Hamia kwenye habari

Je, Mashahidi wa Yehova Hutoa Misaada Wakati wa Misiba?

Je, Mashahidi wa Yehova Hutoa Misaada Wakati wa Misiba?

 Ndiyo, Mashahidi wa Yehova huwasaidia watu misiba inapotokea. Sisi hutoa msaada kwa Mashahidi na watu ambao si Mashahidi kulingana na agizo linalopatikana kwenye Wagalatia 6:10: “Tuwatendee wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” Sisi pia hujitahidi kuwasaidia waathiriwa kihisia na kiroho, msaada ambao wao huhitaji sana wakati huo.—2 Wakorintho 1:3, 4.

Mipango

 Msiba unapotokea, wazee wa makutaniko yaliyo katika eneo lililokumbwa na msiba huo hujaribu kuwasiliana na washiriki wa makutaniko yao ili kuona ikiwa wako salama na kujua wanahitaji msaada wa aina gani. Kisha wazee hao hueleza ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova inayosimamia eneo hilo kuhusu matokeo ya uchunguzi wao na msaada ambao wametoa.

 Ikiwa makutaniko katika eneo hilo hayawezi kutoa msaada unaohitajiwa, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova hufanya mipango ili kutoa msaada huo. Utaratibu huo unapatana na utaratibu ambao Wakristo wa karne ya kwanza walifuata ili kutunzana wakati wa njaa kubwa. (1 Wakorintho 16:1-4) Ofisi ya tawi inayosimamia eneo hilo huteua Halmashauri za Kutoa Misaada zitakazopanga na kuelekeza kazi hiyo. Mashahidi kutoka maeneo mengine hutumia wakati na mali zao kusaidia.—Methali 17:17.

Jinsi Misaada Inavyogharimiwa

 Njia moja ya kutumia michango inayotumwa kwenye ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova ni kuwasaidia wale waliokumbwa na misiba. (Matendo 11:27-30; 2 Wakorintho 8:13-15) Kwa kuwa kazi hiyo hufanywa na wajitoleaji wasiolipwa, pesa zilizochangwa hutumiwa hasa kutoa msaada na si kuwalipa watu. Sisi hutumia michango yote kwa uangalifu.—2 Wakorintho 8:20.