Ni Nini Kilichowapata Mashahidi wa Yehova Wakati wa Yale Maangamizi Makubwa ya Wanazi?
Kati ya Mashahidi 35,000 wa Yehova waliokuwa wakiishi nchini Ujerumani na katika nchi zilizokuwa chini ya Wanazi, Mashahidi 1,500 hivi walikufa wakati wa yale Maangamizi Makubwa ya Wanazi. Haijulikani walikufa kwa njia gani katika visa vyote. Kwa kuwa bado utafiti unaendelea, huenda tarakimu na habari nyingine zikabadilishwa wakati ujao.
Walikufa kwa njia gani?
Mauaji: Karibu Mashahidi 400 hivi waliuawa nchini Ujerumani na katika nchi nyingine zilizokuwa chini ya Wanazi. Wengi kati ya waliouawa walifikishwa mahakamani, wakahukumiwa kifo, na kuuawa kwa kukatwa vichwa. Wengine walipigwa risasi au kunyongwa bila kufikishwa mahakamani.
Hali mbaya sana kifungoni: Zaidi ya Mashahidi 1,000 walikufa katika kambi za mateso za Wanazi na katika magereza. Walifanyishwa kazi hadi wakafa au walikufa kwa sababu ya kuteswa, kunyimwa chakula, kuwekwa katika baridi kali, magonjwa, au ukosefu wa matibabu. Kwa sababu ya kutendewa vibaya sana, wengine walikufa upesi baada ya kuachiliwa mwishoni mwa Vita vya Pili vya Ulimwengu.
Sababu nyingine: Baadhi ya Mashahidi waliuawa katika vyumba vya gesi, wakafa kwa kutumiwa kufanyia majaribio hatari ya kitiba, au kwa kudungwa sindano zilizokuwa na dawa ya kuua.
Kwa nini waliteswa?
Mashahidi wa Yehova waliteswa kwa sababu ya kushikamana na mafundisho ya Biblia. Serikali ya Wanazi ilipodai kwamba Mashahidi wafanye kile ambacho Biblia inakataza, Mashahidi walikataa. Walichagua ‘kumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.’ (Matendo 5:29) Fikiria masuala mawili ambayo walifanya hivyo.
Kutounga mkono upande wowote wa mambo ya kisiasa. Kama tu Mashahidi wa Yehova katika nchi zote leo, Mashahidi walioishi chini ya utawala wa Wanazi hawakuunga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa. (Yohana 18:36) Hivyo, walikataa
Kutumikia jeshini au kufanya kazi yoyote iliyohusiana na vita.—Isaya 2:4; Mathayo 26:52.
Kupiga kura wakati wa uchaguzi au kujiunga na mashirika ya Wanazi.—Yohana 17:16.
Kuisalimu bendera yenye alama ya Wanazi (swastika) au kusema “Hitler Atukuzwe!” (Heil Hitler).—Mathayo 23:10; 1 Wakorintho 10:14.
Kuendeleza ibada yao. Licha ya kuzuiwa kufanya ibada yao, Mashahidi wa Yehova waliendelea
Kukutana kwa ajili ya sala na ibada.—Waebrania 10:24, 25.
Kuhubiri ujumbe wa Biblia na kusambaza machapisho yanayotegemea Biblia.—Mathayo 28:19, 20.
Kuwaonyesha majirani wao fadhili, kutia ndani Wayahudi.—Marko 12:31.
Kushikamana na imani, walikataa kutia sahihi hati ya kukana imani yao.—Marko 12:30.
Profesa Robert Gerwarth anafikia mkataa kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa “kikundi pekee katika utawala wa Nazi kuteswa kwa sababu ya imani yao ya kidini tu.” * Wafungwa wengine katika kambi za mateso waliwaheshimu Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya msimamo wao imara. Mfungwa mmoja Mwaustralia alisema hivi: “Hawaendi vitani. Wako tayari kuuawa ili wasimuue mtu yeyote.”
Walifia wapi?
Kambi za mateso: Idadi kubwa ya Mashahidi wa Yehova walikufa katika kambi za mateso. Walifungwa katika kambi kama vile Auschwitz, Buchenwald, Dachau, Flossenbürg, Mauthausen, Neuengamme, Niederhagen, Ravensbrück, na Sachsenhausen. Imethibitishwa kwamba karibu Mashahidi 200 wa Yehova waliuawa katika kambi ya Sachsenhausen pekee.
Magereza: Baadhi ya Mashahidi waliteswa hadi kufa katika magereza. Wengine walikufa kwa sababu ya majeraha waliyopata walipokuwa wakihojiwa.
Mahali walipouawa: Mashahidi wa Yehova waliuawa hasa katika magereza ya Berlin-Plötzensee, Brandenburg, na Halle/Saale. Mbali na maeneo hayo kuna maeneo mengine 80 hivi ambako imethibitishwa kuwa Mashahidi waliuawa.
Baadhi ya waliouawa
Jina: Helene Gotthold
Mahali alipouawa: Plötzensee (Berlin)
Helene, mke na mama ya watoto wawili, alikamatwa mara kadhaa. Katika mwaka wa 1937, alitendewa vibaya sana hivi kwamba pindi moja alipokuwa akihojiwa mimba aliyokuwa amebeba iliharibika. Desemba 8, 1944, aliuawa kwa kukatwa kichwa katika gereza la Plötzensee, Berlin.
Jina: Gerhard Liebold
Mahali alipouawa: Brandenburg
Gerhard aliyekuwa na umri wa miaka 20 aliuawa kwa kukatwa kichwa Mei 6, 1943, miaka miwili baada ya baba yake kukatwa kichwa katika gereza hilohilo. Aliandika maneno haya katika barua ya kuiaga familia yake na mchumba wake: “Bila nguvu za Bwana, nisingeweza kutembea katika njia hii.”
Jina: Rudolf Auschner
Mahali alipouawa: Halle/Saale
Rudolf alikuwa na umri wa miaka 17 tu alipouawa kwa kukatwa kichwa Septemba 22, 1944. Aliandika hivi katika barua ya kumuaga mama yake: “Ndugu wengi wameuawa kwa njia hii, nami pia nitauawa vivyo hivyo.”
^ Hitler’s Hangman: The Life of Heydrich, ukurasa wa 105.