Hamia kwenye habari

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hawasherehekei Sikukuu Fulani?

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hawasherehekei Sikukuu Fulani?

 Mashahidi wa Yehova wanajuaje ikiwa sikukuu fulani inafaa?

 Kabla ya kuamua ikiwa watasherehekea sikukuu fulani, Mashahidi wa Yehova huchunguza Biblia. Baadhi ya sikukuu na sherehe zinavunja kanuni za Biblia waziwazi. Wanapogundua hivyo, Mashahidi wa Yehova hawashiriki sherehe hizo. Lakini kuhusu sikukuu nyingine, kila Shahidi anafanya uamuzi wake mwenyewe akijitahidi “kudumisha dhamiri safi mbele za Mungu na wanadamu.”​—Matendo 24:16.

 Yafuatayo ni baadhi ya maswali ambayo Mashahidi wa Yehova hujiuliza wanapoamua ikiwa watasherehekea sikukuu fulani. *

  •   Je, sikukuu hii inatokana na fundisho linalopingana na Maandiko?

     Kanuni ya Biblia: “‘Tokeni miongoni mwao na mjitenge,’ asema Yehova, ‘na mwache kugusa kitu kichafu.’”​—2 Wakorintho 6:​15-​17.

     Ili kujitenga kabisa na mafundisho yasiyo safi kiroho, yaani, yanayopingana na kile ambacho Biblia inasema, Mashahidi wa Yehova hawasherehekei sikukuu zinazohusisha mambo yafuatayo.

     Sikukuu zinazotegemea imani au ibada ya miungu mingine. Yesu alisema hivi: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.” (Mathayo 4:​10) Kwa sababu ya himizo hilo, Mashahidi wa Yehova hawasherehekei Krismasi, Ista, au May Day, kwa kuwa siku hizo zinatokana na ibada ya miungu mingine tofauti na Yehova. Kwa kuongezea, hawashiriki sikukuu kama hizi zifuatazo.

    •  Kwanzaa. Jina Kwanzaa “linatokana na maneno ya Kiswahili ‘matunda ya kwanza’ na [hilo] linaonyesha kwamba sikukuu hiyo inatokana na sherehe ya mavuno ya kwanza kuwahi kurekodiwa katika historia ya Afrika.” (Kitabu Encyclopedia of Black Studies) Ingawa watu fulani huona kwamba sherehe ya Kwanzaa si ya kidini, kitabu Encyclopedia of African Religion kinalinganisha sherehe hiyo ya Kiafrika na matunda ya kwanza “yanayotolewa kwa miungu na mababu ili kuwashukuru.” Kitabu hicho kinaendelea kusema hivi: “Ni roho hiyohiyo ya kutoa shukrani na kuonyesha uthamini kwa baraka ya uhai uliyopewa na mababu iliyochochea kuanzishwa kwa sikukuu ya Kwanzaa ya Wamarekani waliotoka Afrika.”

      Kwanzaa

    •  Sherehe ya Majira ya Vuli. Hii ni “sherehe ya kumheshimu mungu wa kike wa mwezi.” (Kitabu Holidays, Festivals, and Celebrations of the World Dictionary) Inatia ndani desturi “ya wanawake kumwinamia mungu huyo wa kike, inayoitwa kowtow katika Kichina.”​—Religions of the World​—A Comprehensive Encyclopedia of Beliefs and Practices.

    •  Nauruz (Nowruz). “Sikukuu hiyo inatokana na dini ya Zoastria na ni mojawapo ya siku takatifu zaidi katika kalenda ya kale ya Wazoroastria. . . . Roho ya Noon, inayoitwa [Rapithwin], ambaye anasemekana analazimishwa na Roho ya Baridi Kali kwenda chini ya ardhi wakati wa majira ya baridi kali, ilikaribishwa irudi tena kupitia sherehe hiyo wakati wa mchana siku ya Nowruz kulingana na utamaduni wa Zoroastria.”​—Shirika la Elimu, Sayansi, na Utamaduni la Umoja wa Mataifa.

