Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 WASOMAJI WETU WANAULIZA . . .

Kwa Nini Mungu Anaruhusu Watu Wenye Nguvu Wawakandamize Wanyonge?

Kwa Nini Mungu Anaruhusu Watu Wenye Nguvu Wawakandamize Wanyonge?

Biblia inasimulia visa fulani vya ukandamizaji. Huenda unakumbuka kisa cha Nabothi. * Ahabu, aliyekuwa mfalme wa Israeli katika karne ya kumi K.W.K., alimruhusu mkewe, Yezebeli, apange njama ya kumuua Nabothi na wanawe ili mfalme achukue shamba lake la mizabibu. (1 Wafalme 21:1-16; 2 Wafalme 9:26) Kwa nini Mungu alimruhusu Ahabu atumie mamlaka yake vibaya?

‘Mungu hawezi kusema uwongo.’—Tito 1:2

Acheni tukazie sababu moja muhimu: Mungu hawezi kusema uwongo. (Tito 1:2) Hilo linahusianaje na matendo ya ukandamizaji? Hapo mwanzo, Mungu aliwaonya wanadamu kwamba ikiwa wangemwasi, wangekufa. Maneno ya Mungu yalitimia, wanadamu wamekuwa wakifa tangu uasi ulipotokea katika bustani ya Edeni. Kwa kweli, kifo cha mwanadamu wa kwanza kilisababishwa na ukandamizaji—Kaini alipomwua Abeli nduguye.Mwanzo 2:16, 17; 4:8.

Biblia inafafanua hivi historia ya wanadamu: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” (Mhubiri 8:9) Je, maneno hayo ni ya kweli? Yehova aliwaonya watu wake, taifa la Israeli, kwamba wangekandamizwa na wafalme wao, na hivyo kusababisha wamlilie Mungu. (1 Samweli 8:11-18) Hata Mfalme Sulemani mwenye hekima aliwatoza watu kodi kupita kiasi. (1 Wafalme 11:43; 12:3, 4) Wafalme waovu kama vile Ahabu, waliwakandamiza watu hata zaidi. Hebu fikiria: Ikiwa Mungu angezuia matendo hayo yote ya ukandamizaji, je, haingemaanisha kwamba alisema uwongo?

“Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”Mhubiri 8:9

Pia, kumbuka Shetani anadai kwamba watu wanamtumikia Mungu kwa sababu ya ubinafsi. (Ayubu 1:9, 10; 2:4) Ikiwa Mungu angewalinda watumishi wake kutokana na ukandamizaji wote, je, hilo halingeunga mkono madai ya Shetani? Kama Mungu angezuia watu wasikandamizwe, je, hilo halingemfanya awe mwongo hata zaidi? Kama angezuia watu wasikandamizwe, wengi wangedhani kwamba wanadamu wanaweza kujitawala kwa mafanikio bila Mungu. Lakini Neno la Mungu linasema kinyume kabisa, kwamba mwanadamu hawezi kujitawala kamwe. (Yeremia 10:23) Tunahitaji Ufalme wa Mungu uje, kwa sababu utakomesha kabisa ukosefu wa haki.

Je, hilo linamaanisha Mungu hafanyi lolote kuhusu ukandamizaji? Hapana. Fikiria mambo mawili anayofanya: Kwanza, anafunua wazi ukandamizaji. Kwa mfano, Neno lake linafunua jinsi Yezebeli alivyopanga njama ya kumwangamiza Nabothi. Isitoshe, Biblia inafunua kuwa uovu huo unachochewa na mtawala mwenye nguvu ambaye hataki kujulikana. (Yohana 14:30; 2 Wakorintho 11:14) Biblia inasema kwamba ni Shetani Ibilisi. Kwa kufunua wazi uovu na ukandamizaji pamoja na chanzo chake, Mungu anatusaidia kujiepusha na uovu. Hivyo basi, anataka tuishi milele.

Pili, Mungu anatuahidi kwamba ukandamizaji utakwisha hivi karibuni. Kwa vile Mungu alifunua, akahukumu, na kuwaadhibu Ahabu na Yezebeli, kutia ndani watu wengine waovu, tuna hakika kwamba siku moja atatimiza ahadi yake ya kuwaangamiza waovu. (Zaburi 52:1-5) Pia, Mungu amewaahidi wale wanaompenda kwamba hivi karibuni ataondoa mateso yote yanayosababishwa na uovu. * Wakati huo, Nabothi mwaminifu pamoja na wanawe watafurahia kuishi milele katika dunia paradiso isiyo na ukosefu wa haki.—Zaburi 37:34.

^ fu. 3 Ona makala “Igeni Imani Yao” katika gazeti hili.

^ fu. 8 Ona sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.