Hamia kwenye habari

Kumtumikia Yehova Licha ya Hali Ngumu Nchini Venezuela

Kumtumikia Yehova Licha ya Hali Ngumu Nchini Venezuela

 Miaka ya hivi karibuni, nchi ya Venezuela imekumbwa na matatizo mengi kutia ndani matatizo ya kiuchumi. Shahidi anayeitwa Edgar anasema, “Ndani ya miaka michache, gharama ya kuishi ilipanda sana na tulihisi kana kwamba tulikuwa tumehamia nchi nyingine ingawa bado tulikuwa Venezuela!”

 Edgar anasema hivi: “Mimi na mke wangu, Carmen tulifikiria kuhusu mfano wa wamishonari ambao huhamia nchi ambazo hazina uwezo mkubwa wa kifedha na kujifunza kuishi bila huduma za msingi walizokuwa wamezoea. Jambo hilo lilitusaidia kurahisisha maisha yetu, na kujaribu mambo mapya kama vile kulima ili tupate chakula.”

Carmen na Edgar

 Lakini Edgar na Carmen hawakuishia hapo. Waliwatia moyo waamini wenzao kutia ndani wale waliokuwa wamevunjika moyo. (1 Wathesalonike 5:11) Edgar anasema hivi: “Hatukuwatia moyo tu, tuliwahimiza wawasaidie wengine, na hilo lingewaletea shangwe.”​—Matendo 20:35.

Bidii Katika Huduma Yazaa Matunda

 Janga la COVID-19 lilipoanza Argenis aliamua kuwahubiria watu wake wa ukoo. Baadhi yao walikubali kujifunza Biblia kupitia simu.

Argenis

 Argenis alitamani pia watu wake wa ukoo ambao hakuwa na Intaneti wanufaike na kusanyiko la eneo la 2020. Shahidi aliyekuwa akiishi katika mji jirani aliwapatia rekodi za programu hiyo. Watu wa ukoo wa Argenis waliazima TV kubwa na vikuza sauti. Argenis aliwapigia simu kabla ya programu kuanza ili asali pamoja nao. Kupitia jitihada za Argenis watu 4 wa ukoo na watu wengine 15 walifaulu kuhudhuria programu hiyo.

Wanachochewa na Imani na Upendo

 Jairo na Johana ni wenzi wa ndoa. Kutanikoni mwao ni wao pekee walio na gari, na wanalitumia kuwasaidia wengine kwa ukarimu. Changamoto wanayokabili ni uhaba wa petroli nchini humo. Jairo anasema, “Tunatumia saa nyingi, na wakati mwingine hata usiku mzima kwenye foleni tukisubiri kupata petroli.”

Johana na Jairo

 Jairo anahisi kwamba ni jambo muhimu kutumia gari lao kuwasaidia wengine. Anasema hivi: “Tunapowapelekea akina ndugu vitu, tunashangalia sana kuona wakitoa shukrani si kwetu sisi, bali kwa Yehova, ambaye huwapa watu wake yote wanayohitaji.​—2 Wakorintho 9:11, 14.

Kila Mtu Anaweza Kusaidia

 Ingawa dada anayeitwa Norianni alikuwa na miaka 28 alihisi kwamba yeye ana umri mdogo sana hivi kwamba hawezi kuwasaidia wengine. Hata hivyo alisoma andiko la 1 Timotheo 4:12 linalosema: “Usiruhusu kamwe mtu yeyote audharau ujana wako. Badala yake, uwe mfano mzuri kwa waaminifu.”

Norianni

 Andiko hilo lilimchochea Norianni kuwafikia watu wenye umri mkubwa katika kutaniko lao, na kuwasaidia wanapofanya utumishi wa kuandika barua na hata kuwaalika waandamane naye kwenye mafunzo yake ya Biblia. Pia aliwapigia simu na kuwatumia ujumbe wenye kutia moyo. Norianni anasema hivi: “Yehova amenionyesha kwamba ninaweza kufanya mengi.”

 Ndugu na dada zetu nchini Venezuela wanakabiliana na changamoto nyingi katika nyakati hizi ngumu. Hata hivyo, wanaendelea kuwa na bidii katika huduma na “wamekuwa chanzo cha faraja nyingi” kwa mmoja na mwenzake.​—Wakolosai 4:11; 2 Timotheo 4:2.