    •  Shab-e Yalda. Kitabu Sufism in the Secret History of Persia kinasema kwamba sikukuu hiyo inayosherehekewa katika majira ya baridi kali katika siku ambayo mwangaza wa mchana unakuwepo kwa muda mfupi zaidi katika kizio cha kaskazini, “inahusiana kabisa na ibada ya Mithra,” mungu wa nuru. Pia, imependekezwa kwamba huenda sikukuu hiyo inahusiana na ibada ya mungu jua katika utamaduni wa Waroma na Wagiriki. *

    •  Sikukuu ya Kutoa Shukrani. Kama tu sikukuu ya Kwanzaa, sikukuu hiyo imetokana na sherehe za kale za mavuno zilizokusudiwa kuitukuza miungu mbalimbali. Baada ya muda, “utamaduni huo wa kale ulichukuliwa na kanisa la Kikristo.”​—Kitabu A Great and Godly Adventure​—The Pilgrims and the Myth of the First Thanksgiving.

     Sikukuu zinazohusiana na ushirikina au imani kuhusu bahati. Biblia inasema kwamba wale “wanaoandaa meza kwa ajili ya mungu wa Bahati Njema” ni “kati ya wale wanaomwacha Yehova.” (Isaya 65:11) Hivyo, Mashahidi wa Yehova hawasherehekei sikukuu zifuatazo:

    •  Ivan Kupala. Kitabu The A to Z of Belarus kinasema hivi: “Kulingana na maoni ya wengi, wakati wa [Ivan Kupala] nguvu za kichawi zinaachiliwa kutoka katika viumbe, na nguvu hizo zinaweza kupatikana kupitia ujasiri na bahati.” Mwanzoni, tukio hilo lilikuwa sikukuu ya kipagani iliyosherehekea siku ambayo mwangaza wa mchana ulikuwepo kwa muda mrefu zaidi katika kizio cha kaskazini. Hata hivyo, Encyclopedia of Contemporary Russian Culture inasema kwamba “baada ya wapagani kuukubali Ukristo sikukuu hiyo ilichanganywa na sikukuu ya Kanisa [“siku ya mtakatifu” Yohana Mbatizaji].”

    •  Mwaka Mpya wa Asia (Mwaka Mpya wa Wachina au Mwaka Mpya wa Wakorea). “Kuliko wakati mwingine wowote, huo ndio wakati wa mwaka ambapo familia, marafiki, na watu wa ukoo wanatafuta bahati maishani kwa kuzingatia miungu na mizimu, na kutaka ufanisi mwaka unaofuata.” (Kitabu Mooncakes and Hungry Ghosts​—Festivals of China) Kwa njia hiyohiyo, Mwaka Mpya wa Wakorea “unahusisha ibada ya mababu, desturi za kufukuza roho waovu na kutafuta bahati katika mwaka unaofuata, na [ubashiri] unatumiwa kujua jinsi Mwaka Mpya utakavyokuwa.”​—Kitabu Encyclopedia of New Year’s Holidays Worldwide.

      Mwaka Mpya wa Wachina

     Sikukuu zinazotokana na wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa. Biblia inaeleza wazi kwamba nafsi inaweza kufa. (Ezekieli 18:4) Hivyo, Mashahidi wa Yehova hawasherehekei sikukuu zinazotajwa hapa chini, ambazo zinaendeleza wazo la kwamba nafsi haiwezi kufa:

    •  Siku ya Wafu. Kulingana na New Catholic Encyclopedia, hii ni siku ya “kuwakumbuka waaminifu wote waliokufa. Muda wote wa Enzi ya Kati watu wengi waliamini kwamba nafsi zilizokuwa toharani zingerudi zikiwa mizuka, wachawi, vyura, n.k., na kuwatokea watu waliowakosea walipokuwa hai.”

