Hamia kwenye habari

Je, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Ni Sahihi?

Je, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya Ni Sahihi?

 Sehemu ya kwanza ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa mwaka wa 1950. Tangu wakati huo, watu fulani wametoa maoni mbalimbali kuhusu usahihi wa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya * kwa sababu inatofautiana na tafsiri nyingine za Biblia katika sehemu mbalimbali. Hata hivyo mambo yafuatayo yanaweza kutusaidia kuelewa kwa nini kuna tofauti hizo.

  •   Inategemeka. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inategemea utafiti wa karibuni zaidi unaotegemea hati za zamani zaidi zenye kutegemeka. Tofauti na hilo, tafsiri ya Biblia ya King James Version chapa ya mwaka wa 1611 ilitegemea hati ambazo hazikuwa sahihi kabisa na ambazo hazikuwa za kale kama zile zilizotumiwa kutokeza Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

  •   Inaaminika. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inawasilisha kwa uaminifu ujumbe ule wa awali kabisa ulioongozwa na roho ya Mungu. (2 Timotheo 3:​16) Badala ya kuwasilisha ujumbe wa Mungu kwa uaminifu, tafsiri nyingi za Biblia zinapotosha ujumbe huo kwa kufuata mapokeo ya wanadamu kama vile kuliondoa jina la kibinafsi la Mungu, Yehova, na kuweka jina la cheo Bwana au Mungu, mahali pa jina hilo.

  •   Neno kwa neno. Tofauti na tafsiri nyinginezo ambazo hutaja tu maana ya ujumbe, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imetafsiri maneno kihalisi maadamu kufanya hivyo hakufanyi maneno yasieleweke wala hakufichi maana ya ujumbe wa awali uliokusudiwa. Tafsiri zinazotaja tu maana ya ujumbe wa awali wa Biblia zinaweza kuwa na kasoro kwa sababu huenda zikawa na maoni ya mtu binafsi au hata zikakosa habari fulani muhimu.

Tofauti iliyo kati ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya na tafsiri nyinginezo

 Kukosekana kwa vitabu vingine. Katika Biblia ya Kikatoliki na ya makanisa ya Othodoksi ya Mashariki, kuna vitabu vinavyoitwa na watu wengine vitabu vya Apokrifa. Hata hivyo, vitabu hivyo havikuwa miongoni mwa vitabu vilivyokubaliwa katika mapokeo ya Kiyahudi na ni vyema kuzingatia jambo hilo kwani Biblia yenyewe inasema kuwa Wayahudi “walikabidhiwa maneno matakatifu ya Mungu.” (Waroma 3:​1, 2) Kwa sababu hiyo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya na tafsiri nyingi za Biblia za kisasa hazina vitabu vya Apokrifa.

 Mistari inayokosekana. Tafsiri nyingine za Biblia zimeongezea vifungu vya maneno na mistari ambayo haipo katika hati za kale zaidi zilizopo za Biblia, lakini Tafsiri ya Ulimwengu Mpya haina vifungu hivyo vya maneno au mistari hiyo ya ziada. Tafsiri nyingi za kisasa za Biblia pia zimeondoa habari hiyo iliyoongezwa au zimetoa maelezo kwamba mistari au vifungu hivyo vya maneno haviungwi mkono na vyanzo vyenye kutegemeka zaidi.

 Maneno tofauti. Nyakati nyingine, ujumbe uliotafsiriwa neno kwa neno unaweza kukosa kueleweka vizuri au hata unaweza kumpotosha mtu. Kwa mfano, maneno ya Yesu kwenye Mathayo 5:3 hutafsiriwa hivi mara nyingi: ‘Heri walio maskini wa roho.’ (Union Version; Zaire Swahili Bible; Neno Biblia Takatifu; Biblia ya Kiafrika; Biblia Habari Njema) Watu wengi hawaelewi tafsiri hiyo ya moja kwa moja ya maneno “maskini wa roho,” hali wengine wanafikiri kwamba Yesu alikuwa akikazia umuhimu wa kuwa mnyenyekevu au maskini. Kinyume na hilo, Yesu alifundisha kwamba furaha ya kweli inatokana na kutambua kwamba tunahitaji kuongozwa na Mungu. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inawasilisha maana hiyo kwa usahihi inapotumia maneno “wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”​—Mathayo 5:3. *

Maelezo mazuri kutoka kwa wasomi ambao si Mashahidi kuhusu Biblia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya

  •   Katika barua ya Desemba 8, 1950, msomi maarufu na mtafsiri wa Biblia Edgar J. Goodspeed aliandika hivi kuhusu Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo: “Ninapendezwa na kazi ya watu wenu, na jinsi ambavyo imeenea ulimwenguni kote, na ninapendezwa sana na tafsiri yenu huru, wazi na dhahiri. Ina ujuzi mwingi mno, kama niwezavyo kushuhudia.”

