Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA PILI

“Alitembea Pamoja na Mungu wa Kweli”

“Alitembea Pamoja na Mungu wa Kweli”

1, 2. Noa na familia yake walifanya kazi gani, na walikabili matatizo gani?

NOA alinyoosha mgongo na misuli yake iliyokuwa na maumivu makali. Mwazie akiwa ameketi kwenye ubao mpana, akipumzika katikati ya kazi, huku akitazama safina kubwa iliyokuwa ikijengwa. Harufu kali ya lami iliyoyeyushwa ilitanda hewani na alisikia sauti za vifaa vya kutengeneza vyombo vya mbao. Akiwa mahali alipoketi, Noa aliwaona wanawe wakifanya kazi kwa bidii kwenye sehemu mbalimbali za jengo hilo kubwa la mbao. Wanawe, wake zao, na mke wake mpendwa walikuwa wamefanya kazi ya kujenga safina kwa makumi ya miaka. Walikuwa wamefanya kazi nyingi, lakini haikuwa imekamilika!

2 Watu katika eneo hilo waliwaona kuwa wapumbavu. Noa alipoendelea kujenga safina, watu walimcheka waliposikia kuhusu gharika ambayo ingefunika dunia yote. Walidhani Noa aliwaonya kuhusu msiba wa kuwaziwa, ambao haungetukia kamwe! Hawakuelewa kwa nini mwanamume angepoteza maisha yake, na ya familia yake, akifanya kazi kama hiyo ya upumbavu. Lakini Yehova, Mungu wake hakumwona hivyo.

3. Noa alitembeaje na Mungu?

3 Neno la Mungu linasema: “Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli.” (Soma Mwanzo 6:9.) Hilo linamaanisha nini? Si kwamba Mungu alitembea duniani, wala kwamba Noa alienda mbinguni. Badala yake, Noa alimtii Mungu wake na kumpenda sana kana kwamba yeye na Yehova walitembea pamoja kama marafiki. Maelfu ya miaka baadaye, Biblia ilisema hivi kumhusu Noa: “Kupitia imani [yake] aliuhukumu ulimwengu.” (Ebr. 11:7) Alifanyaje hivyo? Na tunawezaje kuiga imani yake leo?

Mwanamume Asiye na Lawama Katika Ulimwengu Uliopotoka

4, 5. Katika siku za Noa, uovu ulikuwa umeongezekaje duniani?

4 Noa alilelewa katika ulimwengu uliozidi kuwa mbaya. Mambo yalikuwa mabaya tangu siku za Enoko, mwanamume mwingine mwadilifu ambaye alitembea pamoja na Mungu. Enoko alikuwa ametabiri kwamba siku ya hukumu ingekuja juu ya watu wasiomwogopa Mungu. Sasa katika siku za Noa, uovu ulikuwa umeongezeka sana. Kulingana na maoni ya Yehova, dunia ilikuwa imeharibika, kwa sababu ilijaa jeuri. (Mwa. 5:22; 6:11; Yuda 14, 15) Ni nini kilichofanya uovu uongezeke sana?

5 Uasi ulikuwa umetokea miongoni mwa malaika wa Mungu. Tayari mmoja wao alikuwa amemwasi Yehova, na kuwa Shetani Ibilisi kwa kusema uwongo kumhusu Mungu na kuwashawishi Adamu na Hawa wafanye dhambi. Katika siku za Noa, malaika wengine pia walimwasi Yehova. Waliacha makao yao mbinguni na kuja duniani, kisha wakajivika miili ya kibinadamu na kuchukua wanawake warembo wawe wake zao. Malaika hao waasi na wenye kiburi waliwapotosha sana wanadamu.—Mwa. 6:1, 2; Yuda 6, 7.

6. Wanefili walichocheaje uovu duniani, na Yehova aliazimia kufanya nini?

6 Baadaye, uhusiano huo kati ya wanawake na malaika waliojivika miili ya kibinadamu ukatokeza majitu yenye nguvu. Biblia inawaita Wanefili, jina linalomaanisha “Waangushaji.” Wanefili walikuwa wajeuri, na walizidisha ukatili na uovu duniani. Hivyo, Muumba akaona kuwa “ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani na kila mwelekeo wa fikira za moyo wake ulikuwa mbaya tu wakati wote.” Yehova akaazimia kuangamiza kizazi hicho kiovu baada ya miaka 120.​—Soma Mwanzo 6:3-5.

