Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Barua Kutoka Ugiriki

Kuhubiri Katika Sehemu ya Mbali Zaidi Kusini mwa Bara Ulaya

Kuhubiri Katika Sehemu ya Mbali Zaidi Kusini mwa Bara Ulaya

MILIMA inayovutia ya Levká iliyo katika kisiwa cha Crete inapotea taratibu wakati mashua yetu inapoelekea kwenye eneo dogo tambarare linalojitokeza nje kwenye kina cha bahari ya Mediterania. Ndani ya mashua kuna kikundi cha watu 13, ambao wanatazamia kwa hamu kwenda kuhubiri katika kisiwa cha Gavdos. Kwenye ramani, sehemu hiyo ndogo iko mbali zaidi kusini mwa bara Ulaya.

Inaonekana tutakuwa na safari nzuri katika siku hii yenye joto kali. Hata hivyo, muda mfupi baadaye upepo mkali unapiga bahari, na kusababisha mashua yetu kurushwa-rushwa na mawimbi. Huku nikijihisi mgonjwa, ninakumbuka simulizi la Biblia la mtume Paulo, ambaye alikumbwa na dhoruba kali alipokuwa akisafiri katika bahari hii karne nyingi zilizopita​—wakati Gavdos ilikuwa ikijulikana kama Kauda. (Matendo 27:13-17) Ninatumaini tu kwamba tutafika salama Gavdos.

Hatimaye tunaona mahali tunapoelekea, mwamba wenye mteremko mkali unaoingia baharini. Ni sehemu tambarare kabisa yenye urefu wa mita 300 tu hivi, ambayo haina mwinuko wowote. Sehemu hiyo ina misitu mikubwa ya misonobari na karibu kilomita 26 za mraba za kisiwa hicho zimefunikwa na pori. Katika maeneo fulani, kuna miti ya miberoshi ambayo imesitawi kwenye fuko za bahari.

Wakati fulani, kisiwa hiki kilikuwa na wakazi karibu 8,000. Leo, idadi ya wakazi wa kudumu wanaoishi katika kisiwa hiki haizidi watu 40. Inaonekana kwamba kisiwa cha Gavdos hakina maendeleo ya kisasa. Ijapokuwa kwa kawaida meli zinazobeba mizigo na mafuta hupitia karibu na pwani ya kisiwa hiki, feri husafiri mara chache sana kutoka kisiwani kwenda Crete. Mara nyingi feri hiyo huchelewa au safari zake huahirishwa kwa sababu ya hali mbaya ya hewa.

Tumekuja Gavdos ili kuwapa watu ujumbe unaoleta furaha na unaochangamsha moyo​—tumaini hakika la wakati ujao la kuwa na uzima wa milele tukiwa na afya kamilifu. Mashua yetu inapotia nanga, tuna hamu ya kwenda ufuoni ili kuhubiri habari hizo njema.

Baada ya kurushwa huku na huku kwa muda wa karibu saa nne na nusu, sura zetu zenye uchovu zinaonyesha kwamba safari yetu ya kuelekea Gavdos haikuwa yenye kuburudisha. Lakini tunajihisi vizuri tunapolala kidogo na kupata kikombe cha kahawa. Baada ya kupitia kifupi masimulizi ya Biblia kuhusu safari ya mtume Paulo, pamoja na sala ya kutoka moyoni, sasa tuko tayari kuanza kazi yetu.

Wenyeji ni wenye urafiki na ni wakarimu. Wanatukaribisha ndani ya nyumba zao na kutupatia vinywaji. Zaidi ya kuwahubiria habari njema kutoka katika Biblia, tunawasaidia kwa njia nyingine inapohitajika. Anapozungumza na mwanamke mmoja, mshiriki fulani wa kikundi chetu ambaye ni fundi wa umeme anaona kifaa cha umeme kilichovunjika kwenye duka la mwanamke huyo na anajitolea kukirekebisha. Mwanamke huyo anaguswa moyo. Anakubali machapisho ya Biblia tunayompa na anatupongeza kwa sababu ya huduma yetu. Mwanamke mwingine anaonyesha uthamini wake kwa kusema hivi: “Kazi yenu inatoka kwa Mungu, haitoki kwa wanadamu, na jambo hilo ni wazi kwa sababu mmekuja kuhubiri kwenye kisiwa hiki cha mbali.”

