Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 20

Mapigo Sita Yaliyofuata

Mapigo Sita Yaliyofuata

Musa na Haruni walienda kumwambia Farao ujumbe huu kutoka kwa Mungu: ‘Ikiwa hutawaruhusu watu wangu waende zao, nitatuma mainzi juu ya nchi yako.’ Makundi makubwa ya mainzi yakaanza kuvamia nyumba za Wamisri, matajiri kwa maskini. Nchi yote ikajaa mainzi. Lakini katika eneo la Gosheni, ambako Waisraeli walikuwa wanaishi, hakukuwa na mainzi. Pigo la nne na yale yaliyofuata yaliwapata Wamisri peke yao. Farao akamsihi hivi Musa: ‘Mwombe Yehova kwa niaba yangu aondoe mainzi hao, kisha watu wako wanaweza kuondoka.’ Hata hivyo, Yehova alipowaondoa mainzi, Farao akabadili mawazo. Unafikiri Farao angejifunza kutii?

Yehova alisema hivi: ‘Ikiwa Farao ataendelea kukataa kuwaruhusu watu wangu waende zao, mifugo ya Wamisri itapatwa na ugonjwa na kufa.’ Siku iliyofuata, mifugo ikaanza kufa. Ila mifugo ya Waisraeli haikufa. Lakini bado Farao aliendelea kuwa na shingo ngumu na hakutaka kuwaruhusu waondoke.

Kisha Yehova akamwambia Musa arudi kwa Farao na kurusha majivu angani. Majivu hayo yakawa vumbi na kujaza nchi yote na kuwafunika Wamisri. Mavumbi hayo yakasababisha majipu juu ya Wamisri na wanyama wao wote. Ingawa hivyo, Farao alikataa kuwaruhusu Waisraeli waondoke.

Yehova akamtuma tena Musa kwa Farao amwambie hivi: ‘Bado unakataa kuwaruhusu watu wangu waondoke? Kesho mvua kubwa sana ya mawe itanyesha juu ya nchi.’ Siku iliyofuata, Yehova akafanya mvua kubwa ya mawe inyeshe, pia kukawa na ngurumo, na moto. Wamisri hawakuwa wamewahi kuona mvua kubwa kama hiyo. Miti yote na mimea iliharibiwa isipokuwa katika eneo la Gosheni. Farao akasema: ‘Msihi Yehova ili mvua iache kunyesha! Halafu nitawaruhusu mwende.’ Hata hivyo, mara tu mvua ilipoacha kunyesha, Farao akabadili mawazo yake tena.

Kisha Musa akasema hivi: ‘Sasa nzige watakula mimea yote iliyobaki baada ya mvua ya mawe kunyesha.’ Makundi ya nzige wengi wakala kila kitu kilichobaki shambani na kwenye miti. Farao akamsihi Musa hivi: ‘Mwombe Yehova awaondoe nzige hawa.’ Lakini hata baada ya Yehova kuwaondoa nzige, bado Farao aliendelea kuwa na shingo ngumu.

Yehova akamwambia Musa hivi: ‘Nyoosha mkono wako kuelekea angani.’ Papo hapo, giza zito likatokea katika nchi yote. Kwa siku tatu, Wamisri hawakuweza kuona kitu chochote. Waisraeli tu ndio waliokuwa na mwanga katika nyumba zao.

Farao akamwambia Musa: ‘Wewe na watu wako mnaweza kwenda. Lakini mwache wanyama wenu.’ Musa akasema: ‘Lazima twende na wanyama ili tukamtolee Mungu wetu dhabihu.’ Farao alikasirika sana. Akamwambia hivi Musa kwa hasira: ‘Toka hapa! Nikikuona tena, nitakuua!’

“Nanyi mtaona tena tofauti kati ya mtu mwadilifu na mtu mwovu, kati ya yule anayemtumikia Mungu na yule asiyemtumikia.”​—Malaki 3:18