7. Noa na mkewe walikabili matatizo gani katika kuwalinda wana wao wasiathiriwe na mtazamo mbaya?

7 Hebu wazia kulea watoto katika ulimwengu huo! Noa alikabiliana na hali hiyo. Alioa mke mzuri. Baada ya Noa kufikisha umri wa miaka 500, mkewe alimzalia wana watatu, Shemu, Hamu, na Yafethi. * Wazazi hao walishirikiana kuwalinda wavulana wao wasipotoshwe na uovu uliowazunguka. Wavulana wadogo wana mwelekeo wa kustaajabishwa na “watu wenye nguvu” na “wanaume wenye sifa,” na hivyo ndivyo Wanefili walivyokuwa. Noa na mkewe hawangewazuia watoto wao wasisikie kuhusu vitendo vya majitu hayo, lakini wangewafundisha ukweli kuhusu Yehova Mungu, ambaye anachukia uovu. Walihitaji kuwafundisha wavulana wao kwamba Yehova aliumia moyoni kwa sababu ya jeuri na uasi uliokuwa duniani.—Mwa. 6:6.

Noa na mkewe walihitaji kuwalinda watoto wao ili wasiathiriwe na uvutano mbaya

8. Leo wazazi wenye hekima wanawezaje kumwiga Noa na mkewe?

8 Leo, wazazi wanaelewa hali ambayo Noa na mkewe walikabili. Ulimwengu wetu pia umejaa jeuri na uasi. Majiji mengi yamejaa magenge ya vijana waliopotoka. Hata vitumbuizo vya watoto vimejaa jeuri. Wazazi wenye hekima wanajitahidi kabisa kushinda uvutano huo kwa kuwafundisha watoto wao kumhusu Mungu wa amani, Yehova, ambaye siku moja atakomesha kabisa jeuri. (Zab. 11:5; 37:10, 11) Kwa kweli, wanaweza kufanikiwa! Noa na mkewe walifanikiwa. Wavulana wao walikomaa na kuwa watu wazuri, na wakaoa wake ambao pia walikuwa tayari kumtanguliza Yehova Mungu wa kweli maishani.

“Jifanyie Safina”

9, 10. (a) Ni agizo gani la Yehova ambalo lilibadili maisha ya Noa? (b) Yehova alimpa Noa maagizo gani kuhusu kusudi na muundo wa safina?

9 Siku moja, maisha ya Noa yalibadilika kabisa. Yehova alizungumza na mtumishi huyo mpendwa na akamwambia alikusudia kuharibu ulimwengu wa wakati huo. Mungu alimwagiza Noa hivi: “Jifanyie safina ya mti wenye utomvu.”—Mwa. 6:14.

10 Safina hiyo haikuwa meli kama wengi wanavyodhania. Haikuwa na omo, tezi, usukani, wala haikuwa na umbo lililojipinda. Ilikuwa sanduku kubwa sana. Yehova alimpa Noa vipimo kamili vya safina, maelezo kuhusu muundo wake, na akamwagiza aifunike nje na ndani kwa lami. Kisha akamweleza Noa sababu: “Tazama, mimi ninaleta gharika ya maji duniani . . . Kila kitu kilicho duniani kitakata pumzi.” Hata hivyo, Yehova alifanya mapatano haya na Noa: “Nawe uingie ndani ya safina, wewe na wana wako na mke wako na wake za wana wako pamoja nawe.” Pia, Noa alipaswa kuingiza wawakilishi wa aina zote za wanyama. Wale tu waliokuwa ndani ya safina ndio wangeokoka Gharika!​—Mwa. 6:17-20.

Noa na familia yake walishirikiana kutimiza amri za Mungu

11, 12. Noa alipewa mgawo gani mgumu, na alitendaje?

11 Noa angefanya kazi nyingi. Safina hiyo ingekuwa kubwa sana—yenye urefu wa mita 133, upana wa mita 22, na kimo cha mita 13. Ilikuwa kubwa kuliko meli za kisasa zilizotengenezwa kwa mbao. Je, Noa alikataa mgawo huo, alilalamika kwamba ni mgumu, au kubadili maagizo ili arahisishe kazi? Biblia inajibu hivi: “Noa akafanya kulingana na yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru. Alifanya vivyo hivyo.”—Mwa. 6:22.

12 Kazi hiyo ilichukua miaka mingi, labda kati ya miaka 40 hadi 50. Walipaswa kukata miti, kukokota magogo, kukata mbao, kuzichonga, na kuziunganisha. Safina ingekuwa na ghorofa tatu, vyumba vingi, na mlango kwenye ubavu. Inaelekea ingekuwa na madirisha, na vilevile paa ambalo lilikuwa limeinuka katikati ili kuruhusu maji yatiririke.​—Mwa. 6:14-16.

