Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kusonga Mbele Baada ya Talaka

Kusonga Mbele Baada ya Talaka

“Nilishtuka na kuvunjika moyo sana. Maisha yalikuwa sawa kisha ghafula, mambo yakabadilika.”—MARK, * aliyetalikiana mwaka mmoja uliopita.

“Mume wangu alifanya uzinzi na mwanamke aliyekuwa na umri kama wa binti yetu. Tulipotalikiana nilipata nafuu kwa sababu alikuwa mjeuri, lakini nilihisi nimedharauliwa na kwamba sifai.”—EMMELINE, aliyetalikiana miaka 17 iliyopita.

Watu fulani hutalikiana wakitumaini mambo yatakuwa mazuri, na wengine hutamani kuendelea katika ndoa lakini wanashindwa kumzuia mwenzi anayetaka talaka. Hata hivyo, wengi wanaotalikiana hutambua kwamba maisha ni magumu kuliko walivyotazamia. Ikiwa umetalikiana hivi karibuni, huenda unahisi hii ndiyo hali ngumu zaidi maishani. Basi, itafaa uchunguze ushauri fulani katika Biblia unaoweza kukusaidia ufaulu kukabiliana na matatizo yanayoletwa na talaka.

TATIZO LA KWANZA: HISIA ZISIZOFAA.

Mtu anaweza kulemewa na matatizo ya kifedha, kulea watoto, na upweke, na kwa kawaida hisia zisizofaa haziishi haraka. Mwanasaikolojia Judith Wallerstein alisema kwamba miaka mingi baada ya kutalikiana, bado watu fulani huhisi wamesalitiwa, wameachwa, “wameonewa, wamevunjwa moyo, na ni wapweke.”

UNACHOWEZA KUFANYA

  • Ombolezea hali yako. Huenda unamkosa mwenzi ambaye bado unampenda. Hata kama hamkuwa  na uhusiano mzuri, huenda ukaomboleza kwa sababu hukupata shangwe uliyotazamia katika ndoa. (Methali 5:18) Usiaibike kutenga “wakati wa kulia.”Mhubiri 3:1, 4.

  • Usijitenge na watu. Ingawa huenda ukahitaji kuwa peke yako ili uomboleze, si jambo la hekima kuendelea kujitenga. (Methali 18:1) Jitahidi kuwa na mazungumzo yenye kujenga pamoja na marafiki, kwa kuwa ukilalamika mara kwa mara kuhusu mwenzi wako wa zamani, huenda ukawaudhi wengine. Kabla ya kufanya uamuzi wowote mzito baada ya talaka, tafuta ushauri kutoka kwa mtu unayemwamini.

  • Tunza afya yako. Mara nyingi mfadhaiko unaoletwa na talaka husababisha matatizo ya kiafya, kama vile kupanda kwa shinikizo la damu au kuumwa na kichwa. Basi, kula vizuri, fanya mazoezi, na ulale vya kutosha.Waefeso 5:29.

  • Ondoa vitu vinavyofanya umkasirikie mwenzi wako wa zamani au usivyohitaji lakini uhifadhi stakabadhi muhimu. Ikiwa vitu kama picha za harusi vinafanya uhisi vibaya, vifungie katika sanduku na kuvihifadhi kwa ajili ya watoto wako.

  • Jitahidi kuondoa mawazo yasiyofaa. Olga, ambaye alimtaliki mumewe aliyefanya uzinzi anasema: “Nilikuwa nikijiuliza, ‘Aliona nini kwa mwanamke huyo?’” Baadaye Olga alitambua kwamba kuendelea kuwa na mawazo yasiyofaa kulisababisha “roho iliyopondeka.”Methali 18:14.

    Watu wengi wameona kwamba wanapoandika mambo yanayowahangaisha wanaweza kutambua mawazo yao na kuyadhibiti. Unapofanya hivyo, jaribu kufikiria wazo linalofaa ambalo linaweza kuchukua mahali pa wazo lisilofaa unalotaka kuondoa akilini. (Waefeso 4:23) Fikiria mifano miwili:

    Wazo la kale: Mimi ndiye niliyefanya mwenzi wangu asiwe mwaminifu.

    Wazo jipya: Kupungukiwa kwangu hakukumpa mwenzi wangu haki ya kufanya uzinzi.

    Wazo la kale: Nilitumia ujana wangu pamoja na mwanamume asiyefaa.

    Wazo jipya: Nitakuwa na furaha zaidi nikikazia fikira wakati ujao badala ya mambo yaliyopita.

  • Usizingatie maneno yasiyofaa. Huenda watu wa ukoo na marafiki wakakuambia mambo yenye kuumiza au yasiyo ya kweli, kama vile, ‘Hakuwa mke anayekufaa’ au ‘Mungu anachukia talaka.’ * Kwa kufaa Biblia inatushauri hivi: “Usiweke moyoni mwako maneno yote ambayo huenda watu wakasema.” (Mhubiri 7:21) Martina aliyetalikiana miaka miwili iliyopita anasema: “Badala ya kufikiria maneno yenye kuumiza, ninajitahidi kuwa na maoni kama ya Mungu. Mawazo yake yako juu kuliko mawazo yetu.”Isaya 55:8, 9.