    •  Qingming Festival (Ch’ing Ming) na Hungry Ghost Festival. Sikukuu hizo mbili zimekusudiwa kuwaheshimu mababu. Kitabu Celebrating Life Customs Around the World​—From Baby Showers to Funerals wakati wa Ch’ing Ming, “vyakula, vinywaji, na pesa zinateketezwa ili kuhakikisha wafu wasiwe na njaa au kiu na wasikose pesa.” Kitabu hicho pia kinasema kwamba “wakati wa Mwezi wa Mizimu Yenye Njaa, hasa usiku wa mwezi mpevu, [wanaosherehekea wanaamini] kuna uhusiano mkubwa kati ya wafu na watu wanaoishi kuliko usiku mwingine wowote, hivyo, ni muhimu kuchukua tahadhari ili kuwatuliza wafu na kuwaheshimu mababu.”

    •  Chuseok. Kitabu The Korean Tradition of Religion, Society, and Ethics kinasema kwamba sherehe hiyo inatia ndani “kutoa chakula na divai kwa nafsi zilizokufa.” Matoleo hayo yanaonyesha “imani ya kwamba nafsi inaendelea kuishi baada ya mwili kufa.”

     Sikukuu zinazohusiana na uchawi. Biblia inasema hivi: “Mtu yeyote anayefanya uaguzi, mtu yeyote anayefanya uchawi, mtu yeyote anayetafuta ishara za ubashiri, mlozi, mtu yeyote anayewafunga wenzake kwa uchawi, mtu yeyote anayetafuta ushauri kutoka kwa watu wanaowasiliana na roho, mpiga ramli, au mtu yeyote anayetafuta habari kuhusu wafu . . . ni chukizo kwa Yehova.” (Kumbukumbu la Torati 18:10-​12) Ili kuepuka uchawi wowote​—kutia ndani unajimu (kutafuta habari kuhusu wakati ujao)​—Mashahidi wa Yehova hawasherehekei Halloween au sikukuu zifuatazo:

    •  Mwaka Mpya wa Sinhala na Tamil. “Mazoea yanayohusiana na tukio hilo . . . yanatia ndani kufanya mambo fulani kwa kutegemea wakati ulioamuliwa kupitia unajimu.”​—Kitabu Encyclopedia of Sri Lanka.

    •  Songkran. Jina la sikukuu hii ya Kiasia “limetokana na neno la Kisanskriti . . . linalomaanisha ‘mwendo’ au ‘mabadiliko,’ na [sikukuu hiyo] inasherehekea kusonga kwa jua kuelekea alama ya unajimu ya Aries.”​—Kitabu Food, Feasts, and Faith​—An Encyclopedia of Food Culture in World Religions.

     Sikukuu zilizokuwa sehemu ya Sheria ya Musa, ambazo ziliisha baada ya Yesu kutoa dhabihu. Biblia inasema hivi: “Kristo ndiye mwisho wa Sheria.” (Waroma 10:4) Wakristo bado wananufaika na kanuni za Sheria ya Musa ambayo Waisraeli wa kale walitumia. Hata hivyo, hawasherehekei sikukuu zake, hasa sikukuu ambazo zilielekeza kwenye Masihi ambaye Wakristo wanaamini alishakuja. Biblia inasema kwamba “mambo hayo ni kivuli cha mambo yanayokuja, bali uhalisi ni wa Kristo.” (Wakolosai 2:​17) Kwa sababu hiyo, na kwa kuwa baadhi ya sikukuu hizo zimehusisha mazoea yasiyo ya kimaandiko, sikukuu zifuatazo ni baadhi ya zile ambazo Mashahidi wa Yehova hawasherehekei:

    •  Hanukkah. Sikukuu hii ni ya kuadhimisha kuwekwa wakfu tena kwa hekalu la Wayahudi jijini Yerusalemu. Lakini Biblia inasema kwamba Yesu alikuja kuwa Kuhani Mkuu wa “hema [au, hekalu] kubwa na kamilifu zaidi ambalo halikutengenezwa kwa mikono, yaani, si la uumbaji huu.” (Waebrania 9:​11) Kwa Wakristo, hekalu hilo la kiroho lilichukua mahali pa hekalu lililokuwa Yerusalemu.

