Hamia kwenye habari

Faraja na Msaada kwa Wagonjwa

Faraja na Msaada kwa Wagonjwa

Watu wagonjwa sana wanaweza kuwa na mahangaiko, na wakilazwa hospitalini, wanahisi vibaya hata zaidi. Jarida fulani la kitiba liliripoti, “uchunguzi unaonyesha kwamba mahitaji ya kihisia na ya kiroho yanaathiri sana afya ya mgonjwa.” *

Ili kukidhi mahitaji hayo, Mashahidi wa Yehova wanaandaa faraja ya kiroho na msaada kwa Mashahidi wenzao walio hospitalini. Wazee huchukua hatua ya kwanza kuwatembelea washiriki wa kutaniko lao ambao ni wagonjwa. Lakini namna gani ikiwa Shahidi anatibiwa mbali na nyumbani? Katika majiji makubwa ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova wamepanga Vikundi vya Kuwatembelea Wagonjwa (PVG). Wazee wa kutaniko katika vikundi hivyo wanawatembelea kwa ukawaida wagonjwa Mashahidi walio hospitalini pamoja na familia zao ambao wametoka maeneo mengine ya nchi au hata kutoka nchi nyingine, ili wapate matibabu. Kuna wajitoleaji zaidi ya 28,000 katika vikundi 1,900 hivi vya PVG katika mabara sita. *

PVG zinaandaa faraja gani ya kiroho?

William, ambaye ni mshiriki wa PVG anasema hivi: “Nimewafariji Mashahidi na washiriki wa familia zao ambao si Mashahidi kwa kuwatembelea, kuongea nao, na kuwasikiliza. Ninawahakikishia kwamba Yehova Mungu anaelewa hali yao na kwamba anawajali. Wagonjwa na familia zao wanathamini unaposali kwa ajili yao.”

Wengi wamethamini jinsi walivyotiwa moyo na vikundi hivyo. Ifuatayo ni mifano michache kutoka Marekani ambako kuna washiriki 7,000 hivi wanaowatembelea wagonjwa.

  • Priscilla alisema: “Asanteni kwa kumtembelea baba yangu akiwa hospitalini baada ya kupatwa na kiharusi. Aliguswa moyo sana na ziara zenu! Alishangaa kujua kuna uandalizi kama huo. Nafikiri ziara zenu zilimfanya apone haraka zaidi.”

  • Ophilia, binti ya mgonjwa ambaye alikufa, alimwambia hivi mshiriki wa PVG: “Mama alithamini sana kwamba mlimtembelea! Alijua kwamba Yehova ndiye aliyewatuma. Asanteni kwa kutujali kwa upendo.”

  • Mgonjwa mmoja alihangaika na kuvunjika moyo aliposikia kwamba alikuwa na siku chache tu za kuishi. James, mshiriki wa PVG, alikaa naye na kumpa faraja iliyo katika Andiko la Wafilipi 4:​6, 7. James anasema: “Nilipomtembelea siku iliyofuata, mtazamo wake ulikuwa umebadilika kabisa. Licha ya kujua hali yake, sasa alikuwa na mtazamo mzuri kuelekea msaada aliopata kutoka kwa Yehova, na hata yeye ndiye aliyenitia moyo!”

PVG zinatoa msaada gani?

Pauline, ambaye mume wake alikufa wakiwa mbali na nyumbani kwao, aliandika hivi: “Asanteni sana kwa msaada mliotupa wakati huu wenye mkazo mwingi sana katika familia yetu. Kujua kwamba mngekuwa hospitalini usiku wa manane, hata ingawa mlihitaji kwenda kazini siku iliyofuata kulitufariji sana. Asanteni kwa kupanga sote 11 tupate sehemu za kulala na kuwasiliana nasi kila hatua. Namshukuru Yehova na tengenezo lake kwa kuandaa msaada huu wa kutufariji.”

Nicki, Gayle, na Robin walipata aksidenti kilomita 300 hivi kutoka nyumbani. Carlos, mshiriki wa PVG, aliambiwa kuhusu hilo na alikuwepo hospitalini walipofika. Carlos anasema, “Niliwaambia niko tayari kufanya chochote walichohitaji, na niliishia kumshika mbwa mdogo wa Nicki ili yeye aweze kuingia ndani kupata matibabu.” Baadaye Curtis, mshiriki mwingine wa PVG, alifika pamoja na mke wake. Walikaa hospitalini hadi washiriki wa familia za wagonjwa walipofika saa kadhaa baadaye. Mtu aliyewaona alisema hivi: “Wote watatu walifarijiwa na jinsi walivyotunzwa. Lakini Robin, dada ya Nicki ambaye si Shahidi alishangazwa na msaada wote ambao washiriki wa PVG walitoa.”

^ fu. 2 Makala yenye kichwa, “Kushughulikia Mahitaji ya Wagonjwa ya Kihisia na Kiroho,” iliyochapishwa katika jarida The Joint Commission Journal on Quality and Patient Safety, Desemba 2003, Buku la 29, Na. 12, ukurasa wa 661.

^ fu. 3 Kama wazee wote wa Mashahidi wa Yehova, wale walio katika PVG husaidia pia katika makutaniko yao wakiwa wachungaji wa kiroho, walimu, na waeneza injili. Hawalipwi kwa huduma hizo, lakini wanazitoa kwa utayari na kwa hamu.​—1 Petro 5:2.