  • Sali kwa Mungu. Yeye huwatia moyo wale wanaomwabudu ‘wamtupie mahangaiko yao,’ hasa wanapolemewa na hisia.1 Petro 5:7.

JARIBU KUFANYA HIVI: Andika maandiko fulani ya Biblia, na uyaweke mahali unapoweza kuyaona mara kwa mara. Mbali na maandiko ambayo tayari yametajwa, watu wengi waliotalikiana wamefaidika kwa kusoma maandiko yafuatayo: Zaburi 27:10; 34:18; Isaya 41:10; na Waroma 8:38, 39.

Tumia Neno la Mungu ili kupata faraja unapokabiliana na hali kigumu

TATIZO LA PILI: UHUSIANO PAMOJA NA MWENZI WAKO WA ZAMANI.

Juliana, ambaye aliishi katika ndoa kwa miaka 11 anasema: “Nilimsihi mume wangu asiniache. Hata hivyo, alipoondoka nilimkasirikia pamoja na  mwanamke aliyeanza kuishi naye.” Wengi wanaotalikiwa huendelea kumkasirikia kwa miaka mingi mwenzi wao wa zamani. Lakini bado wanalazimika kuwasiliana kwa ukawaida, hasa kama wana watoto.

UNACHOWEZA KUFANYA

  • Dumisha heshima katika uhusiano pamoja na mwenzi wa zamani. Kazia fikira mambo muhimu na uzungumze kifupi na kutaja mambo waziwazi. Wengi wametambua kwamba kufanya hivyo huleta amani.Waroma 12:18.

  • Usitumie maneno yenye kuumiza. Ushauri huu wa Biblia unafaa sana hasa unapohisi kwamba unashambuliwa: “Yeyote anayezuia maneno yake ana ujuzi.” (Methali 17:27) Mkianza kuzozana, unaweza kusema: “Acha nifikirie ulichosema kisha tutazungumza baadaye.”

  • Kwa kadiri iwezekanavyo, tenganisha shughuli zako na za mwenzi wa zamani kutia ndani mambo ya kisheria, kifedha, na matibabu.

JARIBU KUFANYA HIVI: Utakapozungumza na mwenzi wako wa zamani, tambua dalili zinazoonyesha kwamba mmoja wenu anaanza kujitetea au kushikilia maoni yake. Ikihitajika, katisha mazungumzo au umweleze kwamba mtawasiliana kupitia barua-pepe.Methali 17:14.

TATIZO LA TATU: KUWASAIDIA WATOTO WAKO WAKABILIANE NA HALI MPYA.

Maria anakumbuka jinsi ilivyokuwa baada ya kutalikiana: “Binti yangu mdogo alilia kila mara na akaanza tena kukojoa kitandani. Ingawa msichana wangu mkubwa alijaribu kuficha hisia zake, niliona yeye pia alikuwa amebadilika.” Huenda ukahisi huna wakati au nguvu za kuwasaidia watoto wako wakabili hali hiyo ngumu.

UNACHOWEZA KUFANYA

  • Watie moyo watoto wako wakueleze hisia zao hata kama hilo linaweza kusababisha “mazungumzo ya ovyoovyo.”Ayubu 6:2, 3.

  • Kumbuka madaraka yako. Ingawa huenda ukatamani kutiwa moyo na ikaonekana kwamba mtoto wako yuko tayari kukusaidia, hupaswi kumhusisha mtoto katika matatizo ya watu wazima. (1 Wakorintho 13:11) Usimfunulie mtoto mahangaiko yako au kumpa daraka la kuwa mpatanishi kati yako na mwenzi wa zamani.

  • Usivuruge maisha ya mtoto wako. Ni vizuri kuendelea kuishi katika nyumba ileile na kudumisha ratiba yenu, lakini jambo muhimu zaidi ni kudumisha uhusiano wenu pamoja na Mungu, ikitia ndani kusoma Biblia na kuwa na ibada ya familia.Kumbukumbu la Torati 6:6-9.

JARIBU KUFANYA HIVI: Katika juma hili, wahakikishie watoto wako kwamba unawapenda na kwamba hawakufanya wewe na mwenzi wako mtalikiane. Jibu maswali yao bila kumlaumu yule mzazi mwingine.

Unaweza kuendelea na maisha baada ya talaka. Melissa, ambaye alikuwa katika ndoa kwa miaka 16 anasema, “Tulipotalikiana, nilijiambia, ‘Sikutaka maisha yangu yawe hivi.’” Hata hivyo, sasa ameridhika licha ya hali yake. Anasema, “Mara tu nilipoacha kujaribu kubadili mambo ya zamani, nilihisi utulivu.”

^ fu. 2 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 18 Mungu anachukia watu wanaotalikiana kwa udanganyifu na hila. Lakini mwenzi wa ndoa anapofanya uasherati, Mungu anamruhusu mwenzi asiye na hatia kuamua kama atamtaliki. (Malaki 2:16; Mathayo 19:9) Ona makala “Maoni ya Biblia—Mungu Huchukia Talaka ya Aina Gani?” katika gazeti Amkeni! la Februari 8, 1994, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

JIULIZE . . .

  • Baada ya talaka, je, nimetenga wakati wa kuomboleza?

  • Ninawezaje kuondoa hisia zisizofaa kumwelekea mwenzi wangu wa zamani?