Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

INDONESIA

Kikundi cha Bibelkring

Kikundi cha Bibelkring

MWISHONI mwa miaka ya 1930, kikundi kipya kilichoitwa Bibelkring (jina la Kiholanzi linalomaanisha “kikundi cha wanafunzi wa Biblia”), kilianzishwa karibu na Ziwa Toba lililoko Sumatra Kaskazini. Kikundi hicho kilianzishwa na baadhi ya walimu wa shule ambao walipokea machapisho kutoka kwa painia ambaye huenda ni Eric Ewins, aliyetembelea na kuhubiri eneo la Ziwa Toba mwaka wa 1936. Mambo waliyojifunza yaliwachochea kuacha kushirikiana na Kanisa la Kiprotestanti la Batak na kuanzisha vikundi vya kujifunza Biblia nyumbani. Vikundi hivyo viliongezeka na kuenea na kuwa na mamia ya washiriki. *

Dame Simbolon, ambaye awali alishirikiana na kikundi cha Bibelkring

Baada ya kujifunza machapisho yaliyoachwa na painia huyo, washiriki wa zamani wa Bibelkring walitambua baadhi ya kweli za Biblia. Dame Simbolon, mshiriki wa zamani ambaye alikubali kweli mwaka wa 1972 alisema hivi: “Washiriki wa kikundi hicho walikataa kuisalimu bendera na kusherehekea Krismasi na sikukuu za kuzaliwa. Wengine hata walihubiri nyumba kwa nyumba.” Hata hivyo, kwa sababu ya kukosa mwongozo kutoka kwa tengenezo la Mungu, kikundi hicho kilianza kuathiriwa na maoni ya wanadamu. Limeria Nadapdap, mshiriki wa zamani wa kikundi hicho ambaye sasa ni dada yetu wa kiroho anasema hivi: “Wanawake hawakuruhusiwa kujipaka vipodozi, kuvaa vito, mavazi ya kisasa au hata viatu. Pia, washiriki wake walikatazwa kuchukua vitambulisho vya taifa, jambo lililowakasirisha wenye mamlaka.”

Baadaye kikundi cha Bibelkring kiligawanyika katika vikundi kadhaa na mwishowe vikundi hivyo vilitoweka. Mapainia waliporudi tena katika eneo la Ziwa Toba, washiriki wengi wa Bibelkring walikubali kujifunza kweli.

^ fu. 1 Vyanzo fulani hukadiria kwamba vikundi vya Bibelkring vilikuwa na maelfu ya washiriki.