    •  Rosh Hashanah. Hii ni siku ya kwanza ya mwaka wa Wayahudi. Katika nyakati za kale, sikukuu hiyo ilihusisha kumtolea Mungu dhabihu za pekee. (Hesabu 29:​1-6) Hata hivyo, Yesu Kristo, akiwa Masihi, “[alikomesha] dhabihu na toleo la zawadi,” na kufanya zisiwe na thamani machoni pa Mungu.​—Danieli 9:​26, 27.

  •   Je, sikukuu hiyo inahusisha kuchanganya dini?

     Kanuni ya Biblia: “Mwamini ana ushirika gani na mtu asiye mwamini? Na hekalu la Mungu lina makubaliano gani na sanamu?”​—2 Wakorintho 6:​15-​17.

     Ingawa Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kuishi kwa amani na majirani wao na wanaheshimu haki ya kila mtu ya kuchagua atakachoamini, wanaepuka sherehe ambazo zinahusisha kuchanganya imani katika njia zifuatazo.

     Kusherehekea mtu anayeheshimiwa na dini fulani au matukio ambayo yanatia moyo watu wa dini mbalimbali waabudu pamoja. Mungu alipowaelekeza watu wake wa kale kwenye nchi mpya ambako wakaaji walishiriki dini nyingine, aliwaambia hivi: “Hampaswi kufanya agano pamoja nao wala na miungu yao. . . . Mkiiabudu miungu yao, kwa hakika itakuwa mtego kwenu.” (Kutoka 23:32, 33) Hivyo, Mashahidi wa Yehova hawashiriki sikukuu kama zifuatazo.

    •  Loy Krathong. Katika sikukuu hii ya Thai, “watu hutengeneza mabakuli wakitumia majani, wanaongeza mishumaa au vijiti vya ubani, na kuyaachilia mabakuli hayo yaelee majini. Mashua hizo zinasemekana kuondoa bahati mbaya. Lakini katika maana halisi, sikukuu hiyo inatumiwa kukumbuka alama ya nyayo za miguu iliyoachwa na Budha.”​—Kitabu Encyclopedia of Buddhism.

    •  Siku ya Kitaifa ya Kutubu. Kulingana na ofisa mmoja wa serikali aliyenukuliwa katika gazeti The National nchini Papua New Guinea, wale wanaoshiriki tukio hilo “wanakubali mambo ya msingi ya imani ya Kikristo.” Anasema kwamba siku hiyo ndiyo “chanzo cha kanuni za Kikristo nchini.”

    •  Vesak. “Hii ndiyo siku takatifu zaidi ya Wabudha kwani wanasherehekea kuzaliwa kwa Budha, kupata kwake ujuzi, na kifo chake, au jinsi alivyofikia Nirvana.”​—Kitabu Holidays, Festivals, and Celebrations of the World Dictionary.

      Vesak

     Sikukuu zinazotokana na mazoea ya kidini ambayo hayafundishwi na Biblia. Yesu aliwaambia hivi viongozi wa kidini: “Mmelibatilisha neno la Mungu kwa sababu ya mapokeo yenu.” Pia alisema kwamba ibada yao ilikuwa ya bure kwa kuwa walifundisha “amri za wanadamu kuwa mafundisho.” (Mathayo 15:​6, 9) Kwa sababu Mashahidi wa Yehova wanachukua onyo hilo kwa uzito, kuna sherehe nyingi za kidini ambazo hawasherehekei.

    •  Epiphany (Three Kings’ Day, Timkat, au Los Reyes Magos). Wanaoisherehekea wanaadhimisha pindi ambapo wanajimu walimtembelea Yesu au ubatizo wa Yesu. Sikukuu hiyo “ilibadili sherehe fulani za kipagani za majira ya kuchipua ziwe za Kikristo, sherehe ambazo ziliheshimu miungu ya maji yanayotiririka, mito, na vijito.” (Kitabu The Christmas Encyclopedia) Timkat, sikukuu inayohusiana na hiyo, “ina chanzo chake katika mambo ya kitamaduni.”​—Kitabu Encyclopedia of Society and Culture in the Ancient World.

