Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Majibu ya Maswali ya Biblia

Majibu ya Maswali ya Biblia

Je, tunaweza kujua kweli kumhusu Mungu?

Kwa nini Mungu anataka tujue kweli? Soma Yohana 17:3

Sikuzote Mungu huwasiliana na wanadamu. Alitumia roho yake takatifu, au nguvu ya utendaji kuwasilisha mawazo yake kwa waandikaji wa Biblia. (2 Petro 1:20, 21) Tunaweza kujua kweli kumhusu Mungu kwa kusoma Biblia.—Soma Yohana 17:17; 2 Timotheo 3:16.

Katika Biblia, Mungu amefunua mambo mengi kuhusu utu wake. Ametujulisha sababu za kutuumba, mambo atakayotufanyia wakati ujao, na jinsi tunavyopaswa kuishi. (Matendo 17:24-27) Yehova Mungu anataka tujue kweli kumhusu yeye.—Soma 1 Timotheo 2:3, 4.

Kwa nini Mungu anawapenda wale wanaopenda kweli?

Yehova ni Mungu wa kweli, na alimtuma Mwana wake, Yesu, kuwafundisha wanadamu kweli. Kwa hiyo, wale wanaopenda kweli huvutiwa na mafundisho ya Yesu. (Yohana 18:37) Mungu anataka watu hao wawe waabudu wake.—Soma Yohana 4:23, 24.

Kwa kueneza mafundisho ya uwongo kumhusu Mungu, Shetani Ibilisi amesababisha watu wengi wasimjue Mungu. (2 Wakorintho 4:3, 4) Watu wanaopenda mambo mabaya wanavutiwa na mafundisho hayo ya uwongo. (Waroma 1:25) Lakini mamilioni ya watu wanyoofu wanapata kweli kwa kujifunza Biblia.—Soma Matendo 17:11.