13. Noa alipewa mgawo gani mwingine uliokuwa mgumu kuliko kujenga safina, na watu waliitikiaje?

13 Kadiri miaka ilivyopita, safina iliendelea kukamilika, na lazima Noa alifurahi sana kuungwa mkono na familia yake! Alipewa kazi nyingine ambayo huenda ilikuwa ngumu kuliko kujenga safina. Biblia inatuambia Noa alikuwa “mhubiri wa uadilifu.” (Soma 2 Petro 2:5.) Hivyo, kwa ujasiri aliongoza kazi ya kuwaonya waovu kuhusu uharibifu ambao ungekuja. Waliitikiaje? Baadaye, Yesu Kristo alitaja kuhusu wakati huo, na akasema watu hao “hawakujali.” Alisema walijishughulisha sana na mambo ya kawaida maishani kama vile, kula, kunywa, kuoa na kuolewa, hivi kwamba hawakumsikiliza Noa. (Mt. 24:37-39) Bila shaka, wengi walimdhihaki pamoja na familia yake; huenda wengine walimtisha na kumpinga vikali. Labda hata walijaribu kusimamisha kazi ya kujenga safina.

Ingawa watu waliona Yehova akimbariki Noa, bado walimdhihaki na kupuuza ujumbe wake

14. Leo familia za Kikristo zinajifunza nini kutoka kwa Noa na familia yake?

14 Lakini Noa na familia yake hawakuvunjika moyo. Waliendelea na kazi kwa uaminifu ingawa waliishi katika ulimwengu ambao ulizidi kuwashawishi waamini kwamba kazi yao kuu ya kujenga safina ilikuwa ya kipumbavu na haikuwa muhimu. Leo, familia za Kikristo zinaweza kujifunza mengi kutokana na imani ya Noa na familia yake. Tunaishi katika kipindi ambacho Biblia inakiita “siku za mwisho” za ulimwengu huu. (2 Tim. 3:1) Yesu alisema siku zetu zingekuwa kama kipindi ambacho Noa alijenga safina. Watu wasipopendezwa na ujumbe kuhusu Ufalme wa Mungu, tunapodhihakiwa, au kuteswa, tunapaswa kumkumbuka Noa. Zamani wengine pia walikabili matatizo kama hayo.

“Ingia Ndani ya Safina”

15. Noa alikabili misiba gani alipokaribia umri wa miaka 600?

15 Miaka ilipita na mwishowe safina ikakamilika. Noa alipokaribia umri wa miaka 600 alipoteza wapendwa wake. Baba yake, Lameki, alikufa. * Miaka mitano baadaye, Methusela aliyekuwa baba ya Lameki na babu ya Noa, alikufa akiwa na miaka 969, na ndiye mtu aliyeishi miaka mingi zaidi anayetajwa katika Biblia. (Mwa. 5:27) Methusela na Lameki waliishi kipindi kimoja na mwanamume wa kwanza, Adamu.

16, 17. (a) Noa alipokea ujumbe gani mpya alipokuwa na umri wa miaka 600? (b) Eleza jambo la kustaajabisha ambalo Noa na familia yake walijionea.

16 Akiwa na umri wa miaka 600, mzee wa ukoo Noa alipokea ujumbe huu kutoka kwa Yehova Mungu: “Ingia ndani ya safina, wewe pamoja na nyumba yako yote.” Wakati huohuo, Mungu akamwambia Noa aingize aina zote za wanyama ndani ya safina, saba saba walio safi, wanaofaa kutolewa dhabihu, na wengineo wawili wawili.—Mwa. 7:1-3.

17 Lilikuwa jambo la kustaajabisha. Wanyama walikuja kwa wingi, wakitembea, kupaa, na kutambaa, wadogo kwa wakubwa, wenye maumbo na tabia mbalimbali. Noa hakusumbuka kuwaelekeza na kuwakusanya ndani ya safina. Simulizi hilo linasema: “wakaingia . . . kwa Noa ndani ya safina.”—Mwa. 7:9.

18, 19. (a) Tunawezaje kujibu maswali ya wachambuzi wanaoshuku matukio ya simulizi la Noa? (b) Tunaonaje hekima ya Yehova katika njia aliyotumia kuwaokoa wanyama?

18 Huenda wachambuzi fulani wakauliza: ‘Jambo kama hilo lilitokeaje? Na wanyama hao wote wangeishije pamoja kwa amani ndani ya nafasi hiyo ndogo?’ Fikiria jambo hili: Je, Muumba wa ulimwengu wote angeshindwa kuwaongoza wanyama aliowaumba, hata kuwafanya wawe wapole na watulivu? Kumbuka Yehova ndiye Mungu aliyeumba wanyama. Baadaye, alitenganisha Bahari Nyekundu na akafanya jua lisimame. Je, angeshindwa kutimiza kila jambo linalotajwa katika simulizi la Noa? La hasha, hangeshindwa kamwe!