    •  Sherehe ya Kupaa kwa Bikira Maria. Sikukuu hiyo inasherehekea imani ya kwamba mama ya Yesu alipaa kwenda mbinguni akiwa na mwili wa nyama na damu. Kitabu Religion and Society​—Encyclopedia of Fundamentalism kinasema kwamba “imani hiyo haikujulikana na kanisa la awali na hairejelewi katika Maandiko.”

    •  Sherehe ya Kutungwa Mimba Bila Dhambi. “Wazo la kwamba [Maria] alichukuliwa mimba bila dhambi halifundishwi waziwazi katika Maandiko . . . Ni fundisho la Kanisa.”​—Kitabu New Catholic Encyclopedia.

    •  Kwaresima. Kulingana na kitabu New Catholic Encyclopedia, kipindi hicho cha kutubu na kufunga kilianzishwa “katika karne ya nne,” miaka zaidi ya 200 baada ya uandikaji wa Biblia kukamilishwa. Ensaiklopedia hiyo inasema hivi kuhusu siku ya kwanza ya Kwaresima: “Zoea la waaminifu kupokea majivu siku ya Jumatano ya Majivu limekuwepo tangu Baraza la Benevento mwaka wa 1091.”

    •  Meskel (au, Maskal). Kitabu Encyclopedia of Society and Culture in the Medieval World kinasema kwamba sikukuu hiyo inayofanywa nchini Ethiopia inasherehekea “kupatikana kwa Msalaba wa Kweli (msalaba ambao Kristo alisulubiwa), kwa kuwasha moto na kucheza dansi kuuzunguka.” Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova hawatumii msalaba katika ibada yao.

  •   Je, sikukuu hiyo inamtukuza mwanadamu fulani, shirika, au nembo ya kitaifa?

     Kanuni ya Biblia: “Yehova anasema hivi: ‘Amelaaniwa mtu anayewatumaini wanadamu, anayetegemea nguvu za wanadamu, na ambaye moyo wake unamwacha Yehova.’”​—Yeremia 17:5.

     Ingawa Mashahidi wa Yehova wanawathamini wanadamu wenzao na hata kusali kwa ajili yao, hawashiriki matukio na sherehe kama zifuatazo:

     Sikukuu zinazomtukuza mtawala au mtu fulani mashuhuri. Biblia inasema hivi: “Kwa faida yenu wenyewe, acheni kumtumaini mwanadamu, ambaye ni pumzi tu iliyo katika mianzi ya pua yake. Kwa nini afikiriwe?” (Isaya 2:​22) Hivyo, Mashahidi wa Yehova hawashiriki mambo kama kukumbuka siku ya kuzaliwa kwa mtawala wa nchi yao.

     Kusherehekea bendera ya taifa. Mashahidi wa Yehova hawasherehekei Siku ya Bendera. Kwa nini? Kwa sababu Biblia inasema hivi: “Jiepusheni na sanamu.” (1 Yohana 5:​21) Watu fulani leo hawaioni bendera kuwa sanamu​—kitu kinachoabudiwa​—lakini mwanahistoria Carlton J. H. Hayes aliandika hivi: “Leo, ishara kuu ya uzalendo ambayo huabudiwa na wengi ni bendera.”

     Sikukuu au sherehe zinazomtukuza mtakatifu. Ni nini kilichotokea mtu anayemwogopa Mungu alipomwinamia mtume Petro? Biblia inasema hivi: “Petro akamwinua, akisema: ‘Simama; mimi pia ni mwanadamu tu.’” (Matendo 10:25, 26) Kwa kuwa Petro na mitume wengine walikataa kupewa heshima ya pekee au kuabudiwa, Mashahidi wa Yehova hawashiriki katika matukio yanayowaheshimu wale wanaoonwa kuwa watakatifu, kama sikukuu zifuatazo:

    •  Siku ya Watakatifu Wote. “Sikukuu inayowaheshimu watakatifu wote . . . Vyanzo vya sherehe hiyo havijulikani.”​—Kitabu New Catholic Encyclopedia.

