Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

Unipatie tu Mwaka Moja wa Amani na Furaha

Unipatie tu Mwaka Moja wa Amani na Furaha
  • ALIZALIWA MWAKA WA: 1971

  • INCHI: UFARANSA

  • ALIKUWA: MUTU MWENYE JEURI, ALIKUWA ANAFANYA UASHERATI NA KUTUMIA DAWA ZA KULEWESHA

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Familia yangu iliishi Tellancourt, kijiji chenye kuwa kaskazini-mashariki mwa Ufaransa. Baba yangu alikuwa Mufaransa, na mama yangu ni Muitaliano. Wakati nilikuwa na miaka 8, tulihamia katika eneo fulani la muji wa Roma, inchi ya Italia, lenye lilikuwa na watu masikini waliofanya kazi za mikono. Huko, maisha yakakuwa magumu. Wazazi wangu walikuwa wanabishana kwa ukali sana kwa sababu ya magumu yao ya feza.

Wakati nilikuwa na miaka 15, mama yangu alinitia moyo nitafute marafiki. Kwa hiyo, nilianza kufanya muda murefu sana bila kuwa nyumbani. Bila kukawia, nilipata marafiki wabaya. Siku moja, mwanaume fulani mwenye alionekana kuwa rafiki, alinikaribia. Alinipatia dawa za kulewesha, na nikazitumia kwa sababu nilipenda nionekane kuwa nimekomaa. Mara moja, nilijiingiza katika maisha ya dawa za kulewesha na uasherati. Mara nyingi, nililalwa kinguvu. Maisha hayakukuwa tena na maana kwangu; sikuhangaikia kuishi wala kufa. Nilijisikia peke yangu sana. Wakati nilikuwa na miaka 16, nilipima kujiua kwa kunywa chupa ya wiski na kujitupa katika bahari. Hilo lilifanya nipoteze ufahamu kwa siku tatu.

Nilianza kuona uzima kuwa wa maana, lakini nikakuwa mwenye jeuri na mujanja. Nilikuwa ninaomba watu nifanye nao uasherati, nilikuwa ninawapatia dawa za kulewesha katika nyumba zao, na kisha niliiba kila kitu cha maana katika nyumba zao. Mashirika makubwa ya watenda-mabaya yalinitumikisha ili kuuzisha dawa za kulewesha mahali mbalimbali katika Italia. Mara nyingi nilikuwa na shida na polisi. Maisha yangu yalionekana kuwa na kusudi. Hata hivyo, niliamini kuwa hayakukuwa na maana na muongozo. Nilisali kwa Mungu ili anipatie tu mwaka moja wa amani na furaha.

BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU:

Wakati nilikuwa na miaka 24, niliamua kuhamia katika inchi ya Uingereza. Kwa sababu ya kujiunga na wafanyabiashara wa dawa za kulewesha, maisha yangu yalikuwa katika hatari. Mbele ya kuenda, nilitembelea mama yangu na nilishangaa kumukuta mwanaume mumoja mwenye kuitwa Annunziato Lugarà anazungumuza naye juu ya Biblia. * Kwa sababu nilijua kama alikuwa mutu mubaya sana, niliogopa na nikamuuliza sababu gani alikuwa hapo. Aliniambia kuhusu mabadiliko yenye alikuwa amefanya katika maisha yake ili akuwe Shahidi wa Yehova, na alinifanya niahidi kama nitazungumuza na Mashahidi wakati nitafika Uingereza. Niliitika kufanya hivyo. Lakini, wakati nilifika Uingereza, bila kukawia nilirudilia maisha yangu ya zamani.

Siku moja, nilikutana na Shahidi fulani mwenye alikuwa anapatia watu magazeti Munara wa Mulinzi na Amuka! katika barabara moja ya Londres yenye ilikuwa na watu wengi. Wakati nilikumbuka ahadi yenye nilifanya kwa Annunziato, nilimuomba Shahidi huyo ikiwa angeweza kunifundisha Biblia.

Mambo yenye nilijifunza katika Biblia yalinishangaza kweli. Kwa mufano, nilichochewa na andiko la 1 Yohana 1:9, lenye kusema hivi juu ya Mungu: ‘Tukiungama zambi zetu, yeye ni muaminifu na muadilifu [mwenye haki] hata atusamehe zambi zetu na kutusafisha.’ Andiko hilo lilinigusa moyo kabisa, nilijiona kuwa muchafu sana kwa sababu ya maisha yangu. Bila kukawia, nilianza kuenda kwenye mikutano katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Mashahidi walinikaribisha kwa uchangamufu. Wakati niliona urafiki wa sana wenye walikuwa nao, jambo lenye nilikuwa ninatamani tangu zamani, nilipenda kuwa katika kutaniko lao lenye kuwa kama familia.

Hata kama sikukuwa na magumu ya kuacha dawa za kulewesha na uasherati, ilikuwa vigumu sana kubadilisha tabia zangu. Niliona kama nilipaswa kutendea watu kwa heshima na kuwaona kuwa wa maana. Kwa kweli, ninaendelea kupiganisha tabia fulani za mubaya. Lakini, kupitia musaada wa Yehova, nimefanya maendeleo. Kisha kujifunza Biblia kwa miezi sita, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Ilikuwa katika mwaka wa 1997.

FAIDA YENYE NIMEPATA:

Kisha kubatizwa, nilioa Barbara, kijana mwanamuke mwenye pia alitokea tu kuwa Shahidi wa Yehova. Wakati rafiki yangu mumoja wa zamani aliona namna nilibadilika, alianza kujifunza Biblia. Kisha wakati fulani, alifikia kuwa Shahidi wa Yehova, na dada yake mukubwa akafanya hivyo pia. Tena, dada ya tate (nkambo) yangu mwanamuke, mwenye alikuwa na zaidi ya miaka 80, alianza kujifunza Biblia na akabatizwa mbele ya kufa.

Leo niko muzee katika kutaniko moja la eneo letu, na mimi na bibi yangu tuko wahubiri wa wakati wote, tunafundisha Biblia watu wenye kusema luga ya Kiitaliano katika muji wa Londres. Wakati fulani, ninahuzunika juu ya maisha yangu ya zamani, lakini Barbara ananisaidia sana. Mwishowe, niko na maisha ya muzuri ya familia yenye nilitamani sikuzote, na niko na Baba mwenye upendo mwenye nilitaka sikuzote kuwa naye. Nilimuomba Mungu anipatie tu mwaka moja wa amani na furaha, lakini amenipatia mengi zaidi!

Mwishowe, niko na maisha ya muzuri ya familia yenye nilitamani sikuzote, na niko na Baba mwenye upendo mwenye nilitaka sikuzote kuwa naye

^ fu. 10 Soma habari “Biblia Inabadilisha Maisha ya Watu—Nilikuwa na Bunduki Yangu Kila Mahali Nilienda” yenye ilielezwa na Annunziato Lugarà, katika gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 01/07/2014, ukurasa wa 8-9.