    Edgar J. Goodspeed

  •   Profesa Allen Wikgren wa Chuo Kikuu cha Chicago aliitaja Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kama kielelezo cha tafsiri iliyoandikwa kwa lugha ya kisasa na haitegemei tafsiri nyinginezo. Alisema hivi waziwazi kuihusu: “Ujumbe wake hautegemei tafsiri nyinginezo.”​—The Interpreter’s Bible, Buku la I, ukurasa wa 99.

  •   Akizungumza kuhusu Biblia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, Alexander Thomson, mchambuzi wa Biblia kutoka Uingereza aliandika hivi: “Bila shaka, tafsiri hiyo ni kazi ya wasomi wenye ustadi na wenye akili, ambao wamejaribu kuwasilisha maana kamili ya maandishi ya Kigiriki kwa kadiri ambavyo lugha ya Kiingereza inaweza kuwasilisha.”​—The Differentiator, Aprili 1952, ukurasa wa 52.

  •   Hata ingawa mwandishi wa vitabu Charles Francis Potter alisema kwamba aliona maneno fulani yasiyo ya kawaida katika tafsiri hiyo, mwandishi huyo alitaja hivi waziwazi: “Watafsiri hao tusiowajua waliwasilisha kwa njia bora kabisa maana ya Kigiriki na Kiebrania, walikuwa wasomi stadi na wenye uwezo wa kiwango cha juu.”​—The Faiths Men Live By, ukurasa wa 300.

  •   Ingawa alihisi kwamba Biblia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilikuwa na maneno au vifungu vya maneno visivyo vya kawaida na vilevile mambo fulani yanayochangia ubora wake, Robert M. McCoy alikamilisha uchunguzi wake kwa kusema: “Kutafsiriwa kwa Agano Jipya ni uthibitisho wa kuwepo kwa wasomi katika kikundi hicho, [Mashahidi wa Yehova] wasomi ambao wana uwezo wa kushughulikia matatizo yanayohusiana na kutafsiri Biblia kwa busara.”​—Andover Newton Quarterly, Januari 1963, ukurasa wa 31.

  •   Ingawa Profesa S. MacLean Gilmour hakubaliani na jinsi maneno mengine yalivyotafsiriwa katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, alisema kwamba watafsiri waliotumiwa kuitafsiri, walikuwa na “ufahamu usio wa kawaida wa lugha ya Kigiriki.”​—Andover Newton Quarterly, Septemba 1966, ukurasa wa 26.

  •   Katika uchunguzi wake wa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inayofanyiza sehemu ya Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures, Profesa Thomas N. Winter aliandika hivi: “Tafsiri hiyo iliyotokezwa na halmashauri ya watu ambao majina yao hayajulikani, ni tafsiri sahihi kabisa na ya kisasa.”​—The Classical Journal, Aprili-Mei 1974, ukurasa wa 376.

  •   Profesa Benjamin Kedar-Kopfstein, msomi wa Kiebrania nchini Israel, alisema hivi mwaka wa 1989: “Katika utafiti wangu wa lugha unaohusu Biblia ya Kiebrania na tafsiri mbalimbali, mara nyingi mimi hurejezea chapa ya Kiingereza ya Biblia inayoitwa New World Translation. Kwa kufanya hivyo, maoni yangu huthibitishwa tena na tena kwamba tafsiri hii imejitahidi sana kuelewa maandishi kwa usahihi kadiri iwezekanavyo.”

  •   Baada ya kufanyia uchunguzi tafsiri tisa kuu za Biblia, Jason David BeDuhn, profesa wa masomo ya dini, aliandika hivi: “[Tafsiri ya Ulimwengu Mpya] ndiyo tafsiri sahihi zaidi ikilinganishwa na hizo nyingine.” Ingawa wasomi wengi na watu kwa ujumla wanafikiri kwamba tofauti iliyopo katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya na Biblia nyinginezo inatokana na kwamba watafsiri wa Biblia hiyo waliingiza imani zao za kidini, BeDuhn alisema hivi: “Tofauti kubwa zilizopo zinatokana na kwamba NW [Tafsiri ya Ulimwengu Mpya] inatafsiri kwa usahihi na kwa uangalifu maneno ya waandikaji wa kwanza wa Agano Jipya.”​—Truth in Translation, ukurasa wa 163, 165.

^ Maelezo haya yanahusu Biblia za Kiingereza za awali za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, si toleo la 2013.

^ Kwa mfano, chunguza Biblia ya Union Version. Mistari iliyoongezwa ni Mathayo 17:21; 18:11; 23:14; Marko 7:​16; 9:​44, 46; 11:26; 15:28; Luka 17:36; 23:17; Yohana 5:4; Matendo 8:​37; 15:34; 24:7; 28:29; na Waroma 16:24. Tafsiri ya Union Version ina kifungu cha maneno yanayounga mkono fundisho la Utatu kwenye 1 Yohana 5:​8, 9, kifungu cha maneno ambacho kiliongezwa miaka mingi baada ya Biblia kuandikwa.