19 Ni kweli kwamba Yehova angeweza kuwaokoa wanyama kwa kutumia njia nyingine. Hata hivyo, kwa hekima alichagua njia ambayo inatukumbusha jukumu ambalo mwanzoni aliwapa wanadamu la kutunza viumbe wote walio hai duniani. (Mwa.1:28) Kwa hiyo leo, wazazi wengi hutumia simulizi la Noa kuwafundisha watoto wao kwamba Yehova anathamini watu na wanyama alioumba.

20. Huenda Noa na familia yake walifanya kazi gani juma la mwisho kabla ya Gharika?

20 Yehova akamwambia Noa kwamba Gharika ingekuja baada ya juma moja. Familia yake ilikuwa na kazi nyingi sana. Wazia kazi ya kukusanya na kupanga wanyama wote na vyakula vya wanyama na binadamu, kisha kuingiza vitu vingine ambavyo familia ingehitaji. Huenda mke wa Noa, wake za Shemu, Hamu, na Yafethi walijitahidi kutayarisha makao mazuri ndani ya safina.

21, 22. (a) Kwa nini hatushangai kujua kwamba watu katika siku za Noa hawakupendezwa na ujumbe wake? (b) Dhihaka kuelekea Noa na familia yake zilikoma wakati gani?

21 Namna gani watu waliowazunguka? Bado “hawakujali,” ingawa waliona Yehova akimbariki Noa na kazi yake. Walijionea wanyama wengi wakiingia ndani ya safina. Lakini hatushangai kwamba hawakujali. Vivyo hivyo, leo watu hawatambui uthibitisho ulio wazi kwamba tunaishi katika siku za mwisho za ulimwengu huu. Na kama mtume Petro alivyotabiri, wadhihaki wametokea na wanawadhihaki wale wanaotii onyo la Mungu. (Soma 2 Petro 3:3-6.) Hivyo ndivyo watu walivyomdhihaki Noa na familia yake.

22 Dhihaka hizo ziliisha wakati gani? Simulizi hilo linatuambia kwamba baada ya Noa kuingiza familia yake na wanyama ndani ya safina, “Yehova akafunga mlango nyuma yake.” Ikiwa wadhihaki fulani walikuwa karibu, bila shaka tendo hilo la Mungu liliwanyamazisha. La sivyo, walinyamazishwa na mvua, kwa sababu ilinyesha kwelikweli! Ilinyesha, ikanyesha, na ikaendelea kunyesha, mpaka dunia ikajaa mafuriko, kama vile Yehova alivyosema ingenyesha.—Mwa. 7:16-21.

23. (a) Tunajuaje kwamba Yehova hakufurahia kuona watu wakifa siku za Noa? (b) Kwa nini ni jambo la hekima kuiga imani ya Noa?

23 Je, Yehova alifurahia watu hao waovu walipokufa? La! (Eze. 33:11) Badala yake, alikuwa amewapa wakati wa kutosha kubadili njia zao na kufanya mema. Je, wangeweza kubadilika? Maisha ya Noa yanaonyesha kwamba wangeweza. Kwa kutembea pamoja na Yehova na kumtii Mungu wake katika mambo yote, Noa alionyesha kwamba wangeweza kuokoka. Kwa njia hiyo, imani yake ilihukumu ulimwengu wa siku hizo; ilifunua wazi uovu wa kizazi hicho. Imani yake ilimlinda yeye pamoja na familia yake. Ukionyesha imani kama ya Noa, wewe pia unaweza kujiokoa pamoja na wapendwa wako. Kama Noa, unaweza kutembea pamoja na Yehova Mungu akiwa rafiki yako. Na urafiki huo unaweza kudumu milele!

^ fu. 7 Siku hizo, watu waliishi miaka mingi sana kuliko tunavyoishi. Inaelekea ni kwa sababu waliishi kipindi kilichokuwa karibu zaidi na nguvu na ukamilifu ambao Adamu na Hawa walipoteza.

^ fu. 15 Lameki alikuwa amempa mwanaye jina Noa, ambalo huenda linamaanisha “Pumziko” au “Faraja,” na alikuwa ametabiri kwamba Noa angetimiza maana ya jina lake kwa kuwaongoza wanadamu kwenye pumziko ili wasisumbuke kwenye udongo uliolaaniwa. (Mwa. 5:28, 29) Lameki hakuona unabii huo ukitimizwa. Huenda mama ya Noa, ndugu, na dada zake waliangamizwa na Gharika.