    •  Sikukuu ya Bikira wa Guadalupe. Sikukuu hiyo ni ya kumheshimu “mtakatifu anayeilinda nchi ya Mexico,” ambaye anaaminiwa kuwa Maria, mama ya Yesu. Inasemekana kwamba alimtokea kimuujiza maskini fulani mwaka wa 1531.​—Kitabu The Greenwood Encyclopedia of Latino Literature.

      Sikukuu ya Bikira wa Guadalupe

    •  Siku ya Jina. Kitabu Celebrating Life Customs Around the World​—From Baby Showers to Funerals kinasema kwamba “hiyo ni siku ya kusherehekea mtakatifu ambaye mtoto amepewa jina lake wakati wa ubatizo au wa kipa-imara.” Inaendelea kusema kwamba kuna “uhusiano mkubwa wa kidini na siku hiyo.”

     Sikukuu za kisiasa au mapinduzi katika jamii. Biblia inasema hivi: “Ni bora kumkimbilia Yehova kuliko kuwatumaini wanadamu.” (Zaburi 118:​8, 9) Ili Mashahidi wa Yehova waepuke kuonyesha kwamba wanawategemea wanadamu badala ya Mungu kusuluhisha matatizo ya ulimwengu, hawajiungi na sherehe za Siku ya Vijana au Siku ya Wanawake ambazo zinaunga mkono kampeni za kisiasa au za kijamii. Kwa sababu hiyohiyo, hawajiungi na sherehe za Siku ya Kukomesha Utumwa au sherehe nyingine kama hizo. Badala yake, wanasubiri wakati ambapo Ufalme wa Mungu utasuluhisha matatizo ya ubaguzi wa rangi na ukosefu wa usawa.​—Waroma 2:​11; 8:​21.

  •   Je, sikukuu hiyo inainua taifa moja au kabila juu ya lingine?

     Kanuni ya Biblia: “Mungu hana ubaguzi, lakini katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.”​—Matendo 10:34, 35.

     Ingawa Mashahidi wengi wa Yehova wanapenda nchi zao, wanaepuka sherehe zinazotukuza mataifa au makabila katika njia zinazotajwa katika orodha ifuatayo.

     Matukio yanayotukuza jeshi. Badala ya kupendekeza vita, Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.” (Mathayo 5:​44) Hivyo, Mashahidi wa Yehova hawasherehekei sikukuu zinazowatukuza wanajeshi, kutia ndani sikukuu zifuatazo:

    •  Siku ya Anzac. “Anzac inamaanisha Majeshi ya Australia na New Zealand,” na “Siku ya Anzac imegeuka hatua kwa hatua na kuwa siku ya kuwakumbuka wale waliofia vitani.”​—Kitabu Historical Dictionary of Australia.

    •  Veterans Day (Siku ya Kumbukumbu, Jumapili ya Kumbukumbu, Siku ya Ukumbusho). Sikukuu hizo zinawatukuza “wanajeshi na wale waliofia vitani.”​—Kitabu Encyclopædia Britannica.

     Sikukuu ya kukumbuka historia ya taifa au jinsi ilivyoanza kujitawala. Yesu alisema hivi kuhusu wafuasi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16) Ingawa wanafurahia kujua historia ya nchi, Mashahidi wa Yehova wanajitenga na matukio kama yafuatayo:

    •  Siku ya Australia. Kulingana na Worldmark Encyclopedia of Cultures and Daily Life, sikukuu hiyo inasherehekea “siku ambayo wanajeshi Waingereza walipandisha bendera yao mwaka wa 1788 na kutangaza Australia kuwa koloni yao.”

