Hamia kwenye habari

Majumba ya Ufalme Yajengwa kwa Ajili ya Mashahidi Milioni Moja

Majumba ya Ufalme Yajengwa kwa Ajili ya Mashahidi Milioni Moja

Kati ya mwaka wa 1999 na 2015, Mashahidi wa Yehova walijenga zaidi ya Majumba 5,000 ya Ufalme katika Amerika ya Kati * na Mexico. Ili kutosheleza mahitaji ya Mashahidi milioni moja na wengine wanaohudhuria mikutano yetu katika eneo hili, zaidi ya Majumba mengine 700 ya Ufalme yanahitajika.

Zamani ilikuwa vigumu kwa makutaniko katika eneo hili kujenga sehemu za ibada. Kwa mfano, idadi kubwa ya Mashahidi nchini Mexico walifanya mikutano yao kwenye nyumba binafsi. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba kwa miaka mingi sheria haikuruhusu mashirika ya kidini kumiliki majengo. Hata hivyo, katika miaka ya 1990, sheria hiyo ilibadilishwa na Mashahidi wa Yehova wakaanza kujenga Majumba mengi ya Ufalme. Lakini bado ujenzi wa Jumba la Ufalme ulichukua miezi kadhaa.

Ujenzi Waendelea kwa Kasi

Kasi ya ujenzi iliongezeka mwaka 1999, wakati ambapo Vikosi vya Ujenzi wa Majumba ya Ufalme vilianzishwa chini ya mpango mpya wa kujenga Majumba ya Ufalme katika nchi zilizo na uwezo mdogo kifedha, kutia ndani Mexico na nchi saba za Amerika ya Kati. Tangu 2010, ofisi ya tawi nchini Mexico inasimamia kazi za ujenzi katika nchi hizo zote.

Watumishi wa ujenzi wanakabili changamoto za pekee wanapojenga Majumba ya Ufalme katika maeneo ya mbali. Kwa mfano, watumishi wa ujenzi nchini Panama walihitaji kusafiri kwa mashua kwa saa tatu kando ya pwani ya bahari ili kufika katika mradi mmoja wa ujenzi. Na katika jimbo la Chiapas nchini Mexico, kikosi cha ujenzi kilihitaji kutumia ndege ndogo ili kusafirisha vifaa vya ujenzi katika eneo moja la mbali.

Faida za Majumba Mapya ya Ufalme

Hata watu ambao si Mashahidi wa Yehova wanafurahi kuona Majumba mapya ya Ufalme katika maeneo yao. Kwa mfano, mwanamume mmoja nchini Honduras alisema kwamba kabla ya Mashahidi kujenga Jumba la Ufalme katika eneo aliloishi, watu wengine walitaka kutumia kiwanja hicho kujenga klabu ya usiku. Lakini yeye hakutaka hilo. Mashahidi wa Yehova walipomwambia wanataka kujenga Jumba la Ufalme hapo, alijibu: “Hiyo ni baraka iliyoje!”

Katika sehemu nyingi, watu wanapendezwa na bidii ya wajenzi hao. Mwanamume mmoja nchini Guatemala alisema hivi: “Katika utamaduni wetu, mara nyingi wanawake hufanya kazi za jikoni tu. Lakini hapa wanawake wanafanya kazi kama tu wanaume. Ninashangaa kuona wanawake wakiunganisha vyuma na kupiga kuta plasta. Inapendeza sana!” Baadhi ya majirani wamechochewa kununua chakula na viburudisho kwa ajili ya wajenzi.

Pia, watu wengi wamevutiwa na muundo wa Majumba yetu ya Ufalme. Nchini Nikaragua, injinia mmoja alimwambia meya wa jiji moja kwamba Jumba la Ufalme la eneo hilo lilikuwa jengo maridadi lililojengwa kwa kutumia vifaa bora zaidi. Isitoshe, alisema kwamba lilikuwa jengo lililojengwa kwa njia bora zaidi katika jiji lote!

Bila shaka, Mashahidi wa Yehova wanafurahi sana kuwa na sehemu zinazofaa kufanyia ibada. Wametambua kwamba kuna uwezekano mkubwa wa wanafunzi wao wa Biblia kuhudhuria mikutano baada ya Jumba jipya la Ufalme kujengwa. Washiriki wa kutaniko nchini Mexico waliosaidiana na watumishi wa ujenzi katika kujenga Jumba moja la Ufalme walisema hivi kwa shukrani: “Tunamshukuru Yehova kwa pendeleo tulilopata la kujenga Jumba la Ufalme linalotukuza na kulipa heshima jina lake.”

^ fu. 2 Kamusi Merriam-Webster’s Collegiate Dictionary, chapa ya 11, inaeleza kwamba Amerika ya Kati inatia ndani nchi ya Guatemala, El Salvador, Honduras, Nikaragua, Kosta Rika, Panama, na Belize.