonyesha jinsi serikali ilivyojaribu kuangamiza vikundi vya kidini na kijamii. Pia, wakati wa utawala wa Muungano wa Sovieti, vikundi vya kidini katika nchi zilizokuwa chini ya muungano huo vilikandamizwa sana. Ona makala yenye kichwa “Watu Wanaopenda Amani Watetea Jina Lao Zuri,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 2011, linalochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Yehova Mungu aliwapigania watu wake zamani

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yehova Mungu atawapigania watu wake tena wakati wa vita vya Har–Magedoni