    •  Siku ya Guy Fawkes. Hiyo ni “siku ya kitaifa ya kusherehekea na kukumbuka jinsi Guy Fawkes na Wakatoliki wengine wenye maoni kama yake walivyoshindwa kuteketeza Mfalme James wa Kwanza na Bunge la [Uingereza] mwaka wa 1605.”​—Kitabu A Dictionary of English Folklore.

    •  Siku ya Uhuru. Katika nchi kadhaa, hiyo ni “siku iliyotengwa kwa ajili ya kusherehekea siku ambayo nchi ilipata uhuru.”​—Kitabu Merriam-Webster’s Unabridged Dictionary.

  •   Je, sikukuu hiyo inahusisha kutenda bila kujidhibiti na kuwa na maadili mapotovu?

     Kanuni ya Biblia: “Wakati uliopita uliwatosha kufanya mapenzi ya mataifa, mlipofanya vitendo vya mwenendo mpotovu, uchu, kunywa kupita kiasi, karamu zenye vurugu, mashindano ya kunywa, na ibada za sanamu zenye kuchukiza.”​—1 Petro 4:3.

     Kupatana na kanuni hiyo, Mashahidi wa Yehova wanaepuka sherehe zinazohusisha kunywa kupita kiasi na karamu zilizopita kiasi. Mashahidi wa Yehova wanafurahia kuwa pamoja na rafiki zao, na huenda wakachagua kutumia kileo kwa usawaziko. Wanajitahidi kadiri wawezavyo kufuata shauri hili la Biblia: “Iwe mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”​—1 Wakorintho 10:31.

     Hivyo, Mashahidi wa Yehova hawashiriki sherehe za carnival au sherehe nyingine kama hizo zinazohusisha mwenendo mpotovu unaoshutumiwa katika Biblia. Sherehe hizo zinatia ndani sherehe ya Kiyahudi ya Purimu. Ingawa kwa muda mrefu sherehe hiyo ilikusudiwa kukumbuka jinsi Wayahudi walivyookolewa katika karne ya tano K.W.K., kitabu Essential Judaism kinasema kwamba kwa sasa inaweza “kufafanuliwa kuwa njia ya Wayahudi ya kusherehekea Mardi Gras au Carnival.” Kwa wengi wanaoisherehekea, “inahusisha kuvaa mavazi ya pekee (mara nyingi wanaume wanavaa nguo za wanawake), mwenendo unaoonyesha uasi, kunywa kupita kiasi, na kupiga kelele sana.”

 Je, Mashahidi wa Yehova wanapenda familia zao licha ya kwamba hawasherehekei sikukuu fulani?

 Ndiyo. Biblia inawafundisha watu wawapende na kuwaheshimu washiriki wote wa familia licha ya imani yao. (1 Petro 3:​1, 2, 7) Bila shaka, Shahidi wa Yehova anapoacha kushiriki katika sherehe fulani, huenda watu fulani wa ukoo wakakasirika, wakaumia kihisia, au wakahisi wamesalitiwa. Hivyo, Mashahidi wa Yehova wanachukua hatua ya kwanza kuwahakikishia watu wa familia kwamba wanawapenda, kuwaeleza kwa busara sababu zilizofanya waamue hivyo, na kuwatembelea watu wa ukoo katika pindi nyingine.

 Je, Mashahidi wa Yehova wanawaambia watu wengine wasisherehekee sikukuu?

 Hapana. Wanaamini kwamba kila mtu anapaswa kufanya uamuzi wake mwenyewe. (Yoshua 24:15) Mashahidi wa Yehova “[wanawaheshimu] watu wa namna zote” haidhuru wana imani gani ya kidini.​—1 Petro 2:​17.

^ Makala hii haitaji sikukuu zote ambazo Mashahidi wa Yehova wanajiepusha nazo, wala haitaji kanuni zote za Biblia zinazoweza kutumiwa.

^ Mithra, Mithraism, Christmas Day & Yalda, cha K. E. Eduljee, ukurasa wa 31-33.