Inaonekana kwamba watu wanathamini sana machapisho ya Biblia tuliyobeba. Mwanamume mmoja anakubali gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! na anataka machapisho mengi zaidi ya kusoma katika miezi ya majira ya baridi kali. Mwanamume mwingine anataka machapisho ya kujisomea yeye mwenyewe na pia anaomba machapisho mengine ili ayaweke kwenye duka lake kwa ajili ya wateja wake. Anatupatia anwani yake ili tuweze kumtumia magazeti kila mwezi. Familia moja inafurahi sana wanapoonyeshwa kwamba Biblia inataja kisiwa hiki kidogo. Pia, wanafurahi kupokea magazeti yetu.

Ingawa matokeo kama hayo yanatia moyo, kutembelea kisiwa cha Gavdos kunawaletea wengine wetu kumbukumbu zenye kuhuzunisha. Karibu na Ghuba ya Sarakíniko, kuna jengo ambalo wakati mmoja lilitumiwa kuwafunga mateka wa kisiasa. Emmanuel Lionoudakis, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alifungwa ndani ya jengo hilo katika miaka ya 1930 kwa sababu ya kazi yake ya kuhubiri. * Wakati huo kisiwa cha Gavdos kilifafanuliwa kama “kisiwa kisichoweza kuzaa kinachozalisha tu nge hatari, mahali ambapo watu wengi . . . walikufa kwa sababu ya njaa, kutengwa, na magonjwa, [mahali] ambapo kwa kufaa pameitwa kisiwa cha kifo.” Lionoudakis alivua samaki ili kupata chakula, hata ingawa alijishughulisha pia na kazi ya kuwahubiria wafungwa wenzake, kwa sababu alikuwa Shahidi peke yake katika jengo hilo. Binti yake, mwana-mkwe wake, na mjukuu wake wa kike wanaguswa moyo wanapoona mahali alipoishi Lionoudakis miaka 70 hivi iliyopita. Kwa upande wetu mfano wake unatuchochea kubaki tukiwa waaminifu na wenye bidii katika huduma.

Wafungwa wote hawakufurahia kuishi katika kisiwa hiki cha Gavdos. Lakini kwa upande wetu ni mahali pazuri kwa kuwa mwisho-juma huu tumehubiri kila sehemu ya kisiwa hicho na tumewaachia watu wenye urafiki wanaoishi huko magazeti 46 na broshua tisa. Tunatazamia kwa hamu kuwaona tena rafiki zetu wapya!

Tunashangaa kujua kwamba wakati wetu wa kuondoka umewadia. Lakini kwa mara nyingine tena hali ya hewa si nzuri, safari yetu ya saa 11:00 jioni imeahirishwa. Tunaingia ndani ya mashua saa sita usiku ili tujitayarishe kwa ajili ya safari nyingine ngumu. Hatimaye, tunaondoka saa 9:00 usiku na baada ya kurushwa huku na huku kwenye bahari yenye dhoruba karibu muda wa saa tano, tunawasili Crete. Tumechoka na tunahisi miguu yetu ni dhaifu tunapokanyaga kwenye nchi kavu, lakini tunafurahi kwamba tumefanya jina la Yehova lijulikane kwenye kisiwa cha Gavdos. (Isaya 42:12) Washiriki wote wa kikundi wanakubali kwamba jitihada zetu zilikuwa zenye matokeo. Matatizo tuliyoyakabili yatasahaulika hivi karibuni, lakini tuna uhakika kwamba hatutasahau kamwe kumbukumbu za safari yetu.

^ fu. 11 Ili kupata simulizi la maisha la Emmanuel Lionoudakis, ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1999, ukurasa wa 25-29.