Hamia kwenye habari

Walimu Nchini Filipino Watambua Manufaa ya JW.ORG

Walimu Nchini Filipino Watambua Manufaa ya JW.ORG

Mwaka wa 2016, Mashahidi wa Yehova walikuwa na pendeleo la kukionyesha kikundi cha walimu katika Mkoa wa Zamboanga del Norte, nchini Filipino thamani ya video na makala katika tovuti ya jw.org kuhusiana na kufundisha. Kwanza Mashahidi walitembelea Idara ya Elimu ya mkoa katika mji mkuu ulioko jijini Dipolog. Wasimamizi walishangazwa sana na jw.org hivi kwamba wakawaalika Mashahidi wawasilishe habari yao kwa dakika 30 mbele ya walimu ambao wangehudhuria semina tatu zilizofuata ambazo zilihusisha walimu kutoka katika manispaa mbalimbali za eneo la Zamboanga del Norte.

Waliwasilishaje habari yao?

Mashahidi waliwaonyesha walimu 300 hivi waliokuwepo kwenye kila semina video walizochagua na makala zilizopo kwenye Tovuti. Wahudhuriaji walifurahia sana mada hii, “Kukabiliana na Madeni.” Walimu wengi walihisi kwamba mambo hayo yangewanufaisha si wanafunzi pekee bali hata wao pia. Wote walifurahia kupokea nakala ya trakti yenye kichwa Tutapata Wapi Majibu ya Maswali Muhimu Maishani? ambayo inaelezea kwa kifupi habari nyingi na zenye manufaa ambazo zinapatikana kwenye jw.org. Baadhi ya walimu pia walipakua video kutoka katika tovuti.

Matokeo ya maonyesho hayo matatu yalikuwa mazuri sana kiasi kwamba Idara ya Elimu ya mkoa ilipanga habari ziwasilishwe tena ili kuwasaidia washauri na walimu wengine 600 hivi. Kwa mara nyingine tena, wengi walishukuru sana kwa unyoofu.

“Tovuti inasaidia sana”

Baadhi ya wahudhuriaji walieleza baadaye jinsi habari hizo na tovuti ilivyowasaidia. Mwalimu mmoja alisema hivi: “Ningependa kuwashukuru kwa kuwa nimegundua kwamba tovuti hii inafaa sana kuwafundisha wanafunzi wangu.” Mwalimu mwingine alisema hivi: “Nimejifunza mambo mengi, hasa jinsi ya kukabiliana na mkazo. Tovuti hii inasaidia sana, si vijana tu bali pia watu wazima.”

Walimu zaidi ya 350 waliohudhuria maonyesho hayo ya jw.org waliomba wapate habari zaidi. Mashahidi walikubali maombi yao kwa kuwaonyesha ushauri unaofaa kutoka katika Biblia.

Mashahidi wa Yehova wanafurahi kwamba zaidi ya walimu 1,000 walihudhuria maonyesho ya jw.org katika eneo la Zamboanga del Norte na walimu hao walijifunza jinsi tovuti ya jw.org inavyoweza kuwa chanzo kizuri cha ufundishaji. Kifaa hiki chenye thamani cha kufundishia kinaweza kunufaisha walimu ulimwenguni pote kwa kuwafundisha kuwa na maadili mazuri na kupata mwongozo wa kiroho. *

^ fu. 9 Taasisi za elimu nchini Filipino zimepewa wajibu si tu kuwapa wanafunzi ujuzi bali pia “kuimarisha viwango vya maadili na vya kiroho [na] kuboresha maadili mema na nidhamu.”​—Katiba ya Mwaka wa 1987 ya Jamhuri ya Filipino, Kifungu cha XIV, Sehemu ya 3.2.